HOTUBA YA MHE. JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA NA MWENYEKITI MPYA WA CCM KWENYE MKUTANO MKUU WA SABA WA CHAMA CHA MAPINDUZI, CHIMWAGA – DODOMA, 25 JUNI 2006

 

 

Ndugu Mwenyekiti Mstaafu, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa;

 Mwenyekiti Mstaafu, Ali Hassan Mwinyi

Ndugu zangu, wanachama wenzangu,

 

Nimesimama kutoa shukrani kwenu wajumbe wenzangu wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa Chama chetu kwa uamuzi wenu wa kunichagua tena kwa kishindo,  kuwa Mwenyekiti wa Nne wa Chama Cha Mapinduzi.  Natafuta maneno mazuri ya kuelezea

 

//shukrani zangu

 

 

shukrani zangu kwenu lakini Kiswahili hakina maneno zaidi ya Ahsanteni Sana.

Kwa mara nyingine tena natoa shukrani zangu  za dhati kwa Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama chetu kwa imani yao kwangu na hivyo kuamua kunileta mbele yenu kwa uchaguzi huu mlioufanya leo.

          Namshukuru kwa namna ya kipekee mzee wangu na mwalimu wangu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sasa Mwenyekiti Mstaafu wa Chama chetu.  Kwanza namshukuru kwa kunilea na kunilinda mpaka nimefika hapa.  Alikuwa mwalimu wangu wa masuala ya diplomasia kwa kipindi chote cha miaka 10 nilichokuwa Waziri wake wa Mambo ya Nje.  Nimeingia wizarani nikiwa sijui

//chochote kuhusu

 

 

 chochote kuhusu masuala ya uhusiano wa kimataifa lakini nimeondoka nikiwa nimehitimu. Na, hata kabla ya hapo tulipokuwa wote katika Baraza la Mawaziri ambapo mimi nilipojiunga nilimkuta yeye ni Waziri Mwandamizi alinisaidia kwa mengi.  Lakini, pia nilijifunza mengi kuhusu Ubunge na uongozi wa ngazi za mwanzo kutoka kwake kule Wilayani Masasi wakati nilipokuwa Katibu wa CCM wa Wilaya na yeye akiwa Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu. 

Pili, namshukuru sana kwa imani yake na mapenzi yake kwangu  wakati wa mchakato, baada ya uteuzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.

//Na sasa nikiwa Rais,

 

Na sasa nikiwa Rais,  amekuwa mshauri wangu wa kutumaini.  Ni mtu mwepesi na hana taabu ninapomuomba ushauri na msaada kwa jambo lolote ninapoona anaweza kunisaidia. Sina shaka kwamba hata kwa masuala ya Chama nayo ataniwekea milango yake wazi ili niweze kuchota kutoka kwenye hazina yake kubwa ya busara, hekima na maarifa.

          Ushahidi mwingine mkubwa wa upendo na imani yake kwangu, ni uamuzi wake wa kuacha Uenyekiti kabla ya wakati wake na kunipendekeza mimi nichukue nafasi hiyo.  Ni imani iliyoje kwangu mtu anayoweza kuionyesha zaidi ya hii.  Aliponiambia Februari, 2006 kuwa ameamua kuacha Uenyekiti na kuniachia, nilimwambia kuwa naona ilikuwa mapema mno, mimi ningependa kwanza

//nipate nafasi

 

nipate nafasi ya kujiimarisha katika Serikali kabla ya kuchukua Uongozi wa Chama. Nakumbuka kumwambia “Unajua Mzee nina miezi miwili tu sina haraka, endelea mpaka 2007”.  Mzee Mkapa akanijibu

 kuwa na yeye alipokea hivyo hivyo kutoka kwa Mzee Mwinyi.  Alisisitiza kuwa huu ni utaratibu mzuri, ni bora kuudumisha. Akanisihi kuwa nikubali maombi yake.  Nikamjibu sawa ila “siyo sasa”. Akaniambia:  “Haitakuwa ghafla” na hata Mzee Mwinyi alimkabidhi zaidi ya miezi sita baada ya kuchaguliwa, hivyo alidhani mwezi Juni ungekuwa wakati muafaka.  Nikamwambia “Ndiyo Mzee!”.  Muafaka ukafikiwa na  maelewano yetu hayo ndiyo yamezaa shughuli hii ya leo.

