| Taarifa
rasmi - Miaka 40 ya Mapinduzi SMS na SMT - Mapuri -
29.7.2003
Taarifa
rasmi - Sera ya Uzawa - Mapuri - 27.7.2003
Taarifa
rasmi - Miaka 40 ya Mapinduzi SMS na SMT - Mapuri -
29.7.2003
Katika
kikao chake cha tarehe 26-27 Julai, 2003, Kamati Kuu
ya Halmashari Kuu ya Taifa ya CCM ilijadili miongoni
mwa mengine, ujasiri wa Afro-Shirazi Party wa kuikomboa
Zanzibar kutoka makucha ya wakoloni wa Kiingereza na
utawala wa Masultani walowezi, tarehe 12 Januari, 1964.
Iliuthamini mchango mkuba wa mashujaa wa Mapinduzi hayo
chini ya uongozi wa Marehemu Mzee Abeid Amani Karume,
ambao walijitoa mhanga wa maisha yao kwa ajili ya uhuru
wa kweli wa Wazanzibari. Aidha Kamati Kuu ina fahari
kubwa kwamba ASP na hatimaye CCM imeweza kuyaendeleza
na kuyadumisha Mapinduzi hayo kwa karibu miaka 40 sasa
na kuyawekea msingi imara wa kuyadumisha milele. Imesisitiza
kwamba kauli mbiu ya MAPINDUZI DAIMA ni kielelezo cha
dhamira ya kweli ya kuyadumisha Mapinduzi hayo na matunda
yake ambayo kila mzalendo wa kweli wa Zanzibar na Tanzania
nzima anapaswa kujivunia.
Kamati
Kuu imetafakari pia ujasiri wa TANU na ASP chini ya
Baba wa Taifa, Marehemu Mwalimu Julius K. Nyerere na
Jemadari Mkuu wa Mapinduzi ya Zanzibar, Marehemu Mzee
Abeid Amani Karume, wa kuziunganisha Tanganyika na Zanzibar
na kuwa Tanzania tarehe 26 Aprili, 1964. Karibu miaka
40 sasa, Muungano wa Tanzania ndio mfano pekee Barani
Afrika wa
mafanikio
ya utekelezaji wa dhamira ya Waafrika kuungana kikweli.
Kwengineko kote jitihada za kuunganisha nchi zimeshindikana.
Lakini kwa upande wa Muungano wa Tanzania, juhudi zote
za maadui wa Muungano huo za kutaka kuudhofisha na kuusambaratisha
zimegonga ukuta na zitaendelea kugonga ukuta. Kamati
Kuu ina fahari kubwa kwamba vyama vya TANU na ASP na
hatimaye CCM vimeweza kuudumisha Muungano huo kwa kipindi
chote hicho na kuujengea msingi imara wa kudumu milele.
Kwa
hivyo basi, kwa kuthamini mafanikio hayo makubwa na
kuwapa heshima wanayostahili waasisi wa MAPINDUZI na
MUUNGANO, Kamati Kuu imezitaka Serikali zote mbili yaani
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ile ya Mapinduzi
ya Zanzibar ziandae sherehe kubwa za aina yake kuadhimisha
miaka 40 ya Mapinduzi ya Zanzibar hapo tarehe 12 Januari,
2004 na miaka 40 ya Muungano wa Tanzania hapo tarehe
26 Aprili, 2004.
Kamati
Kuu inawataka wananchi wote wasizikubali jitihada zinazojaribu
kufanywa na wezi wa fadhila, za kutaka tarehe hizo muhimu
katika historia ya nchi yetu zisahaulike.