// Waheshimiwa Wajumbe;

         

 

 

 

Waheshimiwa Wajumbe;

          Nilipokuwa namuomba Mwenyekiti Mkapa aendelee mpaka 2007 nilifanya hivyo sio kwa sababu ya kutokujiamini kumudu madaraka ya Mwenyekiti wa Chama bali ni kutokana na kutaka kujipa nafasi ya kujijenga na kujiimarisha katika kazi kubwa mliyonipa ya kuongoza Serikali.  Nimeikubali haja ya kuunganisha kofia sasa.  Naukubali mzigo huu mpya kwa moyo mkunjufu na bila ya hofu. 

Nasema sina hofu kwa sababu ninyi wenzangu mpo.  Ninyi wenye Chama chenu mpo tena mna hamasa kubwa.  Jirani zangu Wazigua wanao msemo maarufu usemao, “Zumbe ni wan’tu” maana yake ni kwamba, “kiongozi ni watu”.  Hali kadhalika Mwenyekiti wa Chama ni wanachama.  Maadamu

//wanachama wa CCM

 

wanachama wa CCM wapo na viongozi na makada wake wapo tena walio imara, sioni sababu kwa nini nisifanikiwe katika kazi yangu ya Uenyekiti.  Mzee Malecela yupo. Rais Karume yupo. Hali kadhalika Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ipo. Sekretariet yenye uwezo wa kiutendaji ipo. Siwezi kushindwa.

Sababu nyingine inayonipa imani kuwa mzigo huu unabebeka “hata na mie ambaye si Mnyamwezi”, ni ule ukweli kwamba narithi Chama imara, chenye wanachama na viongozi wenye msimamo, mshikamano na hamasa ya hali ya juu.  Chama ambacho ni imara kwa muundo wake na bora kwa sera zake.  Chama ambacho kimeweka misingi endelevu ya kupata viongozi na kubadilishana uongozi wa juu bila ya kelele wala mikwaruzo.  Sote

//tunaona mchakato

 

tunaona mchakato huu unavyofanyika katika mazingira ya utulivu na upendo.  Tumeona pia kwa namna gani hata mchakato wenye ushindani mkubwa kama ule wa kutafuta Mgombea Urais ulivyoendeshwa na kumalizika salama. Tulianza kumi na moja na mitandao kumi na moja lakini sasa tuko wamoja, kitu kimoja na mtandao mmoja tu wa CCM.  Waliodhani kuwa Chama chetu kingemeguka walitahayari. Hata kura zilizopigwa zinathibitisha ukweli huo. Tamaa ya fisi tu, mkono wa mwanadamu haukudondoka.

Tuimarishe Chama Chetu

Ndugu Wajumbe;

          Pamoja na ukweli huo, kuhusu uimara na ubora wa Chama chetu natambua hoja na haja ya kuchukua hatua zaidi za kukiimarisha na kukiboresha zaidi

//Chama Cha Mapinduzi.

 

Chama Cha Mapinduzi.  Ni makusudio yangu kushirikiana kwa karibu na wanachama wenzetu na ninyi viongozi wenzangu katika kufanikisha kazi hii muhimu.

Ndugu Wajumbe;

          Chama imara ni kile ambacho viungo vyake vimekamilika na vinafanya kazi vizuri.  Chama ni wanachama, viongozi, vikao, watendaji, rasilimali na Jumuiya za Chama. 

          Kukamilika kwa viungo vyote hivyo na kwa kila kiungo kuwa kinafanya kazi ipasavyo, ndio uimara wa Chama Cha Mapinduzi.  Kwanza kabisa, hatuna budi kuhakikisha kuwa wanachama wa Chama chetu ni madhubuti, wanaongezeka kwa idadi na kwamba wako mstari wa mbele kukitetea na kukipigania Chama chao.  Wanachama wanaotimiza ipasavyo

//wajibu wao

 

wajibu wao wa kikatiba.  Wanaolipa ada zao kwa wakati, wanaotoa michango yao na kushiriki kwa ukamilifu vikao vya Chama vinavyowahusu na shughuli mbalimbali za Chama.  Naomba kwa pamoja tupime ubora wa kiungo hiki na kubaini mapungufu yaliyopo na kuyarekebisha.

Wajumbe wenzangu,Wajumbe wenzangu;

            Katika kuimarisha Chama chetu hatuna budi tuhakikishe kuwa kiungo cha viongozi kiko imara kweli kweli. Safu za Uongozi ziwe zimekamilika ipasavyo, hakuna mapengo na kwamba viongozi hao wako mstari wa mbele kutimiza wajibu wao wa uongozi.  Kiongozi ndiye mwonyeshaji njia, lazima viongozi wa Chama Cha Mapinduzi tuifanye kazi hiyo kwa umahiri mkubwa.  Viongozi pia lazima waongoze kwa mfano na siyo kwa maneno.  Kauli za

//fuata maneno

 

fuata maneno yangu usijali matendo hazina nafasi katika uongozi wa Chama cha watu. Tuseme tunayotenda ili tujenge moyo kwa watu kutuamini. 

Kwa vile Chama chetu ni Chama tawala, viongozi wetu wanao wajibu wa kuifanya kazi hiyo ndani ya Chama na nje ya Chama ndani ya Umma.  Ni ukweli usiofichika kwamba, viongozi wa Chama chetu hawaifanyi vya kutosha kazi ya uongozi miongoni mwa umma.  Wakati mwingine ukitulinganisha na viongozi wa vyama vya upinzani, viongozi wa Chama Cha Mapinduzi hatufanyi sana mikutano ya hadhara na umma.  Mikutano ya hadhara ni nyenzo ya kuwavutia watu upande wetu.  Inatoa fursa ya kufafanua masuala mbalimbali yahusuyo sera na siasa ya Chama chetu.  Naomba wenzangu tubadilike ili tuzuie upotoshaji na

//kuhakikisha kuwa

 

kuhakikisha kuwa wananchi wanapata ukweli wa mambo kutoka midomoni mwetu.

          Tutaendelea kuhimizana kuhusu kuzingatia  jambo hili muhimu.  Kadhalika tutalipa umuhimu unaostahili suala la mafunzo ya viongozi na makada wetu.  Kwa ajili hiyo tutafuatilia kwa karibu uamuzi wa NEC wa kuwa na Chuo cha Chama pale Ihemi, Iringa.  Baada ya muda si mrefu tutaanza kuchukua hatua za utekelezaji wake.

Waheshimiwa Wajumbe wenzangu;

          Kama tulivyosikia katika taarifa ya Chama kuwa hali ya ufanyikaji wa vikao vya Chama siyo nzuri hasa kwa ngazi za mwanzo za Chama chetu.  Huko ndiko waliko wanachama na huko ndiko kiliko Chama.  Hivyo udhaifu huu ni jambo lisilofurahisha hata kidogo.  Hatuna budi tubadilike. Kama tujuavyo

//maamuzi ya Chama

 

maamuzi ya Chama hufanywa kwenye vikao tofauti na Serikali ambapo Rais, Waziri, Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya wanaweza kuamua  wenyewe bila vikao.  Katika Chama maamuzi hufanywa kupitia vikao na   hata Mwenyekiti wa Chama na viongozi wa Chama hawana maamuzi yao binafsi labda iwe kutelekeza maamuzi yaliyofanywa kabla au maagizo ya katiba na kanuni. 

Hivyo basi, kutokufanyika vikao vya Chama vya ngazi husika kunadhoofisha sana mfumo mzima wa maamuzi ndani ya Chama. Kutofanyika vikao kunaua dhana nzima ya demokrasia ya ndani ya Chama na dhana ya uongozi wa pamoja.   Wanachama na wajumbe wa vikao husika wawe wakali kudai kufanyika kwa vikao vya ngazi zao.  Naomba tubadilike ili kiungo hiki muhimu sana

//tukipe nafasi

 

tukipe nafasi stahiki ya uhai wake.