Omar
R. Mapuri
KATIBU MWENEZI WA CCM TAIFA
30/07/2003
Rudi
Juu
Taarifa
rasmi - Sera ya Uzawa - Mapuri - 27.7.2003
Katika
Kikao chake cha tarehe 26-27 Julai, 2003 Kamati Kuu
ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kwa niaba ya Halmashauri
Kuu ya Taifa imemteua Ndugu Aron T. Mwasamale kuwa Katibu
wa CCM wa Mkoa. Kabla ya uteuzi huu, Ndugu Mwasamale
alikuwa Katibu Msaidizi Mkuu wa Idara ya Uenezi Makao
Makuu ya Chama. Ndugu Mwasamale amepangiwa kujaza nafasi
iliyokuwa wazi ya Mkoa wa Iringa.
Aidha
Kamati Kuu imejadili kuhusu sera ya uzawa ambayo hivi
karibuni imekuwa katika mjadala kwenye vyombo vya habari.
Kamati
Kuu imejiridhisha kwamba sera hiyo si ya CCM na wala
haina mnasaba wo wote na Mkakati wa Uwezeshaji wa Wananchi
Kiuchumi uliomo katika ibara ya 6 ya “Ilani
ya Uchaguzi Mkuu ya Mwaka 2000" ambayo
inasema ifuatavyo:-
“Ingawa Mwelekeo wa
Sera za CCM katika Miaka ya Tisini ulitamka kwamba lengo
la Ujamaa na Kujitegemea ni kuhakikisha kwamba wananchi
wenyewe wanamiliki na kuendesha uchumi wa nchi yetu,
utekelezaji wake umekuwa mgumu kufanikiwa kutokana na
ukweli kwamba Watanzania walio wengi, huko nyuma hawakupewa
nafasi ya kushiriki katika uchumi wa kisasa wa kilimo,
viwanda na biashara. Watanzania walio wengi waliachwa
kwenye sekta ya uchumi wa jadi wa kilimo, ufugaji na
uvuvi na kuwa vibarua na soko la sekta ya kisasa, hali
iliyopelekea hadi leo kuwa pembezoni mwa sekta ya kisasa
ya uchumi wa taifa letu. Kutokana na hali hiyo, Chama
Cha Mapinduzi kimebuni mkakati wa Uwezeshaji wa Wananchi
Kiuchumi ambao utawafanya Watanzania walio wengi nao
waweze kumiliki na kuendesha uchumi katika nchi yao.
Dhana ya Uwezeshaji maana yake ni kuunda mazingira mwafaka
yatakayowapatia Watanzania fursa ya kumiliki na kuendesha
uchumi wa nchi yao.”
Kamati
Kuu imesisitiza kwamba neno “uzawa” si msamiati
wa CCM, haliakisi chochote katika sera zake na haliendani
na ibara ndogo ya 5(15) ya Katiba ya CCM ambayo inaelezea
moja kati ya malengo ya CCM kuwa ni “Kuona kwamba
Serikali na vyombo vyote vya umma vinatoa nafasi zilizo
sawa kwa raia wote, wanawake na wanaume bila kujali
rangi, kabila, dini au hali ya mtu.”
Kwa
hivyo, Kamati Kuu inawataka viongozi na wanachama wote
wa CCM wasilitumie neno hilo la
“uzawa” katika kuelezea sera
za CCM. Aidha, imewataka viongozi na wanachama wanapokuwa
na mawazo ambayo wangependa yafikiriwe kuingizwa katika
Sera za CCM, watumie utaratibu wa vikao halali vya Chama
kuwasilisha mapendekezo yao na waheshimu maamuzi ya
Chama baada ya kuyazingatia mapendekezo hayo. Kamati
Kuu pia imearifiwa kwamba Serikali hivi sasa imo katika
hatua za mwisho za maandalizi ya utekelezaji wa Mkakati
wa Uwezeshaji wa Watanzania Kiuchumi kwa kuzingatia
maelekezo yaliyomo katika ibara ya saba (7) ya Ilani
ya Uchaguzi.
Taarifa
hii imetolewa na:
Mhe.
Omar Ramadhan Mapuri,
KATIBU MWENEZI WA CCM TAIFA
27/07/2003
Rudi
Juu
|