Ndugu Wajumbe;

          Watendaji ni kiungo cha msingi kabisa katika uhai na maendeleo ya Chama chetu.  Ndicho kiungo unganishi kwa shughuli zote za Chama.  Ndicho kiungo kitendaji cha Chama chetu.  Bila ya kiungo hicho mambo yetu yatakuwa mabaya au hayatowezekana.  Hatuna budi basi kukiangalia vizuri kiungo hiki.   Tuhakikishe kuwa Chama chetu kina watendaji waliokamilika ipasavyo kwa mujibu wa ikama. 

Watendaji wa Chama chetu wawe ni watu wenye ujuzi, maarifa  na uwezo wa hali ya juu wa kazi zao za kiutendaji. Aidha, ni wajibu wetu kuwawezeshea watendaji wetu kutimiza ipasavyo majukumu yao kwa maana ya mafunzo, zana na vifaa vya kazi. 

//Pamoja na hayo,

Pamoja na hayo, tuwatengenezee mazingira mazuri ya kufanyia kazi:  maofisini na katika hali ya maisha yao.

          Lakini, tunapozungumzia watendaji, zana na vitendea kazi vya Chama tunazungumzia suala zima la kujenga uwezo wa raslimali na kifedha wa Chama chetu ulio mkubwa zaidi kuliko ilivyo sasa. 

Ni lazima tukae chini kuzungumzia kujenga uwezo wa kifedha na rasilimali wa Chama chetu. Hili ni jambo la msingi sana.  Hakuna majawabu rahisi kuhusu nini na vipi tufanye, lakini lazima tufanye kwani hakuna badala yake. Tufanye hivyo katika kila ngazi ya Chama chetu. Nawaomba wenzangu kila kiongozi na kila mwanachama katika ngazi yake alipe suala hili uzito unaostahili.  Tuchune bongo zetu, tubuni mikakati, mbinu na mipango ambayo

//itakiingizia Chama

 

 itakiingizia Chama chetu fedha na kukipatia rasilimali za kufanyia kazi kwa uhakika. 

Waheshimiwa Wajumbe;

Nalisemea hili kwa sababu ya umuhimu wake na kwa sababu naamini wote tunautambua ukweli huo.  Sasa wakati umefika kwa Chama chetu kuondokana na maisha ya kutafuta fedha na rasilimali za kufanyia shughuli zake kwa taratibu za zimamoto.  Kufanya hivyo kuna hatari ya siku moja kujikuta moto umekuwa mkubwa mno na hauzimiki kwa urahisi.  Lakini jambo baya zaidi ni hatari ya  kuhusishwa na watu tusiokuwa na uhakika nao na kupata hatari ya  kuishia kupata fedheha.

Waheshimiwa Wajumbe;

          Jumuiya za Chama ni kiungo chenye nafasi ya pekee kwa Chama chetu.  Jumuiya ziliundwa kwa nia

//ya kukisogeza Chama

 

ya kukisogeza Chama chetu karibu na umma wa Watanzania.  Ni chombo kilichoundwa kukipatia Chama chetu wanachama, marafiki, wapenzi na washabiki miongoni mwa makundi mbalimbali ya jamii pana ya Watanzania.  Na kwa wakati huu siasa ya vyama vingi jumuiya ni chombo muhimu cha kukitafutia Chama chetu kuungwa mkono na Watanzania walio wengi wakati wa uchaguzi.  Hivyo basi kwa Jumuiya za Chama Cha Mapinduzi kuwa imara ni jambo ambalo halina mjadala.

 Naomba wana CCM wenzangu tuelewe hivyo. Hasa naomba viongozi na wanachama wa UWT, Vijana na Wazazi watambue umuhimu wao huo.  Naomba watambue kuwa, Jumuiya kuwa imara ni kwa maslahi mapana ya Chama chetu. Hatuna budi tufanye kila tuwezalo kuhakikisha kuwa Jumuiya

//zetu zinaimarishwa

 

zetu zinaimarishwa ipasavyo kwa ngazi zote.  Napenda kuitumia fursa hii kuwahakikishia wana CCM na wanachama na viongozi wa jumuiya zetu  ushirikiano wangu wa hali ya juu katika jitihada za kujenga na kuimarisha jumuiya zetu.

Ndugu Wajumbe wenzangu;

Leo tunakutana kwa mara ya kwanza tangu Mei Nne mwaka wa jana, wakati wa Mkutano Mkuu Maalum wa uteuzi wa Mgombea Urais kwa tiketi ya CCM. Pia, ni mara ya kwanza tangu uchaguzi kuisha. 

Kwa mara nyingine napenda kuwashukuru sana kwa imani na heshima kubwa mliyonipa ya kubeba bendera ya Chama chetu wakati wa Uchaguzi Mkuu wa Disemba mwaka wa jana.

Lakini, shukrani kubwa zaidi nazitoa kwa  kwenu kwa jinsi mlivyokipigania Chama chetu

//wakati wa kampeni

 

wakati wa kampeni na kukiwezesha kupata ushindi mnono ambao umewashangaza wengi. Nimeiona nguvu ya viongozi, wanachama na makada wa Chama wanapoamua kukipigania Chama chao.  Hakuna mfano wake.

Nakosa maneno mazuri ya kuelezea shukrani na pongezi zangu kwenu kwa jitihada zenu kubwa zilizokipatia ushindi mkubwa sana Chama chetu. Ushindi tulioupata ni matunda ya juhudi zenu kwa pamoja. Naomba mnikubalie tu wenzangu niseme tena Ahsanteni sana, tena sana. Nawashukuru na nawapongeza sana!

Ndugu zangu, Wajumbe wenzangu;

Mzee Mkapa alitukumbusha jana kuwa, mwisho wa uchaguzi mmoja ndiyo mwanzo wa uchaguzi mwingine. Maandalizi ya uchaguzi wa 2010

//yalitakiwa kaunza

 

yalitakiwa kuanza saa 10 jioni  siku ya tarehe 14 Desemba, 2005 baada ya kupiga kura. Hembu tujiulize:- Je, tumeanza au bado tunasherehekea ushindi?  Ndugu zangu tuanze sasa kwa kujenga na kuimarisha Chama chetu na kutafuta nyenzo na vifaa muhimu vya kuendeshea kampeni.  Wachina wana msemo “Jasho jingi wakati wa amani, damu kidogo wakati wa vita”.

Ndugu Wajumbe wenzangu;

Wakati tunazindua kampeni za uchaguzi za chama chetu pale Uwanja wa Jangwani, tarehe 21 mwezi wa nane mwaka jana, Mwenyekiti wetu wa CCM wa wakati ule, Mheshimiwa Benjamin William Mkapa, alinikabidhi Ilani ya Uchaguzi ya Chama chetu ili nikainadi kwa wananchi kwa niaba yenu.

//Kazi hiyo nimeifanya

 

Kazi hiyo nimeifanya kwa nguvu na uwezo wangu wote na ninyi wenzangu ni mashahidi. Tena, tumeifanya sote kwa ushirikiano na mafanikio makubwa.

Vilevile, siku ile  Mwenyekiti Mkapa alinikabidhi Ilani sio tu  kwa ajili ya kuinadi tu, bali pia iwe ndio dira ya Serikali ya Awamu ya Nne pindi wananchi watakapokuwa wametupa ridhaa ya kuwaongoza. Sasa Chama chetu kimekamata dola, na mchakato wa utekelezaji wa Ilani mliyotukabidhi tumeuanza. Tena tumeianza kazi hiyo kama kauli mbiu ya Chama Cha Mapinduzi inavyosema:  Kwa Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya.   

Katika kipindi chote ambacho tumekuwa madarakani, tumetumia kila mwanya kukumbusha na kusisitiza kwa watumishi wa umma kwamba Ilani

//ya CCM ndio dira

 

ya CCM ndio dira na mwongozo wa Serikali ya Awamu ya Nne, kama ambavyo Chama chetu na wananchi kwa ujumla wanategemea iwe.   Tumechukua hatua kadhaa kuhakikisha kwamba mipango, mikakati na program kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu inatokana na Ilani ya CCM.

Kwanza, katika mkutano wangu wa kwanza wa Baraza la Mawaziri niliwaagiza Mawaziri wote watengeneze mipango, mikakati na program za utekelezaji wa Ilani  ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi kwa mambo yanayohusu sekta zao.  Kila Waziri tulimpa nakala ya Ilani na kila Wizara tuliipa nakala kadhaa za Ilani.

Pili, nilifanya ziara katika Wizara zote na Idara mbalimbali za Serikali nikiwa nimebeba Ilani ya chama chetu mkononi. Nia yangu ilikuwa

//kuwakabidhi watumishi

 

kuwakabidhi watumishi wa umma Ilani hiyo na kuwakumbusha kwamba katika utumishi wao Serikalini wanao wajibu kutekeleza  Ilani ya Chama kilichopata ridhaa ya wananchi hata kama utashi na mapenzi yao ni vinginevyo. 

Ndugu Wajumbe;

Kwa ujumla, kama alivyosema Waziri Mkuu tumejipanga vizuri kutekeleza kauli mbiu ya uchaguzi ya chama chetu ya kuleta Maisha Bora kwa Kila Mtanzania. Naomba muendelee kutuunga mkono.

Ndugu Wajumbe;

Tumepanga kutekeleza kauli-mbiu hiyo ya Chama chetu kwa kuongeza na kuboresha huduma za kijamii na kiuchumi kwa Watanzania na kukuza

//kipato cha Watanzania

 

kipato cha Watanzania wakulima na wanyakazi walioko mijini na vijijini.  Kwa upande wa huduma mkazo utawekwa katika sekta za afya, maji, elimu, umeme, barabara n.k.

 Tumesikia maoni ya wajumbe wakati wa kuchangia taarifa za Serikali.  Tutayatafakari na kuyafanyia kazi. Kwa upande wa barabara, nimesikia sauti za Ruvuma, Kigoma na Tabora.  Tumepanga  kuweka msisitizo kwa barabara za maeneo ya mipakani ambayo bado hayajaunganishwa na sehemu nyingine za nchi yetu kwa kiasi cha kuridhisha.  Barabara za Ruvuma, Rukwa, Kigoma na Tabora zipo kwenye kipaumbele cha juu.  Mazungumzo na wafadhili yapo katika hatua mbalimbali. Daraja la Malagarasi mambo yake ni

//mazuri.

 

 

mazuri.  Hivyo hivyo kwa umeme.

Waheshimiwa Wajumbe;

 Mimi na wenzangu Serikalini tunatambua kuwa maisha bora kwa Watanzania yatawezekana tu kwa kuhakikisha kwamba kipato cha Watanzania kinaongezeka. Ndiyo, maana tumeamua kuweka mkazo maalum kwenye kuongeza tija na uzalishaji katika shughuli wanazojihusisha nazo Watanzania walio wengi ambazo ni kilimo, uvuvi na ufugaji. Tutaimarisha sekta zitakazochangia kukua kwa kilimo, hasa viwanda vya usindikaji wa mazao ya kilimo na kuzalisha bidhaa zinazotakiwa na sekta hiyo.

Ndugu zangu;

Katika suala la kilimo, ninalo ombi maalum kwenu, Viongozi wa CCM. Chama chetu kina historia

//ya muda mrefu

 

ya muda mrefu na ya kutukuka ya kuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha, kusukuma na kusimamia mageuzi ya kilimo nchini. Tulikuwa tukiwahamasisha wakulima wakati wa utayarishaji wa mashamba, kupanda, kupalilia, kuvuna na hata wakati wa kuhifadhi mazao. Chama chetu kilikuwa mstari wa mbele katika kutoa miongozo kwa wakulima wetu juu ya kanuni za kilimo bora. Lakini, siku hizi, majukumu haya ya msingi tumeyaacha. Matokeo yake ni maendeleo ya kilimo kurudi nyuma. 

Ndugu zangu, wanachama wenzangu na viongozi wenzangu, Tumewaahidi Watanzania mageuzi ya kilimo. Nawasihi turudie ule utaratibu wetu mzuri wa zamani. Lazima tufanye hivyo ili tufanikiwe katika azma yetu hii. Ilani hii ni yetu sote. Na, sote, katika Chama na Serikali, tutapimwa na

//wananchi kwa mafanikio

 

wananchi kwa mafanikio ya utekelezaji wake. 

Ndugu Wajumbe;

          Katika mikakati ya kuongeza kipato kwa Watanzania, lipo suala zima la kuwapatia ajira wasiokuwa na ajira. Tumeanza kuchukua hatua za kukuza ajira Serikalini. Vilevile tumeanza kuweka mazingira ya kuwawezesha vijana, wanawake na Watanzania kwa ujumla wanaotaka kujiajiri kufanya hivyo.  Waziri Mkuu atalifafanua vizuri zaidi kesho.  Ninachosema ni kuwa, tunajali na  tunaheshimu ahadi zetu.  Tunajiandaa pia kukuza uwekezaji ili tukuze ajira na kukuza uchumi.

Ndugu zangu, utekelezaji wa Ilani yetu unahitaji uwezo mkubwa wa kirasilimali wa Serikali. Tunafanya jitihada kuhakikisha kwamba uwezo huo unakuwepo. Tutahakikisha kwamba mapato ya

//Serikali yataendelea

 

 

Serikali yataendelea kukua. Vilevile, mimi na wenzangu Serikalini tunaendelea na juhudi za kujenga mahusiano mazuri na nchi wahisani, marafiki na mashirika ya Kimataifa ili tuendelee kupata misaada ya kutuwezesha kutekeleza mipango yetu. Nafurahi kwamba hadi sasa juhudi za Serikali yetu zimepokelewa vizuri duniani kote. Na kila nilipoenda kwenye ziara nje, nimepewa matumaini ya kuungwa mkono katika jitihada zetu.  La msingi zaidi katika kujenga uwezo wetu ni kuhakikisha kwamba uchumi wetu unakuwa mkubwa zaidi ili tuweze kujitegemea wenyewe. Hii lazima iwe azma yetu ya muda mrefu.

Kwahiyo, ndugu zangu, Ilani ya chama chetu iko katika mikono salama. Tutahakikisha inatekelezwa.

//Na, kwa kweli

 

Na, kwa kweli Bajeti yetu ya kwanza iliyopitishwa kwa kishindo na Bunge Jumatatu inathibitisha dhamira yetu ya kutekeleza yale tuliyoyaahidi katika Ilani ya Chama chetu.

Ni dhahiri kwamba yote tuliyoyaahidi hayataonekana kwenye bajeti ya mwaka huu. Ilani yetu ni ya miaka mitano na ahadi zetu tulizotoa zitatekelezwa ndani ya kipindi hicho.

Ndugu wajumbe wenzangu;

Leo hii tunajigamba juu ya uwezo wetu wa kutekeleza Ilani ya Chama chetu na kuendesha mambo yetu  kwa sababu moja kuu: nayo ni msingi mzuri  aliotujengea na kutuachia Rais wetu na Mwenyekiti wetu Mstaafu, Mhe. Benjamin William Mkapa.

Ndugu zangu, mkiniona natembea kifua mbele,

//kama ambavyo

 

kama ambavyo chama changu kinanitegemea niwe, mkiniona nasimama kwa kujiamini, kama ambavyo mwana-CCM anategemewa awe, ni kwamba nimesimama juu ya mabega ya miamba iliyonitangulia: Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mzee Ali Hassan Mwinyi na Mzee Benjamin William Mkapa.

Misingi aliyotuachia Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere inaifanya kazi yetu ya kudumisha na kuendeleza umoja, mshikamano na utulivu wa taifa letu iwe rahisi. Misingi aliyotuachia Mzee Mwinyi inaifanya kazi yetu ya kuhubiri uvumilivu wa tofauti zetu za kisiasa na kijamii isiwe ngumu. Na, misingi imara ya kiuchumi aliyotuachia Mzee Mkapa inalifanya jukumu la msingi la Serikali ya Awamu ya

//Nne- jukumu la kukuza

 

Nne – jukumu la kukuza uchumi, kuinua kipato cha Watanzania na kuwaletea maisha bora – liwezekane.

Ndugu zangu, sisi kama Serikali ya CCM, hatuanzi upya wala hatubomoi tulichokikuta. Tunaendeleza pale alipotuachia Rais Mstaafu Benjamin Mkapa. Na kwa kuwa aliiacha nchi yetu mahali pazuri, tumeanza kazi yetu vizuri. Tungetetereshwa sana na matatizo yaliyotukabili ya umeme, upungufu wa chakula na bei za juu za mafuta kama Mzee Mkapa hakuacha mfumuko wa bei ukiwa chini, akiba ya fedha za kigeni ikiwa kubwa, uchumi ukiwa unakua, uwekezaji unaongezeka na ukusanyi wa mapato ya Serikali ukiwa mzuri.

Mzee wetu Mkapa, umelifanyia Taifa letu kazi

//kubwa na nzuri

 

kubwa na nzuri  na umeiletea heshima kubwa nchi yetu. Tunakushukuru sana kwa utumishi wako uliotukuka. Pumzika ukitambua kwamba tunaufahamu, tunaujali na tutauenzi mchango wako kwa Taifa letu na kwa Chama chetu. Usituchoke tutakapoendelea kuja kuchota katika chemchem yako ya busara na hekima.

Kabla ya kumaliza naomba nisemee mahusiano na vyama vingine vya siasa nchini na nje ya nchi. Napenda kuwahakikishia kuwa, tutaendelea kujenga uhusiano mwema na vyama vyote vya siasa nchini na vyama rafiki nje ya nchi. Tunatambua umuhimu wa vyama vya siasa kwa kuendeleza demokrasia nchini mwetu.  Nawaahidi ushirikiano wa karibu.  Utaratibu aliouonyesha Mwenyekiti Mkapa wa mawasiliano na vyama vya siasa nitauendeleza kwa kasi mpya,

//nguvu mpya na ari mpya.

 

nguvu mpya na ari mpya. Tunajenga nyumba moja si busara kugombea fito.  Tutashindana wakati wa uchaguzi, ukiisha sote tujenge nchi yetu.

MWISHO

Ndugu Wajumbe;

            Leo najiona nimezaliwa upya katika historia ya maisha yangu na katika historia ya uanachama wangu kwa Chama chetu.  Nilipojiunga na utumishi wa Chama cha TANU Aprili 2, 1975 na kuanza kazi pale Singida sikujua na wala sikuotea kuwa hatimaye safari yangu ile iliyopitia Kisiwandui, Ofisi Ndogo, Tabora, Monduli, Nachingwea, Masasi na katika Umoja wa Vijana,  NEC na Kamati Kuu hatimaye  itanifikisha hapa nilipofikia leo. 

          Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sitatambua na kutoa neno la shukrani kwa Umoja wa Vijana wa

//TANU na Umoja

 

TANU na Umoja wa Vijana wa CCM. Umoja wa Vijana wa TANU na Umoja wa Vijana vilikuwa uwanja muhimu na darasa lililonipatia mbinu na maarifa ya Uongozi.  Kadhalika, lilikuwa darasa la kujifunzia siasa na sera za Chama na kuniandaa kuwa mwanachama wa TANU na CCM.

          Nawashukuru wazee na walezi wangu wa kisiasa hususan Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Mzee Rashid Kawawa, Mzee Ali Hassan Mwinyi kwa malezi mazuri.  Sitomsahau Mzee Pius Msekwa katika orodha hiyo.

Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia rehema zake. Na, nazidi kumuomba Mola wetu anijalie karama zake nimudu vyema majukumu ya Uenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na yale ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini, pia

//nawashukuru sana

 

nawashukuru sana Viongozi wangu na wanachama wenzangu wa TANU na sasa CCM kwa malezi yao, ushirikiano wao na msaada wao.  Bila ya ushirikiano huo nisingekuwa hivi nilivyo sasa. Nategemea kwa kiasi kikubwa ushirikiano wenu katika jukumu hili kubwa na zito la Uenyekiti wa Chama chetu. Kwa pamoja, tunaweza kukijenga, kukidumisha na kukiimarisha Chama chetu ili kiendelee kuwa tumaini na kimbilio la Watanzania. Naamini inawezekana.  Mwalimu Nyerere alipata kusema “it can be done, play your part”

Kwa mara nyingine, napenda kuwashukuru kwa imani kubwa mliyoinyesha kwangu.

Nawashukuru sana kwa kunisikiliza. Sasa, naufunga rasmi mkutano huu. Nawatakia safari njema ya kurejea nyumbani.

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI