CHAMA CHA
MAPINDUZI
MAFANIKIO YA
SERIKALI YA AWAMU YA TATU (1995-2005) NA UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI YA
CCM YA MWAKA 2000
Kimetolewa
na Makao Makuu ya CCM
S.L.P.
50, DODOMA.
Aprili,
2005
UTANGULIZI
1. Serikali ya
Awamu ya Tatu ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ilitekeleza Ilani mbili za Uchaguzi za CCM; yaani Ilani ya 1995 na ile
ya 2000. Sura ya kwanza ya taarifa hii
inaelezea kwa ufupi mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi chote cha
miaka kumi cha 1995-2005 cha uongozi wa Awamu ya Tatu. Maelezo hayo yana umuhimu mkubwa wakati huu
tukijiandaa kwa Awamu ya Nne ya uongozi wa nchi yetu. Kutokana na ukubwa wa mafanikio hayo ambayo yameweka msingi wa
maendeleo ya haraka zaidi kwa nchi yetu,
Awamu ya Nne itawajibika kuyaendeleza.
2. Kwa kuwa
Serikali ya Awamu ya Tatu inamaliza muda wake wa kikatiba wa kuwa madarakani,
ni vyema kuchukua fursa hii ya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya
CCM, pia kugusia japo kwa muhutasari mafanikio ya Awamu hiyo.
3. Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000 ilikuwa ni programu ya utekelezaji wa kipindi cha
kwanza cha Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 Hadi 2010. Lakini pia ilisadifu kipindi cha pili cha
Awamu ya Tatu ya uongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini
ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa.
4. Sura zote
zilizobaki za taarifa hii zinaelezea kwa ufafanuzi utekelezaji wa Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2000 yakiwa ni
sehemu ya maandalizi ya Ilani ya 2005 ambayo imechapishwa katika kijitabu
tofauti. Utekelezaji wa Ilani ya 2000
kwa upande wa Zanzibar unaelezewa katika Sura ya Sita.
SURA YA
KWANZA
MAFANIKIO YA SERIKALI YA
AWAMU YA TATU:1995-2005
5. Uchaguzi
Mkuu wa 2005 utafanyika katika mazingira ambapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania itaingia katika awamu mpya ya uongozi (Awamu ya Nne) baada ya Awamu
ya Tatu iliyoanza 1995 chini ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa kumaliza
muda wake kwa mafanikio makubwa. Katika
kipindi chake cha kwanza cha uongozi
cha 1995 – 2000, Awamu ya Tatu ilifanya
kazi nzuri ya kukamilisha kwa mafanikio makubwa utekelezaji wa sehemu ya pili
na ya mwisho ya Mwelekeo wa CCM Katika Miaka ya Tisini. Utekelezaji
huo ulifanyika kupitia Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 1995. Aidha katika kipindi chake cha pili na cha
mwisho cha 2000 - 2005, Awamu ya Tatu
imeweza kutekeleza kwa mafanikio makubwa
ya kujivunia, sehemu ya kwanza ya Mwelekeo wa Sera za CCM Katika
Miaka ya 2000 Hadi 2010 kupitia Ilani
ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2000.
6. Mafanikio
ya Awamu ya Tatu kutokana na utekelezaji wa dhati wa Sera na Ilani za CCM yanadhihirika katika mkakati wa
urekebishaji wa uchumi wa nchi kutoka uchumi
uliodumaa hadi kufikia uchumi
uliochangamka na unaokua. Mafanikio
hayo ya msingi yameweza kuzaa mafanikio
katika Sekta zote za Kiuchumi, Kijamii na Kisiasa na kuiweka Tanzania katika
njia ya uhakika ya maendeleo na kupambana na umaskini.
7. Kwa
jumla, katika kipindi cha miaka 10 iliyopita mafanikio makubwa yamepatikana yanayoendana
na matarajio ya Dira ya Taifa ya 2025 hasa katika nyanja kuu zifuatazo:-
(a)
Utulivu wa kisiasa.
(b)
Utawala bora.
(c)
Utulizaji wa misingi ya uchumi mkuu (stabilization of macro-economic
fundamentals)
(d)
Ukuaji mkubwa wa sekta ya Madini
8. Mafanikio
hayo ni kama yafuatavyo:-
(a) Mafanikio Katika Uchumi
(i) Pato la Taifa
limeongezeka kutoka Dola (za Kimarekani) 5.6 bilioni mwaka 1995 hadi Dola 9.8
bilioni mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 75.
(ii) Pato la kila
mtu limeongezeka kutoka Dola 160 mwaka 1995 hadi Dola 260 mwaka 2004 likiwa ni
ongezeko la asilimia 62.5.
(iii) Ukuaji wa Pato la Taifa
umeongezeka kutoka asilimia 3.6 mwaka 1995 hadi asilimia 6.7mwaka 2004.
(iv) Mfumuko wa bei umeshuka kutoka asilimia 27.1 mwaka 1995 hadi
asilimia 4.2 mwaka 2004.
(v) Asilimia ya
Watanzania wanaoishi kwa kipato cha chini ya Dola moja ilishuka kutoka 50 mwaka
1995 hadi 20 mwaka 2004.
(vi) Utekelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma
umeweza kuiondolea Serikali mzigo mzito
wa kuendesha uchumi moja kwa moja.
Ubinafsishaji umeanza kujenga mazingira ya ongezeko la tija na
ufanisi katika uzalishaji wa bidhaa za
viwandani. Baada ya kubinafsishwa makampuni na mashirika hayo sasa yanaipatia Serikali mapato makubwa badala ya kuendeshwa kwa
ruzuku ya Serikali.
(vii) Mauzo ya nje ya bidhaa yameongezeka kutoka thamani ya Dola 682.9
milioni mwaka 1995 hadi Dola 1,165.9 milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la
asilimia 70.7
(viii) Akiba ya fedha za kigeni kwa ajili ya kuagizia bidhaa kutoka nje
imeongezeka kutoka uwezo wa kukidhi mahitaji ya mwezi 1.6 mwaka 1995 hadi mahitaji ya miezi 9 mwaka 2004.
(ix) Ruzuku ya Serikali Kuu kwa Serikali za Mitaa ambazo ni chombo
cha wananchi wenyewe cha kusimamia
maendeleo yao kule kule waliko, imeongezeka kutoka Shilingi 12.3 bilioni
mwaka 1995/96 hadi shilingi 392.2 bilioni mwaka 2004/05. Hili ni ongezeko la asilimia 3,088.6(yaani
zaidi ya mara 30).
(x) Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kuweka
mazingira mazuri ya kuvutia vitega uchumi na kupambana na
rushwa, hivi sasa Tanzania ni miongoni
mwa nchi zinazoongoza katika Afrika
katika kuvutia uwekezaji. Mwaka 2004 Tanzania ilipata tuzo ya kuwa nchi
ya kwanza Afrika kwa uwekaji wa mazingira mazuri ya uwekezaji. Uwekezaji wa
moja kwa moja wa mitaji kutoka nje umeongezeka kutoka Dola 50.2 milioni mwaka
1995 hadi Dola 247.8 milioni mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 394.
(xi) Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kupambana na
rushwa na kuziba mianya ya ukwepaji
wa kulipa kodi pamoja na zoezi
la ubinafsishaji wa mashirika ya umma, hatua ambayo imeboresha uzalishaji,
makusanyo ya mapato ya Serikali yameongezeka kutoka wastani wa shs. 25 bilioni
kwa mwezi, mwaka 1995 hadi wastani wa sh. 160 bilioni kwa mwezi, mwaka
2005. Hili ni ongezeko la asilimia 540.
(xii) Tanzania ilitimiza masharti ya Mpango wa Kuzifutia Madeni Nchi
Zenye Madeni Makubwa (HIPC) na
hivyo kuingizwa katika Mpango huo mwaka 1999.
Kutokana na hali hiyo, kuanzia mwaka 2002/2003 hadi 2004/2005, Tanzania
ilitekeleza Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) ambapo fedha
ambazo zingetumika kulipia madeni ya nje yaliyofutwa, sasa zilielekezwa katika
sekta teule za huduma za jamii na kiuchumi na miundombinu zinazowagusa moja kwa moja wananchi wa kawaida
kwa manufaa ya pamoja. Sekta hizo ni
elimu, afya, maji, barabara za vijijini, kilimo na utawala bora, hususan
Mahakama.
(xiii) Kutokana na juhudi za makusudi za kuimarisha utalii kwa lengo la
kuchangia katika ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira, idadi ya watalii
walioingia nchini imeongezeka kutoka watalii 295,000 mwaka 1995 hadi 582,000
mwaka 2004. Hili ni ongezeko la
asilimia 97.3 Aidha, mapato yatokanayo
na utalii nayo yameongezeka kutoka Dola 259 milioni mwaka 1995 hadi Dola 746
milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 188.0. Nafasi za ajira kwenye Sekta ya Utalii
zimeongezeka kutoka 96,000 hadi 160,750 sawa na ongezeko la asilimia 67.4
(xiv) Kutokana na utekelezaji wa sera za makusudi za kuvutia
wawekezaji wakubwa na teknolojia ya
kisasa katika uchimbaji wa madini, hasa dhahabu, imefunguliwa migodi mikubwa
Nzega, Geita, Kahama, Mara n.k.
Kutokana na maendeleo hayo, uuzaji wa madini umeongezeka kwa kiasi
kikubwa kutoka thamani ya Sh. 452.0 milioni mwaka 1995 hadi Sh. 22,786.0 milioni
mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 4,941.
(xv) Kutokana na
utulivu wa mazingira ya kisiasa na kiuchumi, biashara imechangamka nchini. Mchango wa Sekta ya Biashara kwa Pato la
Taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.4 mwaka 1995 hadi asilimia 16.8 mwaka
2004. Mchango wa Sekta ya Fedha
umeongezeka kutoka asilimia 5.9 hadi asilimia 12.1 katika kipindi hicho. Mchango wa Sekta ya Viwanda nao uliongezeka
kutoka asilimia 4.5 hadi 8.7. Aidha,
mchango wa Sekta ya Madini kwa Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 0.1
mwaka 1995 hadi asilimia 3.0 mwaka 2004.
(b) Mafanikio
katika Huduma za Kiuchumi Na Miundombinu
(i) Toka mwaka 2001, Serikali imekuwa ikitenga Sh.1.8 bilioni kila mwezi kwa ajili ya ujenzi wa
barabara nchini. Fedha hizo kwa pamoja
na zile za Mfuko wa Barabara na za
wahisani zimewezesha uimarishaji na utanuzi wa kiasi kikubwa wa mtandao wa
barabara kuu na za vijijini nchi nzima.
Urefu wa barabara za lami nchini umefikia kilomita 4,837 mwaka
2004. Kwa upande wa barabara za
changarawe/udongo, urefu umefikia kilomita 80,063 mwaka 2004. Aidha, wakati ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ukiwa unaendelea kwa
kasi, barabara za changarawe/udongo za Taifa, Mikoa, Wilaya na za Vijijini ziko katika hali nzuri ya
kupitika kuliko zilivyokuwa 1995 kutokana na kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara.
(ii) Ujenzi wa Daraja la Mto Rufiji linalojulikana sasa kama Daraja la
Mkapa ulikamilika mwaka 2004 na hivyo kuifungulia milango ya maendeleo ya kiuchumi Mikoa ya Kusini.
Mawasiliano
(iii)
Tanzania katika kipindi hiki
imeshuhudia ongezeko kubwa la mtandao wa mawasiliano, hasa ya simu za
mkononi. Idadi ya watu wanaomiliki simu
(za aina zote) imefikia watu 2,115,591
mwaka 2004.
Uchukuzi na Usafirishaji
(iv) Reli ya Dodoma - Singida
ilifunguliwa katika kipindi
hiki. Aidha, kwa jumla, huduma za usafirishaji na uchukuzi wa
abiria na mizigo kwa njia za barabara, reli, maji na anga zimekuwa bora zaidi
kwa kiwango kikubwa mijini na mikoani
kuliko zilizvyokuwa mwaka 1995
Umeme
(v) Katika sekta ya umeme, Mradi wa Gesi ya Songosongo umekamilika na
kuunganishwa na mfumo wa uzalishaji wa umeme wa Gridi ya Taifa mwaka 2004. Aidha, mradi wa umeme wa Kihansi
ulikamilika. Miradi hiyo imeliongezea
Taifa uhakika wa upatikanaji wa umeme.
(vi) Hadi kufikia mwishoni mwa
mwaka 2004, Serikali ilikwishafikisha umeme katika miji iliyo Makao Makuu ya
Wilaya 8 kati ya 18 zilizoahidiwa na CCM katika Ilani yake ya
Uchaguzi ya 2000. Ufikishaji umeme katika miji mingine 6 ulikuwa umefikia
hatua kubwa kwa ajili ya ufunguzi mwaka 2005.
Miradi ya ufikishaji umeme katika miji 5 iliyobaki iko katika hatua za maandalizi ya awali.
Sekta
ya Fedha
(vii)
Sekta ya Fedha, hasa huduma za mabenki,
imeimarika kwa kiasi kikubwa kutokana na kufunguliwa mabenki kadha makubwa ya
biashara na ya rasilimali. Mabenki hayo
yameweka msingi wa kuwawezesha wawekezaji kwa kuwapatia mikopo na hivyo kuchangamsha harakati za kiuchumi
na kupambana na umaskini.
(c) Mafanikio Katika Huduma za Jamii
Kuongezeka
kwa ubora wa huduma mbalimbali za kiuchumi na kijamii ni miongoni mwa manufaa
ya kukua kwa uchumi wa taifa ambayo wananchi wa kawaida vijijini na mijini
wameanza kuyafaidi kwa pamoja.
(i) Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2000, uliandaliwa Mpango
wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) mwaka 2002 kama sehemu ya
utekelezaji wa Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) na ni matunda
ya Tanzania kuingia katika HIPC. Aidha,
Mpango wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ulibuniwa kwa ajili ya kusaidia
nguvu za wananchi kwa kutumia mbinu shirikishi kama ilivyoelekezwa na Sera
za CCM na Ilani zake, katika juhudi zao za kujiondolea kero.
Kiasi cha asilimia 60 ya miradi ya TASAF katika Wilaya 40 za
kwanza za majaribio imekuwa katika sekta
ya Elimu. Chini ya mipango hiyo
miwili, yafutayo yamefanyika na yanaendelea:-
·
Kufutwa kwa ada ya shule za msingi za Serikali mwaka 2003.
·
Shule nyingi zimekarabatiwa nchi nzima.
·
Idadi ya vyumba vya madarasa ya elimu
ya msingi imeongezeka kutoka
vyumba 57,708 Mwaka 1995 hadi vyumba 96,215 Mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 66.7
·
Idadi ya shule za msingi za Serikali imeongezeka kutoka 10,891mwaka
1995 hadi 13,533 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 24.3.
·
Idadi ya watoto walioandikishwa Darasa la Kwanza kila mwaka imeongezeka
kutoka 712,593 mwaka 1995 hadi 1,368,315 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la
asilimia 47.9
·
Idadi ya wanafunzi katika ngazi ya elimu ya msingi imeongezeka kutoka
wanafunzi 3,877,643 mwaka 1995 hadi wanafunzi 7,083,063 mwaka 2004 likiwa ni
ongezeko la asilimia 82.7.
·
Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi kwa kutumia kigezo cha GER
(wanafunzi wote kama asilimia ya idadi ya watoto wa rika husika la umri wa miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia
77.5 mwaka 1995 hadi asilimia 106.3 mwaka 2004.
·
Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi kwa kutumia kigezo cha NER (wanafunzi wa miaka 7 - 13 kama
asilimia ya watoto wote wa rika husika
la miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia 55.3 mwaka 1995 hadi asilimia 90.5
mwaka 2004.
·
Kiwango cha kufaulu katika Mtihani wa Darasa la Saba kimefikia asilimia
48.6 mwaka 2004 kutoka asilimia 14.6 mwaka 1995.
·
Idadi ya watahiniwa wanaofaulu mitihadi ya ufundi stadi imeongezeka
kutoka asilimia 51 mwaka 1995 hadi asilimia 70 mwaka 2004.
·
Idadi ya watahiniwa wa Mitihani ya Ufundi Stadi imeongezeka kutoka
11,000 mwaka 1995 hadi 22,000 mwaka
2004 ambalo ni ongezeko la watahiniwa 11,000 sawa na asilimia 100.
·
Idadi ya wanafunzi katika shule za sekondari imeongezeka kwa asilimia
117.
·
Viwango vya kufaulu katika shule za sekondari vimeongezeka kutoka
asilimia 24.6 hadi asilimia 38.8 kwa sekondari za kawaida na asilimia 70.7 hadi
80.7 kwenye sekondari za juu.
·
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vya umma imeongezeka kutoka 7,785
mwaka 1995 hadi 32,681 mwaka 2004/05 sawa na ongezeko la asilimia 319.8. Kwa upande wa wanafunzi wa kike,
waliongezeka kutoka 1,135 hadi 10,039 sawa na ongezeko la asilimia 784.5.
(ii) Baada ya mafanikio mazuri ya kusisimua ya MMEM, Serikali
imeanza kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES)
kuanzia mwaka 2004. Ada ya shule za
sekondari za kutwa za Serikali
imepunguzwa kwa asilimia 50 wakati hatua nyingine za kukarabati na kujenga
majengo ya sekondari nchi nzima zinaendelea.
Afya
(iii) Chanjo za watoto chini ya umri wa miaka mitano zimefikia asilimia
90 mwaka 2004. Kwa kiwango hicho, Tanzania imevuka kiwango cha kimataifa cha
asilimia 80.
(iv) Pamoja na janga la UKIMWI, Sensa ya Taifa ya 2002 imeonyesha
kwamba matarajio ya kuishi ya Mtanzania yameongezeka kutoka umri wa miaka 50
mwaka 1988 hadi miaka 51 mwaka 2002.
(v)
Mifuko ya Afya ya Jamii
imeanzishwa ili kuwawezesha wananchi wa kawaida vijijini na mijini kukabiliana na gharama za
tiba. Aidha, Bima ya Afya imeanzishwa kwa ajili ya wafanyakazi wa
Sekta ya Umma.
(vi) Ukarabati mkubwa wa hospitali kuanzia Hospitali ya Taifa ya
Muhimbili mpaka hospitali za Mikoa na
Wilaya ama umekamilika au uko katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Mashine za “X-Ray” na “Ultra-sound”
na jenereta zimefungwa katika hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa.
(vii) Katika harakati za kuongeza ubora wa utoaji wa huduma za afya,
kumekuwa na ongezeko la mtandao wa vituo vya kutolea huduma nchi nzima kama
ifuatavyo:-
·
Hospitali kutoka 194 mwaka 1995 hadi 221 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko
la asilimia 14.
·
Vituo vya afya kutoka 343 mwaka 1995 hadi 433 mwaka 2004, likiwa ni
ongezeko la asilimia 26.2.
·
Zahanati kutoka 3,832 mwaka
1995 hadi 4,622 mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 20.6.
(viii)
Kufutwa kwa kodi kwenye vyandarua na bidhaa zinazosaidia vita dhidi ya
malaria.
(ix)
Programu kabambe ya kukabiliana na janga la UKIMWI imeanzishwa na
inatekelezwa.
(x)
Kwa jumla uhaba wa dawa uliokuwepo miaka ya tisini sasa haupo tena.
Maji
Mijini na Vijijini
(x) Idadi ya wakazi mijini wanaopata huduma ya maji safi na salama
imeongezeka kutoka asilimia 60 mwaka 1995 hadi asilimia 74.0 mwaka 2004.
(xi) Idadi ya wananchi vijijini wanaopata maji safi na salama
imeongezeka kutoka asilimia 42 mwaka 1995 hadi asilimia 53.5 mwaka 2003
(xii) Sambamba na miradi midogo midogo ya maji inayoendelea nchi nzima,
miradi mikubwa ya maji ya Dodoma na Chalinze imekamilika. Aidha, miradi kabambe ya Dar es Salaam na kuvuta maji toka Ziwa Victoria kwenda
Shinyanga Mjini na Kahama imeanza na inaendelea.
Ardhi
na Makazi
(xiii) Uwekezaji mkubwa wa sekta binafsi na wa wananchi mmoja mmoja
umeongezeka katika ujenzi wa majumba, na hivyo kubadili sura ya Jiji la Dar es
Salaam na miji mingine kwa kiasi kikubwa.
(xiv) Mwamko unaoongezeka wa kujenga nyumba nzuri miongoni mwa
wananchi vijijini unabadilisha kwa kasi
sura ya vijiji vingi nchi nzima.
(xv) Mradi wa kupima viwanja 20,000 katika jiji la Dar es Salaam
umepunguza bughudha katika kupata
viwanja na kuziba mwanya mkubwa wa rushwa iliyokuwa ikiwasumbua wananchi.
(d) Mafanikio Katika Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi
Uwezeshaji
wa Wananchi Kiuchumi ni sera iliyokusudiwa kuwajengea mazingira Watanzania
yanayowawezesha kufaidi mmoja mmoja manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa
katika kuongeza vipato vyao kutokana na juhudi zao za kupambana na umaskini. Katika kipindi hiki, Serikali ya CCM imeweza
kuchukua hatua kadha za kuyafikisha kwa wananchi mmoja mmoja manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa kama
ifuatavyo:-
(i) Kufuta kodi ya maendeleo mwaka 2004 na nyingi nyingine ambazo
zilikuwa kero kwa wananchi na ambazo
pia zilidumaza ari ya kupambana na umaskini.
Hatua hii imewakombolea wananchi kipato chao kilichokuwa kikiwatoka ambacho sasa wanakitumia wenyewe
katika harakati zao za kupambana na umaskini.
Pia imeziba mwanya wa rushwa uliokuwa ukiwasumbua sana wananchi, kupitia
kodi hii.
(ii) Serikali imeanza kutoa fidia kwa mbolea na baadhi ya dawa za
mifugo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji
wa Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi
Kiuchmi unaowasaidia kupambana na
umaskini kwa namna ambayo itawaongezea kipato.
(iii) Pamoja na kuongezeka na kushamiri kwa harakati za kujiajiri, ajira
katika sekta rasmi pia zimeongezeka.
Idadi ya waajiriwa katika sekta
rasmi ya umma na isiyokuwa ya umma imeongezeka kutoka 817,626 mwaka 1990
hadi 1,179,155 mwaka 2000. Hili ni
ongezeko la nafasi 361,529 za ajira sawa na asilimia 44. Hii ni kinyume na imani ya baadhi ya watu
kwamba eti ajira imepungua.
(iv) Mshahara wa kima cha chini wa kisheria umeongezeka kutoka Shs.
5,000/= mwaka 1995 hadi Shs. 48,000/=
mwaka 2004 likiwa ongezeko la asilimia 174.4 Ukilinganisha na kushuka kwa
mfumuko wa bei katika kipindi hicho kutoka asilimia 27.1 hadi asilimia 4.1, ni
dhahiri kwamba kipato cha mfanyakazi kimeongezeka.
(v) Mwaka 2004, Serikali ya CCM ya Awamu ya Tatu ilitunga Sera ya utekelezaji ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi na kutunga sheria ya utekelezaji wa sera hiyo. Hatua hizo ni utekelezaji wa ibara za 6 na 7 za Ilani ya CCM ya 2000 zilizotoa na kufafanua dhana na Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi. Katika utekelezaji wa Sera hiyo, imeandaliwa mikakati miwili ifuatayo ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi.
·
Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kuondoa Umaskini Tanzania (MKUKUTA). Mkakati huu wa miaka mitano
umeandaliwa mwaka 2005 kuchukua nafasi ya Mkakati wa Kupunguza
Umaskini (MKU) ambao umemaliza muda
wake wa miaka mitatu kwa mafanikio makubwa.
MKUKUTA unakusudiwa kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi na kujenga
mazingira ya kuwawezesha wananchi kiuchumi ili wachangie kwa kiwango kikubwa
zaidi ukuzaji wa uchumi wa Taifa na wao wenyewe kuumiliki na kuuendesha uchumi
huo na kujiongezea kipato na hivyo kuondokana na umaskini.
·
Mkakati wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara Tanzania (MKURABITA): Mkakati huu ambao ni sehemu ya MKUKUTA
unakusudiwa kuweka utaratibu rahisi na mwepesi wa kuzitambua rasilimali (hasa
ardhi na nyumba) na biashara wanazomiliki wananchi bila ya kuzisajili na
hatimae rasilimali hizo zirasimishwe kwa kusajiliwa. Zikisharasimishwa, rasilimali hizo zitaweza kutumika kama dhamana
za mikopo kutoka mabenki na taasisi nyingine za fedha. Hatua hiyo itawaongezea wananchi uwezo wa
kupambana na umaskini kwa kutumia rasilimali zao ambazo hivi sasa ni mfu na
wakati huo zitakuwa hai, na kuwapatia mitaji.
(e)
Mafanikio ya Kisiasa
(i) Mazingira yaliyowezesha mafanikio haya makubwa ya kiuchumi na
kijamii ni kuwapo kwa amani na utulivu wa kisiasa nchini. Serikali ya CCM ya Awamu ya Tatu imeweza
kuendelea kujenga na kudumisha hali ya
amani na utulivu kwa kipindi chote cha uongozi wake tangu ilipoingia
madarakani.
Kupanuka na Kuimarika kwa Demokrasia na Utawala Bora
(ii)
Katika kipindi hiki, demokrasia imeendelea kupanuka na kuimarika katika
nyanja za uhuru wa kuabudu, kutoa maoni, kuanzisha asasi zisizo za Kiserikali
na uhuru katika nyanja mbalimbali zinazowagusa
wananchi vikiwemo vyombo vya habari, vyama vya siasa na kuanzishwa kwa
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala
Bora.
(iii)
Idadi ya vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu imeongezeka kutoka 13
mwaka 1995 hadi 18 mwaka 2005.
(iv)
Kwa upande wa vyombo vya habari, katika miaka 10 iliyopita, idadi ya
magazeti ya kila siku imeongezeka kutoka 22 hadi 42; magazeti ya kila wiki
kutoka 67 hadi 171, na vituo vya redio kutoka 2 hadi 63.
Mapambano Dhidi ya
Rushwa
(v) Kuimarika kwa taasisi za demokrasia na utawala bora pamoja na
mazingira ya ukweli na uwazi yamejenga mwamko na hamasa ya kupambana na rushwa
miongoni mwa wananchi. Hayo pamoja na
hatua za makusudi za Serikali za kuziba
mianya ya rushwa na kuwachukulia hatua
za kisheria na kiutawala wanaobainika kujihusisha na rushwa kufuatia
mapendekezo ya Tume ya Warioba, kiwango cha rushwa kimeanza kuonyesha dalili za
kupungua. Katika tathmini za Kimataifa kama zile za Taasisi
ya Uwazi (Transparency International)
kiwango cha rushwa kimeshuka kwa kiasi cha asilimia 84 katika kipindi
cha 1998-2004. Tanzania sasa si
miongoni tena mwa nchi zinazoongoza kwa rushwa Afrika na hata duniani. Aidha,
kwa mujibu wa utafiti wa Benki ya Dunia, katika kipindi cha 1996-2004, Tanzania
ndiyo nchi pekee barani Afrika iliyopiga hatua kubwa kuimarisha utawala bora
kwa vigezo vyote vitatu vya Sauti na
Kuwajibika kwa Wananchi; Utendaji wa Serikali; na Kudhibiti Rushwa.
(vi) Kwa kuongozwa na Sera ya CCM ya kuwa na jeshi dogo la usalama na raia
lakini lenye uwezo mkubwa wa kitaaluma na kinyenzo, Serikali imekuwa ikichukua hatua za makusudi kuviimarisha
vyombo vinavyoshughulikia usalama wa
raia na mali zao ili kuviongezea
ufanisi. Kutokana na hatua hizo, kuna dalili za kupungua kwa uhalifu nchini kwani idadi ya matukio yote ya
uhalifu yaliyoripotiwa Polisi imepungua
kutoka 460,578 mwaka 1995 hadi
261,098 mwaka 2004. Huu ni upungufu wa
asilimia 76.4. Makosa yenye sura ya
ujambazi miongoni mwayo yalipungua kutoka 9,061 mwaka 1995 hadi 8,693
mwaka 2004, ukiwa ni upungufu wa asilimia 4.2.
(vii) Katika kutekeleza sera ya CCM ya kuwashirikisha wananchi katika
ulinzi na usalama wao na wa mali zao, Serikali imo katika hatua za awali za
kuweka utaratibu wa Polisi Jamii ambao utavishirikisha vikundi vya aina
mbali mbali vya ulinzi wa jadi na vya kujiajiri kwa uhakika na ufanisi zaidi.
(viii) Kuhusiana na wahalifu wanaohukumiwa vifungo magerezani, mtazamo
umebadilika kuelekea katika kuthamini haki zao za kibinadamu na dhana ya urekebishaji wa tabia zao. Kutokana
na mwelekeo huo, juhudi za makusudi za kupunguza msongamano magerezani na
kuwafundisha wafungwa amali za kujitegemea zimefanywa kwa njia zifuatazo:-
·
Kupanua magereza yaliyopo na kuongeza mapya.
·
Kuongeza ubora wa lishe,
matibabu, malazi, usafi na mavazi kwa wafungwa magerezani.
·
Misamaha ya mara kwa mara ya Rais.
·
Parole na vifungo vya nje.
·
Kuanzishwa kwa utaratibu wa huduma kwa jamii ambapo wahalifu wataohukumiwa vifungo vya muda mfupi kwa baadhi ya makosa hawatopelekwa magerezani na badala yake
watatumikia vifungo vyao kwa kufanya kazi kwenye miradi ya jamii wakiwa
majumbani mwao.
·
Kufufua miradi ya uzalishaji
mali magerezani kama vile kilimo, ufugaji, ufundi stadi, ujenzi
n.k.
10. Mafanikio yote
haya ya kiuchumi, kijamii na kisiasa yaliyopatikana katika kipindi cha
miaka 10 ya uongozi wa Awamu ya Tatu ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, yamepatikana kutokana na uadilifu na umakini wa utekelezaji wa
Sera na Ilani za CCM chini ya usimamizi
wa uhakika wa CCM yenyewe. Ili
kuyaendeleza mafanikio hayo, ni muhimu
Serikali ya Awamu ya Nne iwe tena ya CCM.
11. Serikali ya
Awamu ya Nne itawajibika kujenga juu ya msingi wa mafanikio haya. Itapaswa kuyaendeleza mafanikio haya kwa
nguvu na kasi mpya na wakati huo huo kupanua upeo wa masuala ya kiuchumi,
kijamii na kisiasa na kuyaendeleza ili kukidhi matarajio ya Watanzania na
kudumisha matumaini yao. Katika kipindi
cha miaka 10 ijayo tutapaswa kuelekeza juhudi zetu katika kukuza uchumi kwa
kuchangamsha harakati za kiuchumi ambazo zitawezesha yafuatayo:-
(a)
Kuzalisha ajira.
(b)
Kuongeza tija.
(c)
Kujenga utajiri wa nchi.
(d)
Kuboresha kiwango cha maisha cha Watanzania.
TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM YA MWAKA 2000
SURA YA PILI
UCHUMI
12. Uchumi wa
Tanzania umeendelea kuwa bora na
thabiti tangu Serikali ya Awamu ya Tatu iingie madarakani mwaka 1995
kufuatia utekelezaji wa kina uliofikiwa katika marekebisho mbalimbali ya uchumi
na ujenzi wa mazingira ya kiuchumi yenye kuvutia wawekezaji. Katika kipindi cha utekelezaji wa Ilani ya
CCM ya 2000, usimamizi wa utekelezaji wa sera za mapato, matumizi na fedha
uliendelea kwa makini
zaidi. Viashiria vya mafanikio hayo
yaliyoleta kutengamaa kwa uchumi mkuu ni pamoja na kuongezeka kwa mitaji katika
sekta za umma na sekta binafsi, na kuongezeka kwa akiba ya fedha za kigeni.
13. Hali ya ukame iliyojitokeza katika baadhi ya mikoa nchini mwaka 2003,
haikuathiri sana utulivu wa uchumi na hii ni ishara ya mafanikio makubwa ya
mageuzi yetu ya uchumi. Wastani wa
ukuaji wa Pato la Taifa kutoka mwaka 2000 hadi mwaka 2004 ulikuwa asilimia 5.7
kwa mwaka. Ukuaji halisi wa Pato la
Taifa mwaka 2004 ulikuwa asilimia 6.7, ukiongezeka kutoka asilimia 4.9 mwaka
2000.
14. Ukuaji wa uchumi katika kipindi hicho ulichangiwa hasa na hatua za kisera na kimkakati zilizochukuliwa na Serikali katika jitihada zake za kuimarisha uchumi na ustawi wa jamii. Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ni pamoja na zifuatazo:-
(a) Kuendeleza kwa msukumo mkubwa na kwa
ufanisi zaidi hatua za kujenga uchumi
unaoendeshwa na soko kwa ushiriki mkubwa wa sekta binafsi.
(b) Kutekeleza kwa ufanisi mikakati ya
kutengemaza uchumi (macro-economic stability);
(c) Kutekeleza kwa ufanisi mikakati ya
kuimarisha ukusanyaji wa mapato na
kudhibiti matumizi ya Serikali.
Ukusanyaji wa mapato uliongezeka kwa wastani wa Sh. 77.5 bilioni mwaka 2000
hadi wastani wa Sh. 160.0 bilioni mwaka 2005.
(d) Kutekeleza kwa ufanisi sera za kudhibiti
ujazi wa fedha, kupunguza mfumuko wa bei, urekebishaji wa Mashirika ya Umma na
ulipaji wa madeni ya nje na ndani. Juhudi hizo zimeiongezea nchi imani kwa wahisani. Mfumuko wa bei ulishuka kutoka asilimia 6.0 mwaka 2000 hadi asilimia 4.1 mwaka
2004. Aidha, urekebishaji wa mashirika
ya umma unaelekea mwishoni.
(e)
Mikakati ya kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji wa ndani na nje, na
kuweka mazingira mazuri ya utawala bora kwa lengo la kukuza rasilimali na kuongeza
ajira. Hadi Desemba 2004, jumla ya
miradi 2,527 ilikuwa imeidhinishwa na Kituo cha Uwekezaji (TIC). Miradi hiyo inakadiriwa kutoa nafasi 498,539
za ajira. Ukuzaji rasilimali
uliongezeka kutoka Sh. 1,281,046 milioni mwaka 2000 hadi Sh.2,593,501 milioni
mwaka 2004.
(f) Kuanza utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo inayotoa mwelekeo wa muda mrefu wa
maendeleo ya Tanzania, na pia kwa kuzingatia Malengo ya Maendeleo ya Milenia
(MDGs).
SURA YA TATU
SEKTA ZA UZALISHAJI MALI
Kilimo
15. Tanzania ni nchi inayotegemea kilimo kama
nguzo yake kuu ya uchumi katika kuleta maendeleo na kuondoa umaskini. Kilimo huajiri zaidi ya asilimia 70 ya
Watanzania na karibu asilimia 80 ya Watanzania wanaoishi vijijini wanategemea
kilimo kwa chakula chao na mapato ya fedha za kununulia mahitaji yao
mengine. Kilimo kilichangia wastani wa
asilimia 47 ya Pato la Taifa na wastani wa asilimia 29.1 ya mapato ya fedha za
kigeni kati ya 2000-2003. Tanzania
huzalisha zaidi ya asilimia 95 ya chakula kinachotumika nchini na hununua cha
kujazia pengo lo lote linapotokea kutoka nje.
Mwaka 2003/2004 Taifa lilijitosheleza kwa chakula kwa asilimia 90
kutokana na hali ya ukame ulioyakabili baadhi ya maeneo ya nchi. Viwanda vingi
husindika mazao yanayotokana na kilimo na, kwa hiyo, hutumia mazao ya kilimo
kama malighafi. Kwa hiyo, kilimo
kimeendelea kutoa mchango katika uchumi wa Taifa na kina uwezo wa kutoa mchango
zaidi iwapo matatizo yanayokwamisha kukua kwa uzalishaji katika kilimo yatapatiwa
ufumbuzi wa kudumu, kwa kuzingatia modenaizesheni.
16. Katika kipindi
cha 2000-2005 hatua mbali mbali zilichukuliwa na Serikali katika jitihada za
kupunguza matatizo yanayokwamisha kilimo, zikiwemo zifuatazo:-
(a)
Kuandaa na kukamilisha miradi 75 ya umwagiliaji mashambani yenye eneo
la hekta 27,470 na mabwawa 6 yenye hekta 860.
(b)
Kurejeshwa kwa utaratibu wa kutoa ruzuku kwa pembejeo za kilimo kwa
kuanzia na mbolea kwa baadhi ya mikoa.
(c)
Kuweka utaratibu bora zaidi wa kuwawezesha waagizaji na wasambazaji
wa pembejeo na zana za kilimo kupata
mikopo kutoka Mfuko wa Taifa wa Pembejeo za Kilimo kupitia benki kwa lengo la
kuongeza ufanisi katika utoaji na urejeshaji wa mikopo.
(d)
Kuratibu kwa ufanisi zaidi upatikanaji wa mbegu bora, kusimamia ubora
wa mbegu hizo na kuzalisha mbegu za msingi katika mashamba ya mbegu
yanayosimamiwa na Serikali.
(e)
Kutoa ruzuku kwa Halmashauri za Wilaya ili kuendeleza kilimo.
(f)
Kuweka mazingira mazuri ya kuvutia wawekezaji ikiwa ni pamoja na
kuanzisha Benki ya Ardhi.
(g)
Ubinafsishaji wa baadhi ya mashamba makubwa.
(h)
Kuanzisha mradi wa kuboresha miundombinu ya masoko ikiwa ni pamoja na
kujenga magulio, kuboresha barabara za vijijini na kujenga maghala ya
kuhifadhia chakula.
17. Matokeo ya hatua hizo na nyinginezo zenye
mwelekeo wa modenaizesheni ni pamoja na yafuatayo:-
(a)
Tija katika baadhi ya mazao imeongezeka. Kwa mfano katika maeneo yanayolima mpunga kwa njia ya
umwagiliaji, tija imeongezeka kutoka wastani wa tani 1.8 kwa hekta mwaka
2000/2001 hadi tani 5.0 kwa hekta mwaka 2003/2004.
(b)
Uzalishaji wa mazao makuu ya biashara hususan sukari, chai, tumbaku na
mkonge uliongezeka katika kipindi cha 2000/2001 – 2003/2004 kama ifuatavyo:-
(i) Sukari: Kutoka tani 135,534 hadi
tani 228,000 likiwa ni ongezeko la asilimia 68.2.
(ii) Tumbaku: Kutoka tani 28,000 hadi tani
46,725 likiwa ni ongezeko la asilimia 66.9.
(iii) Chai: Kutoka tani 26,386 hadi tani
30,700 likiwa ni ongezeko la asilimia 16.3
(iv) Mkonge: Kutoka tani 20,500 hadi tani
23,858 likiwa ni ongezeko la asilimia 16.4.
(c)
Uzalishaji wa mazao ya chakula uliongezeka kutoka tani 7.3 milioni
mwaka 1999/2000 hadi tani 15.6 milioni mwaka 2003/2004 sawa na ongezeko la
asilimia 113.7.
(d)
Kiwango cha Tanzania kujitosheleza kwa chakula kimefikia wastani wa
asilimia 95 katika kipindi hiki kutoka asilimia 92 mwaka 2000/2001.
(e)
Ukuaji wa sekta ya kilimo umeongezeka kutoka asilimia 3.4 mwaka 2000
hadi asilimia 5.1 mwaka 2004.
18. Sekta ya
mifugo ni muhimu sana katika kusaidiana na kilimo kukuza uchumi wa Taifa,
kulilisha Taifa, kutoa ajira kwa wananchi na juhudi za kupambana na
umaskini. Katika kipindi kilichopita
cha 2000-2005 sekta ya mifugo, Serikali ya CCM iliendelea kuchukua hatua mbali
mbali kwa lengo la kuyapunguza matatizo yanayoikwaza na kuiingiza katika
mtiririko wa modenaizesheni. Zifuatazo ni miongoni mwa hatua
hizo:-
(a)
Kutekeleza mikakati ya kuendeleza Sekta ya Mifugo kupitia ugani, tiba,
kinga, usambazaji wa maji na uboreshaji wa malisho.
(b)
Kuimarisha kituo cha madume cha Usa River cha kuzalishia mbegu bora za
ng’ombe, ambapo uwezo wa kituo hicho umeongezeka kutoka kuzalisha dozi 190,000
za mbegu mwaka 2000 hadi dozi 230,000 mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la
asilimia 21.1.
(c)
Kuendeleza mashamba ya ng’ombe ya Sao Hill, Mabuki, Nangaramo,
Ngerengere, Kitulo na Kibaha kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa mitamba na
kuisambaza kwa wafugaji wadogo chini ya utaratibu wa “kopa ng’ombe/mbuzi lipa
ng’ombe/mbuzi”.
(d)
Ubinafsishaji wa baadhi ya ranchi za Serikali umeanza kwa kuzikata
katika ranchi ndogo ndogo na kuwauzia wawekezaji wadogo wa Kitanzania katika
kutekeleza Mkakati wa Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi kwa kufuga kibiashara. Ranchi zinazohusika ni pamoja na Mkata,
Mzeri, Dakawa, Kalambo, Usangu, Kikulula, West Kilimanjaro, Kitengule, Misenyi
na Uvinza.
(e)
Kutenga maeneo ya hekta 20,000 (kila moja) kwa ajili ya kutumika kama
ranchi za mfano katika baadhi ya mashamba ya mifugo.
(f)
Utengaji wa maeneo kwa wafugaji kwa lengo la kupunguza migogoro baina
ya wafugaji na wakulima. Utaratibu huo
ulianza kutekelezwa kwa ufanisi katika mikoa ya Morogoro, Mbeya, Iringa,
Dodoma, Pwani na Mwanza.
(g)
Kuhimiza uanzishaji wa vikundi vya ushirika wa wafugaji. Zaidi ya
vikundi 200 vimeanzishwa kuanzia 2000 hadi 2004.
(h)
Kutoa elimu na mafunzo kwa wafugaji kuhusu matumizi bora ya ardhi, hasa
uwiano wa mifugo na malisho, kutunza nyanda za malisho, umuhimu wa kupunguza
mifugo kwa kuiuza, na umuhimu wa kutibu mifugo kwa wakati na namna ya kudhibiti
na kukabili magonjwa ya mlipuko.
(i)
Ujenzi/ukarabati wa malambo 280 kuanzia 2000 hadi 2004 kwa lengo la
kuwapunguzia wafugaji haja ya kuhama hama.
(j)
Miundombinu ya masoko ya mifugo iliendelea kuhuishwa kwa kukarabati
vituo vidogo vidogo vya kupumzikia na kuhifadhia mifugo, minada ya awali na ya
sekondari na minada ya mipakani. Aidha,
machinjio ya kisasa ikiambatana na Chuo cha Ukataji wa Nyama imejengwa Dodoma.
19. Kutokana na hatua hizo na nyingine za
kawaida za ugani, uzalishaji katika Sekta ya Mifugo uliongezeka kama
ifuatavyo:-
(a) Nyama
ya Ng’ombe: Kutoka tani 175,000 mwaka 2000 hadi tani
184,000 mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 5.1.
(b) Nyama ya Kuku: Kutoka tani 45,000 mwaka 2000 hadi tani
63,000 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 40.0.
(c) Mayai: Kutoka mayai 450 milioni mwaka 2000 hadi mayai 910 milioni mwaka
2004 sawa na ongezeko la asilimia 102.2.
(d) Nyama ya Mbuzi, Kondoo na Nguruwe: Kutoka tani 5,800 mwaka 2000 hadi tani 6,000
mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 3.4.
(e) Ngozi ya Ng’ombe: Kutoka vipande 1.3 milioni mwaka 2000 hadi
vipande 1.6 milioni mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 23.1.
20. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000 hadi
2004 hatua zilizochukuliwa katika utekelezaji wa Ilani katika sekta ya uvuvi ni
pamoja na:-
(a) Elimu ya ufugaji samaki ilitolewa kwa
wafugaji samaki katika mikoa ya Ruvuma,
Morogoro, Kilimanjaro, Arusha, Mbeya, Kigoma, Singida na Kagera, na kwa
wakulima wa mwani 9,000 katika mikoa ya Lindi, Mtwara na Tanga.
(b) Kuandaa Mpango Kamambe wa Kuendeleza Uvuvi
nchini ambapo miradi 15 yenye kipaumbele iliainishwa. Katika kutekeleza mpango huo ujenzi wa masoko ya samaki ya Dar es
Salaam na Mwanza ulikamilika.
(c) Kuimarisha doria kwa kuhudumia maboti 11 ya
doria yaliyoko Dar es Salaam, Mwanza, Kigoma, Mtera na Nyumba ya Mungu. Aidha, maboti 4 ya doria yalinunuliwa kwa
ajili ya kuimarisha doria katika bahari na maeneo ya maeneo ya maziwa, na vikundi
511 vya ulinzi wa raslimali za uvuvi viliendelezwa katika Ziwa Victoria.
(d) Kurekebisha Sheria ya Uvuvi Namba 6 ya mwaka
1970 na kuwa Sheria Namba 22 ya mwaka 2003 ili kutekeleza Sera ya Uvuvi ya
mwaka 1997 na kuzingatia mabadiliko ya shughuli za uvuvi ambazo zimepanuka
sana.
(e) Kuhakikisha usalama wa mazao ya uvuvi kwa
walaji kwa kuimarisha shughuli za kudhibiti ubora wa mazao ya uvuvi. Sampuli 2,616 za udongo, samaki na maji
zilifanyiwa uchunguzi wa kimaabara nchini na nje ya nchi na kuonekana kuwa
katika viwango vinavyokubalika kimataifa.
Uhakiki wa mazao ya uvuvi ulisaidia kuhakikisha usalama wa walaji na pia
soko.
(f) Sekta binafsi ilihamasishwa kuanzisha
viwanda vya kusindika samaki ambapo viwanda 20 vimejengwa na vingine
vinaendelea kujengwa.
(g) Vikundi vya wavuvi wadogo wadogo vimeendelea
kuundwa na kupatiwa mikopo.
(h) Mabwawa ya kufugia samaki yameongezeka
kutoka 10,000 mwaka 2000 hadi 14,000 mwaka 2004, ikiwa ni ongezeko la asilimia
40.
21. Matokeo ya
hatua hizo ni kwamba wavuvi wadogo wadogo wameongeza tija ya uzalishaji na
idadi ya meli za uvuvi katika Ukanda wa Uchumi wa Bahari (EEZ) imeongezeka
kutoka meli 5 mwaka 2000 hadi meli 78 mwaka 2004. Kutokana na ongezeko hilo la meli, biashara ya mazao ya uvuvi
iliongezeka toka Dola 64,635,114 mwaka 2000 hadi Dola 129,605,815 mwaka 2004
sawa na ongezeko la
asilimia 100.6.
22. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2000 hadi
2004 hatua zilizochukuliwa na mafanikio
yaliyopatikana katika utekelezaji wa Ilani ni pamoja na:-
(a) Kuwezesha TAWIRI kupata idadi ya wanyamapori
kwa madhumuni ya kuandaa viwango vya matumizi kwa kufanya sensa katika mapori
ya akiba, hifadhi za taifa na maeneo mengine yenye wanyamapori. Matokeo ya sensa yalionyesha kuwa idadi ya
tembo iliongezeka kufikia 120,000 mwaka 2004 ikilinganishwa na 88,000 mwaka
2000. Hili ni ongezeko la asilimia
36.4.
(b) Kutathmini viwango vya matumizi (quota)
ya wanyamapori ambapo katika kipindi hiki jumla ya wanyamapori 7,623,237
waliidhinishwa kwa ajili ya biashara ya nyara.
(c) Kutenga maeneo ya ardhi oevu yenye umuhimu
wa kimataifa (Ramsar Sites) ambapo jumla ya kilometa za mraba 47,563.35
zilitengwa kwa ajili hiyo.
(d) Kuandaa mipango ya Uendeshaji wa mapori ya
akiba ambapo rasimu za mipango ya usimamizi wa mapori 18 ya akiba ya Mkomazi,
Umba, Rungwa, Kizigo, Muhesi, Selous, Ikorongo, Grumeti, Muyowosi, Kigosi,
Maswa, Burigi, Biharamulo, Ibanda, Rumanyika, Usangu, Mpanga-Kipengele na
Ugalla ziliandaliwa. Aidha, Mipango ya
Usimamizi kwa mapori ya akiba ya Mkomazi, Selous, Rungwa, Kizigo na Muhesi
ilipitiwa.
(e) Kuweka mazingira ya kuwezesha jamii
kuhifadhi wanyamapori kwenye ardhi za vijiji ambapo Kanuni na Mwongozo kwa
ajili ya kushirikisha wananchi katika uhifadhi wa wanyamapori, hususan uanzishaji
wa Maeneo ya Jumuiya ya Hifadhi ya Wanyamapori (WMAs) ziliandaliwa.
(f) Kuanzisha na kusimamia WMAs ambapo vijiji
74 katika Wilaya 10 vilitenga maeneo ya ardhi yenye jumla ya kilometa za mraba
15,272.27 kwa ajili ya kuanzisha WMA.
Wilaya zilizohusika ni Liwale, Tunduru, Namtumbo, Morogoro (V), Rufiji,
Monduli, Sikonge, Urambo, Babati na Kiteto.
(g) Kununua ndege moja na magari 50 kwa ajili ya
kuimarisha doria dhidi ya ujangili.
(h) Hifadhi ya Taifa ya Kitulo yenye ukubwa wa
kilomita za mraba 273 ilitengwa na Pori la Akiba la Saadani lenye kilomita
1,141 lilipandishwa hadhi na kuwa Hifadhi ya Taifa.
(i) Jumla ya miti 292,428,845 ilipandwa katika
mikoa yote Tanzania Bara katika kampeni ya kupanda miti na kuhifadhi mazingira.
(j) Kuhamasisha wananchi kupanda na kutunza
miti na kuhifadhi uoto wa asili ambapo wananchi wa Mkoa wa Shinyanga
walihifadhi maeneo ya “ngitiri” yenye zaidi ya hekta 300,000. Aidha, wananchi wa vijiji 95 katika mikoa ya
Kilimanjaro, Tanga, Arusha, Morogoro na Dodoma walihamasishwa kutenga na
kuhifadhi maeneo ya hifadhi ya misitu ya asili. Wananchi wa vijiji katika mikoa ya Tabora, Lindi, Pwani, Morogoro
na Iringa walitenga hekta 33,000 kuwa misitu ya hifadhi ya vijiji.
Utalii
23. Katika kipindi cha 2000 hadi 2004 biashara
ya utalii iliendelea kukua. Pamoja na
kuathiriwa na vita vya Irak, ugaidi n.k. idadi ya watalii walioingia nchini
iliongezeka kutoka watalii 501,660 mwaka 2000 hadi watalii 578,812 mwaka 2003.
24. Katika kuimarisha biashara ya utalii, miongoni mwa mambo yaliyofanyika ni pamoja
na:-
(a) Kuanzishwa kwa chombo kinachmilikiwa na
sekta binafsi kiitwacho Tourist Comfedation of Tanzania ambapo chombo hiki kwa
kushirikiana na Serikali kimeandaa Tourism Directory.
(b) Kubaini maeneo mapya ya utalii wa utamaduni
ambapo vivutio vya utalii wa utamaduni katika maeneo mapya vilibainishwa katika
mikoa ya Singida, Lindi, Mtwara, Mbeya, Iringa, Dar es Salaam, Kagera na Mara.
(c) Kuendeleza masoko ambapo mkakati wa pamoja
wa kuendeleza masoko ya utalii katika Jumuiya ya Ulaya, Canada na Japan
uliandaliwa. Jumla ya majarida 120,000,
majalada 33,000 na mabango 85,000 yalichapishwa na kusambazwa katika ofisi zetu
za Ubalozi nchi za nje na maonyesho mbalimbali ya kitaifa na kimataifa. Aidha, nakala 44,600 za filamu za video
zilisambazwa kwa wadau mbali mbali.
(d) Kuandaa Sera ya Mambo ya Kale katika
jitihada za kupanua wigo wa vivutio vya kiutalii.
(e) Kutekeleza mpango wa uhifadhi na uendelezaji
wa maeneo ya kihistoria ambapo majengo ya kihistoria ya miji ya Kilwa Kisiwani
na Songo Mnara pamoja na jengo la Livingstone yalikarabatiwa.
(f) Sekta ya Utalii imezalisha nafasi 322,258
za ajira katika kipindi cha 2000 hadi
2004.
25. Katika kipindi kilichopita, Serikali katika
utekelezaji wa Ilani iliendelea kutekeleza sera ya ubinafsishaji. Pia iliandaa Sera Endelevu ya Viwanda,
Sera ya Viwanda Vidogo na Biashara Ndogo na Sera ya Utekelezaji ya
Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.
Sera zote hizo zilisaidia sana
katika kuimarisha viwanda.
Aidha, yalianzishwa maeneo maalum ya uzalishaji kwa ajili ya kuuza nje
(EPZ). Viwanda vingi vimepata
wawekezaji wapya wenye uwezo wa kuingiza teknolojia mpya na uzoefu wa kuendesha
viwanda kisasa.
26. Matokeo ya hatua hizo za ubinafsishaji wa
viwanda ni pamoja na:-
(a) Kuongezeka kwa uzalishaji wa bidhaa
viwandani na hivyo kukidhi mahitaji ya wananchi. Kwa mfano, uzalishaji wa nguo uliongezeka kutoka mita za mraba
73.6 milioni mwaka 2000 hadi mita za mraba 109.8 milioni mwaka 2004; usagishaji
wa ngano kutoka tani 162,634 mwaka 2000 hadi tani 333,789 mwaka 2004;
uzalishaji wa chuma kutoka tani 11,182 mwaka 2000 hadi tani 46,559 mwaka
2004. Ongezeko kubwa la uzalishaji
lilipatikana pia katika bia, sigara, bati, saruji, biskuti na tambi;
utengenezaji wa kamba za katani, uuzaji nje wa samaki wa kusindikwa; n.k.
(b) Kuongezeka kwa ukuaji wa Sekta ya Viwanda
kutoka asilimia 4.8 mwaka 2000 hadi asilimia 9.0 mwaka 2003.
(c) Kuongezeka kwa thamani ya miradi
iliyoidhinishwa kutoka Tshs. 123.8 bilioni mwaka 2000 hadi Tshs. 239.6 bilioni
mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 93.5.
(d) Kuongezeka kwa ajira viwandani kutoka
153,938 mwaka 2000 hadi 207,571 mwaka 2003 sawa na ongezeko la asilimia 34.8.
27. Serikali katika kutekeleza Ilani ya CCM ya
2000 katika Sekta ya Madini iliongozwa na Sera ya Madini ya mwaka 1997; Sheria
ya Madini ya mwaka 1998 na Kanuni za mwaka 1999. Sera hiyo ililenga kuvutia wawekezaji
binafsi. Azma ya kuwavutia wawekezaji
imefanikiwa kwa kiwango kikubwa. Utafiti wa madini uliongezeka na migodi mikubwa
ilifunguliwa. Ushiriki wa sekta binafsi
katika utafutaji na uchimbaji wa madini umewezesha kuwepo kwa migodi yenye
hadhi ya kimataifa kama vile Geita Gold Mine, Kahama Mining, Buhemba Gold Mine
(Musoma), Afrika Mashariki Gold Mine (Tarime) na Tulawaka Gold Mine
(Biharamulo). Kwa upande wa wachimbaji
wadogo wadogo, wamekuwa wakipatiwa mafunzo katika nyanja mbali mbali kama vile
uchimbaji salama wa madini, utunzaji wa mazingira, utafutaji wa madini,
biashara ya madini, masuala ya afya n.k.
Aidha, wachimbaji wadogo wadogo walifundishwa namna ya kupata mikopo
kutoka SIDO na taasisi nyingine zinazotoa mikopo. Kutokana na hatua hizo, sekta ya madini imeweza kupata mafanikio
yafuatayo katika kipindi cha 2000-2005:-
(a) Tanzania kwa sasa inazalisha takriban tani
50 za dhahabu kwa mwaka na kuifanya kuwa miongoni mwa nchi zinazoongoza katika
uzalishaji wa dhahabu Barani Afrika.
(b) Sekta ya Madini imekuwa kati ya sekta zenye
kasi kubwa ya ukuaji. Ukuaji
uliongezeka kutoka asilimia 13.9 mwaka 2000 hadi asilimia 14.1 mwaka 2004 ikiwa
ilifikia kilele cha asilimia 17.0 mwaka 2003.
(c) Mchango
wa sekta ya madini katika mauzo ya nje uliongezeka kutoka asilimia 26.9 mwaka
2000 hadi asilimia 51.4 mwaka 2004 na hivyo kuongoza katika mauzo ya nje
ikilinganishwa na mauzo ya bidhaa nyingine.
(d) Mchango wa sekta ya madini kwa mapato ya
fedha za kigeni umekua kutoka Dola za Kimarekani 178.2 milioni mwaka 2000 hadi
dola za Kimarekani 543.0 milioni mwaka 2004.
Hili ni ongezeko la asilimia 204.8.
(e) Watafutaji na wachimbaji madini wakubwa na
wadogo hulipa ada za leseni na mrabaha kwa madini wanayouza. Tangu mwaka 2000, maduhuli ya Serikali
yaliyokusanywa na Wizara yaliongezeka kutoka Shilingi 7.441 bilioni mwaka
2000/01 hadi Shilingi bilioni 22.786 mwaka 2003/04, likiwa ni ongezeko la
asilimia 206.2.
(f)
Migodi mikubwa imekuwa ikisaidia katika utekelezaji wa miradi ya jamii
kama vile afya, elimu, maji na barabara.
Huduma hizo huvinufaisha vijiji vinavyozunguka migodi hiyo. Baada ya uchimbaji madini kufikia kikomo, majengo
ya migodi hiyo yatatumika katika huduma za jamii kama vile kuanzisha shule au
huduma nyingine kulingana na vipaumbele vya wanajamii katika eneo husika.
(g)
Ajira rasmi katika migodi mikubwa imeongezeka kutoka 1,781 mwaka 1997
hadi 7,082 mwaka 2003 likiwa ni ongezeko la asilimia 297.6. Aidha, mwaka 2003 inakadiriwa kuwa
zilizalishwa nafasi 42,000 za ajira nje ya migodi kutokana na kuwapo kwa migodi
hiyo. Kwa upande wa kujiajiri,
inakadiriwa walikuwapo wachimbaji wadogo zaidi ya 500,000 waliokuwa wamejiajiri
wenyewe.
28. Biashara ni muhimu sana katika jitihada za kuongeza pato
la wananchi na kuendeleza uchumi. Dunia ya sasa ya utandawazi imeegemea sana
kwenye biashara ya kimataifa. Kwa
kutambua hilo, Serikali imeweka msukumo wa pekee katika kukuza mauzo ya bidhaa
zetu nje na kuongeza wingi na ubora wa bidhaa katika soko la ndani. Kutokana na msukumo huo hatua zifuatazo
zilichukuliwa katika kipindi kilichopita:-
(a)
Kuondoa kero ya ulipaji wa kodi ya makisio (provisional tax)
kabla ya hata kuanza biashara yenyewe.
Serikali iliweka wazi masharti ya kuanzisha biashara, viwango vya ada
kwa aina mbalimbali za biashara na hivyo kupunguza vishawishi vya rushwa.
(b)
Kushiriki katika majadiliano kuhusu mfumo wa biashara kimataifa. Mwezi
Julai, 20001, Tanzania iliandaa Mkutano
wa Mawaziri wa Biashara kutoka nchi maskini sana (LDCs) uliofanyika
Zanzibar. Tamko Rasmi la Zanzibar (Zanzibar
Declaration) liliweka msimamo wa pamoja katika mikutano ya Shirika la
Biahsara la Dunia (WTO) ya Doha, Qatar mwezi Novemba, 2001 na Cancun, Mexico,
mwezi Septemba 2003. Ushirikiano huo
ulizuia upitishaji wa agenda ambazo zingeendeleza na kuimarisha maslahi ya nchi
kubwa dhidi ya nchi changa. Mchango wa
Tanzania katika kujenga nguvu hii ulikuwa mkubwa.
(c)
Ili kukuza maendeleo ya kiuchumi, na hasa viwanda na biashara, Serikali
iliendelea kushirikiana na nchi majirani, hasa za Afrika Mashariki kupitia Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya
ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).
(d) Kutunga Sheria ya kudhibiti uingizaji holela
wa bidhaa kutoka nje ili kuilinda nchi yetu isigeuzwe kuwa dampo la bidhaa
hafifu kutoka nje.
(e) Kuanzisha maeneo huru ya biashara.
(f) Kuwasaidia wafanyabiashara wadogo wadogo
katika taaluma za ujasiriamali, namna ya kupata mikopo kutoka Mifuko mbali
mbali na Mabenki, na kurahisisha taratibu za kupata mikopo chini ya Mkakati
wa Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.
(g) Kupunguza mlolongo wa leseni kabla ya
kuanzisha biashara.
(h) Kutungwa sera na mikakati ifuatayo ikiwa ni
sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika kuwezesha ukuaji wa
biashara kubwa na ndogo:-
(i) Sera ya
Utekelezaji ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi.
(ii) MKUKUTA
(iii) MKURABITA
29. Kutokana na hatua hizo na nyinginezo,
mafanikio makubwa yamepatikana yakiwemo yafuatayo:-
(a)
Ukuaji wa Sekta ya Biashara uliongezeka kutoka asilimia 6.5 mwaka 2000
hadi asilimia 7.4 mwaka 2004.
(b)
Mauzo ya nje yaliongezeka kutoka Dola 663.3 milioni mwaka 2000 hadi
1,142.0 milioni mwaka 2003, likiwa ni ongezeo la asilimia 72.2.
(c)
Biashara imechangamka zaidi nchini
30. Ilani ya CCM katika kipindi cha 2000-2005
iliweka malengo yaliyokusudia kuimarisha na kuendeleza ushirika kama njia ya
kumwezesha Mtanzania wa kawaida hupambana na umaskini. Katika utekelezaji, hatua kadhaa
zilichukuliwa na mafanikio kupatikana kama ifuatavyo:-
(a)
Serikali ilibadilisha Sera ya Ushirika ya mwaka 1997 na kuifanyia
marekebisho Sheria ya Ushirika ya mwaka 1991 ili kuzifanya shughuli za ushirika
ziendane na mabadiliko katika uendeshaji uchumi wa soko. Sera ya Maendeleo ya Ushirika ilitungwa
mwaka 2002 na Sheria Mpya ya Vyama vya Ushirika ilitungwa upya mwaka 2003.
(b)
Wakulima, wafugaji, wavuvi na wachimba madini wadogo wadogo wameanza
kuingia katika utaratibu wa kuanzisha vyama vya ushirika wa kuweka na kukopa
(SACCOs).
(c)
Vyama vya ushirika vya kuweka na kukopa vimeongezeka kutoka 803 Mwaka
2000 hadi 1,719 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 114.1
(d)
Baadhi ya Mikoa na Wilaya imeanzisha benki za ushirika k.v. Kagera
Farmers Cooperative Bank, Kilimanjaro Cooperative Bank na benki za wananchi za
Dar es Salaam Community Bank na Mufindi Community Bank.
(e)
Hisa na akiba za wanachama zimeongezeka kutoka Shilingi 14.04 bilioni
mwaka 2000 hadi Shilingi 42.98 bilioni sawa na ongezeko la asilimia 20.6
(f)
Wanachama wa vyama vya Ushirika wa akiba na mikopo wameongezeka kutoka
133,134 mwaka 2000 hadi wanachama 251,631 mwaka 2004 sawa na ongezeko la
asilimia 89.0.
(g)
Mikopo iliyotolewa imeongezeka kutoka shilingi 11.52 bilioni mwaka 2000
hadi shilingi 54.14 bilioni mwaka 2004 sawa na asilimia 370.0.
(h)
Umeanzishwa utaratibu wa kutoa dhamana ya mikopo kwa vyama vya ushirika
(na wafanyabiashara binafsi ili kununulia mazao (Export Credit Guarantee
Scheme). Dhamana hiyo imevisaidia
sana vyama vya ushirika kununua mazao ya wakulima katika ushindani na makampuni
binafsi. Wanachama wameanza tena kuwa na imani na vyama vyao vya ushirika. Bila ya utaratibu huo baadhi ya vyama vya
ushirika vingekufa.
(i)
Vyama vya ushirika vimeruhusiwa kuuza moja kwa moja mazao ya wanachama
wake nje ya nchi.
(j)
Vyama vya ushirika vimepewa uwezo wa kushitaki moja kwa moja wale
wanaosababisha wizi na ubadhirifu katika ushirika.
(k)
Chuo cha Ushirika Moshi kimepandishwa hadhi na kuwa Chuo Kikuu
Kishiriki (cha Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine).
Maendeleo Ya Masoko
31. Tanzania ina fursa kubwa ya kukuza soko la ndani na la nje kwa kupitia mikataba na makubaliano mbalimbali. Jitihada kubwa zimefanywa katika kuwaelimisha wakulima kuzalisha mazao kibiashara na hasa kuzingatia mahitaji ya soko, hususan ubora, madaraja na ufungashaji. Katika kipindi cha 2000/2001 – 2004/2005, Tanzania imejipatia mafanikio kutokana na kuongezeka kwa uuzaji wa mazao yaliyomo katika makubaliano hayo. Tanzania ni mwanachama katika mikataba na makubaliano kama vile:-
(a) Soko la Amerika kwa mujibu wa “African
Growth and Opportunity Act” – AGOA.
(b) Jumuiya ya Ulaya (EU) chini ya utaratibu wa
“Every thing But Arms. (EBA)”
(c) Upendeleo maalumu unaotolewa na baadhi ya
nchi marafiki.
(d) Jumuiya ya Afrika Mashariki.
(e) Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa
Afrika (SADC).
32. Ununuzi na mauzo yanayofanywa na makampuni
yanayosafirisha mazao ya biashara asilia (traditional export crops) kama
kahawa, chai, tumbaku, mkonge na pamba umekuwa ukiongezeka katika kipindi cha
miaka kumi iliyopita isipokuwa zao la pamba.
Katika kipindi cha 1995 hadi 2000, uzalishaji wa zao la pamba ulishuka
kwa asilimia 14. Hata hivyo, katika
kipindi cha 2000 hadi 2004, zao hilo pamoja na lile la tumbaku yameonekana
kuongezeka zaidi kuliko mazao mengine.
33. Matatizo yanayoendelea kuathiri uzalishaji
usiwe mkubwa zaidi ni pamoja na kutegemea zaidi mvua, mabadiliko ya hali ya
hewa (hasa ukame), uduni wa miundombinu ya masoko ambayo imekuwa ikiongeza
gharama za usafirishaji, upungufu wa taarifa za mahitaji ya masoko hasa ya nje,
upungufu wa mitaji kwa wafanyabiashara wadogo wadogo na uingizwaji holela wa
bidhaa kutoka nje.
34. Katika jitihada za kupunguza matatizo na
kuongeza ufanisi, hatua zifuatazo miongoni mwa nyingine zilichukuliwa katika kipindi
kilichopita:-
(a) Kuendelea na maonyesho ya Sikukuu ya
Wakulima (Nane Nane).
(b) Kuwashirikisha wazalishaji katika Maonyesho
ya Kimataifa kama yale ya mboga mboga na matunda kule Rostock, Ujerumani
(2003/2004) na Maonyesho ya Mazao ya Chakula kule Moscow (2004/2005). Maonyesho ya Rostock yameanza kuwanufaisha
wakulima wadogo wadogo kwa kuingia mikataba (contract farming) ya
kuyauzia makampuni makubwa ambayo yanashughulikia biashara ya kimataifa.
(c) Kuanzishwa kwa mradi wa Uendelezaji
Miundombinu ya Masoko Vijijini. Mradi
huu unatekelezwa na Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (MVIWATA) kwa
lengo la kuwa na soko la uhakika la mazao yanayozalishwa na wakulima. Mradi huu unatekelezwa katika Wilaya za
Kongwa na Mvomero.
(d) Kuanzishwa kwa Programu ya Kuendeleza Mifumo
ya Masoko ya Mazao ya Kilimo (Agricultural Marketing Systems Development
Programme). Moja ya malengo ya programu
hii ni kuimarisha miundombinu ya masoko vijijini hasa barabara na maghala ili
kupunguza gharama za uzalishaji na usafirishaji hivyo bidhaa zetu kuweza
kushindana na bidhaa kutoka sehemu yo yote duniani.
(e) Kuandaa Sera ya Masoko ya Mazao ya Kilimo
Yenye mwelekeo wa kuwaunganisha wazalishaji wakubwa na wadogo kwa upande mmoja
na wanunuzi/wasindikaji wa mazao ya kilimo na mifugo kwa upande mwingine kwa
lengo la kupata soko la uhakika na bei nzuri.
35. Ardhi
ni sekta yenye umuhimu mkubwa katika ujenzi wa uchumi wetu na upunguzaji
wa umaskini nchini. Katika kipindi cha 2000-2005, Serikali imeendelea kuboresha
maisha ya wananchi kwa kupambana na kero mbali mbali za ardhi na makazi. Hatua zilizochukuliwa na mafanikio
yaliyopatikana ni pamoja na ifuatavyo:-
(a) Sera ya Taifa ya Ardhi, Sheria ya Ardhi,
Sheria ya Ardhi ya Vijiji na Sheria ya Mahakama za Ardhi zimeendelea kutumika
ipasavyo. Aidha wananchi wameendelea
kuelimishwa kuhusu Sheria za Ardhi ili waitambue ardhi wanayomiliki kuwa ni
raslimali ya kuwaondolea umaskini na waweze kupanga mipango ya matumizi bora ya
ardhi hiyo.
(b) Sheria ya Ardhi ya Vijiji imeziwezesha
Halmashauri za Vijiji kupata vyeti vya Ardhi ya Vijiji na kusajili Hatimiliki
za Kimila za Ardhi kwa wakazi wake;
(c) Umilikaji wa ardhi kimila vijijini
umeboresha usalama wa miliki na umetoa fursa ya kutumia hati miliki hizo kama
dhamana katika Vyombo vya Fedha, Mahakama na Taasisi za Elimu ya Juu;
(d) Katika Mikoa minane ya Tanzania Bara mipaka
ya Vijiji 2048 imepimwa kwa kutumia vifaa vya kisasa. Mikoa hiyo ni: Arusha,
Kilimanjaro, Manyara, Mbeya, Morogoro, Ruvuma, Shinyanga na Singida;
(e) Msukumo mkubwa ulielekezwa katika upimaji wa
viwanja mijini na vijijini na pia wa mashamba makubwa kwa ajili ya
uwekezaji. Mikoa yenye idadi kubwa ya
mashamba yaliyopimwa ni: Mbeya (12,660);
Dar es Salaam (1,261); Pwani (1,097); Arusha (608); Tanga (325); Morogoro
(238); Kilimanjaro (207); Kagera (151) na Iringa (99). Kumbukumbu zimetunzwa kwa kufungua majalada
52,000 ya viwanja na mashamba na kuyaingiza kwenye Kompyuta;
(f) Kwa kutumia Mabaraza ya Usuluhishi wa Ardhi
na Mabaraza ya Nyumba, jumla ya mashauri ya ardhi 5,703; kesi za nyumba 6,765;
rufaa za ardhi 581 na rufaa za nyumba 523 zilisikilizwa na kutolewa uamuzi;
(g) Umeanzishwa mpango wa kurasimisha rasilimali
na biashara (MKURABITA) ambao utaihusu sana sekta ya ardhi kwani
wananchi wengi wanamiliki rasilimali ya ardhi kwa njia zisizo rasmi.
Nishati
36. Nishati (hasa umeme) ni nyenzo ya msingi
katika uchumi kwani viwanda na shughuli nyingi za kiuchumi zinategemea
umeme. Katika kipindi cha 2000 - 2005,
hatua zilizochukuliwa kuikuza sekta hii na mafanikio yaliyopatikana ni kama
ifuatavyo:-
(a)
Katika kipindi cha 2000 – 2005, umeme umepelekwa katika miji mikuu ya
Wilaya nane zifuatazo: Geita, Igunga, Mbarali, Meatu, Mkuranga, Ruangwa,
Tandahimba na Sikonge. Hadi kufikia
mwisho wa mwaka 2005, miji mikuu ya Wilaya za Ngara, Biharamulo, Rufiji,
Serengeti, Ukerewe na Urambo itakuwa imepatiwa umeme. Hatua zimeanza kuchukuliwa ili kufikisha umeme katika miji ya
Wilaya za Bukombe, Kilindi, Simanjiro,
Kibondo na Kasulu.
(b)
Kati ya mwaka 2002 na 2004, umeme ulisambazwa kwa vijiji 197;
(c)
Urekebishaji wa uendeshaji wa TANESCO.
(d)
Gesi ya Songo Songo ilianza kuzalisha umeme Oktoba 2004 kwa kuendesha
mitambo 4 ya Ubungo yenye uwezo wa kuzalisha MW 112 za umeme. Pia viwanda vya bia (TBL), saruji (Wazo
Hill) na Kioo Limited vimeanza kutumia gesi hii kama nishati katika uzalishaji;
(e)
Zimeandaliwa taratibu za kuanza kuunganisha umeme katika miji na vijiji
vilivyomo mipakani na nchi za Zambia, Uganda na Kenya
(f)
Umesainiwa mkataba wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi ya Mnazi Bay kwa
ajili ya miji ya Mtwara na Lindi;
37. Mtandao wa barabara ambao umeendelea
kujengwa upande wa Tanzania Bara una urefu wa kilomita 84,950. Kati ya hizo, Serikali Kuu husimamia
kilomita 10,300; Serikali za Mitaa kilomita 49,950 na Vijiji kilomita
24,700. Ukiondoa kilomita 795 za
barabara kuu na kilomita 673 za barabara za Vijijini ambazo ziliendelezwa
katika kipindi cha 1995-2000, mafanikio ya kipindi cha 2000-2005 ni haya
yafuatayo:-
(a)
Jumla ya kilomita 28,051 za barabara kuu na 30,653 za barabara za Mikoa zimetengenezwa;
(b)
Madaraja 2,790 ya barabara kuu na
2,144 ya barabara za Mikoa
yametengenezwa;
(c)
Kuzifanyia matengenezo makubwa
km. 989 na ya kawaida km. 2716 ya barabara za Mikoa ya Ruvuma na Iringa
Kusini.
(d)
Ujenzi wa daraja la Mto Rufiji
(Daraja la Mkapa) ulikamilika na
lilifunguliwa Agosti, 2003.
(e)
Hadi kufikia mwaka 2004/2005 wa Fedha, Serikali inaendelea na
kuzifanyia matengenezo kilomita 13,474 za barabara na madaraja 1,692 katika
barabara kuu na za Mikoa;
(f)
Kutokana na kuimarisha ukusanyaji wa kodi nchini, Serikali imebuni na
kuanza kutekeleza Mradi Maalum wa Ujenzi wa Barabara Kuu kwa kiwango cha lami
kwa kutumia fedha zetu wenyewe. Jumla
ya kilomita 469 zinajengwa katika kiwango cha lami kwa utaratibu huu;
(g)
Kukaribishwa kwa Sekta binafsi
kushiriki katika ujenzi wa miradi ya barabara, madaraja na majengo ya
Serikali;
(h)
Kukamilishwa na kuidhinishwa
rasmi kwa Sera ya Taifa ya Ujenzi ambayo ni Mwongozo wa utekelezaji wa shughuli
zote za Sekta ya Ujenzi.
(i)
Kuvifanyia ukarabati vivuko 8 vya:-
Pangani (Tanga), Ruhuhu
(Ruvuma), Ilagala (Kigoma), Kigongo - Busisi na Kome (Mwanza), Magogoni (Dar es
Salaam), Rufiji (Pwani) na Kyanyabasa (Kagera).
(j)
Vilinunuliwa vivuko vipya vya: Kilombero, Bugolora-Ukara na Kilambo
(Tanzania - Msumbiji).
(k)
Baadhi ya Barabara kuu za jiji
la Mwanza zilitengenezwa kwa kiwango cha lami.
38. Katika kipindi cha 2000-2005, hali ya usafiri na usafirishaji kwa jumla iliendelea kuwa nzuri kutokana na miundombinu ya barabara na reli kuwa bora zaidi na vyombo vya usafiri na usafirishaji wa ardhini, baharini na angani kuongezeka. Hatua zilizochukuliwa pamoja na mafanikio yaliyopatikana yalikuwa kama ifuatavyo:-
(a)
Sekta binafsi iliendelea kuleta mapinduzi katika usafirishaji mijini na
vijijini kwa kuongeza idadi na ubora wa mabasi na njia (routes)
yaliyohudumia. Hivyo hivyo kwa malori
ya uchukuzi wa mizigo.
(b)
Yalifanyika maandalizi ya kuanzisha mradi wa mabasi ya usafiri wa haraka
(CBRT) jijini Dar es Salaam.
(c)
Shirika la Reli Tanzania (TRC) lilitandika kilometa 62.5 mpya za reli
na kumwaga kokoto kilometa 112 katika maeneo mbalimbali. Injini 92, mabehewa 469 ya mizigo na 48 ya
abiria yalikarabatiwa. Aidha, ujenzi wa
njia ya mawasiliano kati ya Morogoro na Tabora ulikamilika.
(d)
TAZARA nayo ilikarabati mabehewa 2,736 ya mizigo na 142 ya abiria
pamoja na njia ya reli kwa kuchomelea kutoka Dar es Salaam hadi Igurusi
(kilometa 657).
(e) Ili kuimarisha ubora wa huduma za uchukuzi
kwa wananchi waishio kando kando ya maziwa makuu, Serikali ilijenga magati ya
Kinesi, Bugando, Nansio na Shirati.
Yote yako katika Ziwa Victoria.
Aidha, ukarabati wa gati la Kasanga umekamilika na ujenzi wa gati la
Karema katika Ziwa Tanganyika; Kiamkwikwi,
Maisome na Kome katika Ziwa Victoria unaendelea. Maandalizi ya ujenzi wa gati la Manda
na Mbamba Bay yalifanyika.
(f) Kwa upande wa ukanda wa Mtwara ambao unaanzia bandari ya Mtwara hadi Mbamba Bay na kuunganisha mikoa ya Kusini (Mtwara, Lindi na Ruvuma) na Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, mpango wa utekelezaji ulikamilishwa. Wawekezaji walihamasishwa kuwekeza katika maeneo mbalimbali kama vile barabara, reli, usafiri kwa njia ya maji na anga, kilimo, utalii na viwanda.
(a)
Katika kuboresha usafiri wa anga, juhudi zilizofanywa ni pamoja
naKununua Meza na Radio za kuongozea ndege Zanzibar, Arusha, Mwanza na kufungwa
katika viwanja hivyo; kufunga mitambo ya mionzi ya jua, kuboresha nguvu za umeme katika viwanja vya
Kigoma, Mtwara, Songea na Zanzibar; kununua mitambo ya kuongozea ndege katika
viwanja vya ndege vya Mtwara na Mbeya; kuzindua huduma za Rada kwa saa 24
Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaam; na kununua vifaa vya kuzimia moto. Aidha, ujenzi wa Uwanja mpya wa Ndege wa
Songwe, Mbeya uliendelea na matengenezo
mbalimbali ya viwanja vilivyopo yalifanyika ili kuwezesha ndege kutua na kuruka
kwa usalama.
(h) Ufanisi wa Bandari ya Dar
es Salaam umeongezeka kutoka uwezo wa kuhudumia makontena 10 kwa saa mwaka 2000
hadi 25 mwaka 2005. Kwa kigezo hicho,
Bandari hiyo hivi sasa ndiyo yenye ufanisi mkubwa kuliko zote katika eneo la
Mashariki na Kusini mwa Afrika.
39. Sekta ya mawasiliano imeleta mapinduzi
makubwa ya kiuchumi na kijamii nchini mwetu katika kipindi cha miaka 10
iliyopita, hasa kutokana na kupanuka kwa haraka sana kwa mtandao wa simu za
mikononi na matumizi ya mtandao wa internet. Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, hatua zilizochukuliwa
na mafanikio yaliyopatikana ni kama ifuatavyo:-
(a) Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL) iliweka
mtambo wenye uwezo wa kupokea malipo kabla ya huduma (pre-paid system)
katika miji ya Dar es Salaam, Arusha, Mwanza, Dodoma na Zanzibar. Aidha, ilipanua huduma za simu za mezani kwa
kuifikisha katika maeneo muhimu ya uchumi kama vile migodi ya dhahabu ya Kahama
na Buhemba, Kiwanda cha Saruji cha Tanga, Kiwanda cha Sukari cha Kagera na
kwenye Mashamba ya Chai ya Kibena na Mufindi.
Pia mitambo ya zamani ya analogue ilibadilishwa kwa kuweka
mitambo ya kisasa aina ya digital katika baadhi ya miji. Mtandao wa simu nchini umefikia wamiliki 5
wa simu kwa kila watu 100 (yaani teledensity ya 5/100).
(b) Katika eneo la simu za mkononi, kampuni mpya
ya Celtel ilianza kutoa huduma ikiongezea juu ya zile zilizokuwa zikitolewa na
Vodacom, Zantel na Mobitel.
(c) Idadi ya wenye simu za mezani na za mkononi
iliongezeka kutoka 300,237 mwaka 2000 hadi 2,115,591 mwaka 2004. Hili ni ongezeko la asilimia 604.6.
(d) Serikali imeweza kuweka mtandao wa tovuti
katika vituo vya mikoa 26 (regional points) isipokuwa mitatu ambayo ni
Lindi, Rukwa na Ruvuma. Tanzania sasa
ina internet Service Providers 25 na internet cafes 4,000.
(e) Utoaji huduma kibiashara
umesaidia Shirika la Posta kuongeza ufanisi na ubora wa huduma zake kwa
wateja.Idadi ya makampuni yenye leseni za kutoa huduma za posta imeongezeka
kutoka makampuni 13 mwaka 2000 hadi makampuni 29 mwaka 2004.
(f) Tanzania iliongeza kasi ya kuingia katika
mfumo wa Jamii Habari (Information society). Huu ni mfumo wa
maisha ambamo jamii ina haki na uwezo wa kuwasiliana, kujifunza na kupashana
habari bila vikwazo. Kwa kutambua
umuhimu huo, Serikali ilitoa Sera ya Habari mwaka 2003 ili kuleta mabadiliko
katika matumizi ya teknolojia za habari na mawasiliano (TEKNOHAMA). Vituo vinane vya mawasiliano (telecenters)
vimejengwa. Vituo hivyo ni pamoja na
Tanzania Global Distance Learning Centre
(Dar es Salaam); Sengerema Telecenter, Kasulu Internet Café; Ngara UNHCR
Telecenter, Wino Telecenter; Multipurpose Telecenter Kinampanda, Mpwapwa na
Mtwara. Vituo hivi vinatumiwa na jamii
katika kueneza matumizi ya TEKNOHAMA.
40. Sekta ya Fedha ni huduma ya kiuchumi ambayo
ni mwezeshaji mkuu siyo tu wa shughuli za kiuchumi, bali pia hata
miundombinu. Kupanuka na kuendelea kwa
Sekta ya Fedha kumechangia kwa kiasi kikubwa katika kuchangamsha biashara na
kukua kwa uchumi.
41. Kufikia mwaka 2004, Sekta ya Fedha iliweza
kuchangia asilimia 12.1 katika Pato la Taifa.
Huduma za mabenki ziliimarika ambapo baadhi yake yalianza tena kutoa
mikopo kwa shughuli mbali mbali za kiuchumi, ikiwa ni pamoja na mikopo kwa
vyama vya ushirika kwa ajili ya kununulia mazao ya wakulima.
Elimu
42. Elimu ni nyenzo ya msingi katika jitihada za kujenga uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea na kuwawezesha kiuchumi wananchi. Uchumi wa kisasa unahitaji watenda kazi wenye maarifa yanayohusu kanuni na maarifa ya kumudu vitendea kazi vya aina mbalimbali. Aidha, elimu ni sehemu ya mkakati muhimu wa Kitaifa wa kukabiliana na changamoto za utandawazi na modenaizesheni ya uchumi na sekta zote nyingine. Kwa kuzingatia hoja hizi, elimu imekuwa ikipewa umuhimu mkubwa na CCM na Serikali zake.
43. Katika kipindi cha 2000-2005, Serikali
imepanua, kuimarisha na kuboresha elimu kwa kiwango cha juu. Bajeti ya elimu imekuwa ikiongezeka mwaka
hadi mwaka kwa lengo la kutekeleza majukumu katika sekta ya elimu. Mgao wa Elimu katika Bajeti ya Serikali
umeongezeka kutoka asilimia 21.8 mwaka 1999/2000 hadi kufikia asilimia 35.6
mwaka 2003/2004 kwa ajili ya kupanua, kuimarisha na kuboresha elimu.
Elimu ya Awali
44. Elimu ya Awali ni muhimu katika kuwajenga
watoto katika msingi imara wa elimu.
Mafanikio yaliyopatikana katika Elimu ya Awali ni kama ifuatavyo:-
(a) Idadi ya shule za awali zilizoandikishwa, za
Serikali na zisizo za Serikali, imefikia 12,984 mwaka 2004.
(b) Madarasa ya Elimu ya Awali katika shule za
msingi za Serikali yameongezeka kutoka 5,234 mwaka 2000 hadi kufikia 9,701
mwaka 2004. Ongezeko hili la madarasa
4,457 ni sawa na asilimia 85.3.
(d)
Watoto wa umri wa miaka 5-6 walioandikishwa kwa Elimu ya Awali nchini
wameongezeka kutoka 310,933 mwaka 2000 hadi 960,470 ikiwa ni ongezeko la watoto 649,537 sawa na asilimia 208.9.
Elimu ya Msingi
45. Serikali ya CCM ya Awamu ya Tatu imeweka
mkazo mkubwa kwenye elimu ya msingi ili kuhakikisha kwamba Watanzania
wanaostahili elimu hiyo wanaipata na wanaipata kwa kiwango kilicho bora. Ili kutekeleza azma hiyo, Serikali imebuni Mpango
wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) 2002-2006. MMEM umeboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia
mashuleni. Mpango huu umehakikisha
kwamba yanakuwepo majengo mazuri na ya kutosha
ya shule, walimu, vitabu vya kiada na ziada, vifaa vya kufundishia na
kujifunzia na mkao sawa darasani.
46. MMEM ukisaidiwa na Mfuko wa
Maendeleo ya Jamii (TASAF) na kwa ushirikishaji mkubwa wa wananchi umeleta mabadiliko makubwa katika sekta ndogo
ya elimu ya msingi kama ifuatavyo:-
(a) Kuanzia mwaka 2002 hadi 2004 yamejengwa
madarasa 45,000; nyumba za walimu 8,527; kununuliwa madawati 285,898 na matundu
ya vyoo 98,827. Aidha kazi ya ujenzi wa
majengo mapya ilikwenda sambamba na ukarabati wa majengo ya zamani nchi nzima.
(b) Idadi ya shule za msingi za Serikali
imeongezeka kutoka 11,608 mwaka 2000 hadi 13,533 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko
la shule 1,925 sawa na asilimia 16.6.
(c) Lengo maalum la uandikishaji (GER) la
asilimia 85 ifikapo mwaka 2002 lilivukwa kwa kufikia watoto wote
walioandikishwa kuwa asilimia 98.6 ya idadi ya rika husika mwaka 2002 na
kuongezeka hadi asilimia 106.3 mwaka 2004. GER kwa
jumla iliongezeka kutoka asilimia 77.6 mwaka 2000 hadi asilimia hiyo 106.3
mwaka 2004, lengo la Ilani likiwa limekiukwa.
(d) Idadi ya wanafunzi katika shule za msingi
imeongezeka kutoka 4,382,410 mwaka 2000 hadi 7,083,063 mwaka 2004. Ongezeko hili la wanafunzi 2,700,653 ni sawa
na asilimia 61.6.
(e) Kima cha watoto wa rika lengwa la elimu ya
msingi (miaka 7-13) walioko shuleni imeongezeka kutoka asilimia 58.8 mwaka 2000
hadi 90.1 mwaka 2004.
(f) Upatikanaji wa vitabu vya kiada umeongezeka
kutoka uwiano wa kitabu kimoja kwa wanafunzi 8 katika madarasa ya I-IV hadi
wanafunzi 1.3. Kwa madarasa ya V-VII.
(g)
Kiwango cha kufaulu mtihani wa kumaliza elimu ya msingi kimeongezeka
kutoka asilimia 22 mwaka 2000 hadi asilimia 48.6 mwaka 2004. Idadi ya wanafunzi walioendelea na masomo ya
sekondari iliongezeka kutoka 74,432 mwaka 2000 hadi 147,490 mwaka 2004 sawa na
ongezeko la asilimia 90.2.
(h) Serikali imetoa mafunzo kwa Kamati za Shule
za Msingi nchi nzima ili wajumbe wa Kamati hizo wajue wajibu na madaraka yao
katika kupitisha na kusimamia mipango yote na matumizi ya fedha za shule.
(i) Serikali imefuta ada na michango mbalimbali
ya shule za msingi kwa lengo la kuifanya elimu ya msingi kuwa bure na lazima
ili isiwe kikwazo kwa watoto wa familia maskini kujiunga na kubakia shuleni
hadi wahitimu elimu hiyo.
Elimu ya Sekondari
47. Ili kupanua, kuimarisha na kuboresha elimu
ya sekondari, Serikali imebuni Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari
(MMES) 2004-2009.
48. Katika kipindi cha 2000-2005, hatua
zilizochukuliwa na mafanikio yaliyopatikana ni kama ifuatavyo:-
(a) Kutokana na juhudi kubwa za wananchi, idadi
ya shule za sekondari imeongezeka kutoka 927 mwaka 2000 hadi 1,333 mwaka
2004. Ongezeko hili la shule za
sekondari 406 ni sawa na asilimia 43.8.
(b) Idadi ya wanafunzi wa Kidato cha 1-6
imeongezeka kutoka 261,896 mwaka 2000 hadi 435,642 mwaka 2004 ambalo ni
ongezeko la wanafunzi 173,746 sawa na asilimia 66.3.
(c) Idadi ya wanafunzi wasichana katika shule za
sekondari imeongezeka kutoka 120,248 mwaka 2000 hadi 204,528 mwaka 2004. Hili ni ongezeko la wanafunzi wasichana
84,280 sawa na asilimia 70.1.
(d) Mwachano kati ya idadi ya wasichana na
wavulana umezidi kupungua. Wanafunzi
wasichana walikuwa asilimia 45.9 ya wanafunzi wote mwaka 2000 na asilimia 46.9
mwaka 2004.
(e) Serikali ilitenga ruzuku maalum katika
Bajeti yake sh. 1.1 bilioni mwaka
2002; sh. 2.5 bilioni mwaka 2003 na sh.
4.3 bilioni mwaka 2004 kwa ajili ya
kugharamia elimu ya sekondari ya watoto
wa familia maskini.
(f) Serikali imepunguza ada ya elimu ya
sekondari katika shule za Serikali kutoka shilingi 40,000 hadi shilingi 20,000.
(g) GER ya Kidato cha 1-4 imeongezeka kutoka
asilimia 8.5 mwaka 2000 hadi asilimia 13.0 mwaka 2004.
(h)
GER ya Kidato cha 1-6 imeongezeka kutoka asilimia 6.4 mwaka 2000 hadi
7.4 mwaka 2004.
(i) Ufaulishaji katika Mtihani wa Kidato cha 4
katika Daraja la I-III shule za serikali uliongezeka kutoka asilimia 35.6 mwaka
2000 hadi asilimia 45.6 mwaka 2004.
(j) Ufaulu Kidato cha 6 Daraja la I-III
uliongezeka kutoka asilimia 81.4 mwaka 2000 hadi asilimia 86.4 mwaka 2004.
Elimu ya Ualimu:
49. Katika kuhakikisha
kuwa mipango ya MMEM na MMES inatekelezwa ipasavyo, Serikali
imeongeza nafasi za mafunzo ya ualimu na kutoa ajira mpya kwa walimu. Mafanikio
yaliyopatikana kipindi kilichopita katika elimu ya ualimu ni kama ifuatavyo:
(a) Idadi ya wanafunzi wa mafunzo ya ualimu
tarajali wa Daraja A katika Vyuo vya Ualimu imeongezeka kutoka 3,303 mwaka 2000
hadi 24,873 mwaka 2004. Ongezeko hili
la wanafunzi 21,570 ni sawa na asilimia 653.0
(b) Idadi ya wanafunzi wa mafunzo ya ualimu
tarajali wa Stashahada katika Vyuo vya Ualimu imeongezeka kutoka 2,511 mwaka
2000 hadi 4,693 ambalo ni ongezeko la wanafunzi 2,182 sawa na asilimia 86.9.
(c) Jumla ya walimu wapya 37,261 wa Daraja A na
Stashahada wameajiriwa kati ya mwaka 2000 na 2004. Miongoni mwa walimu hao, 15,000 ni wale waliohitimu mafunzo ya
ualimu miaka iliyopita wakati ajira ilipokuwa imesitishwa. Uajiri wa walimu hao uliondoa kero kubwa
iliyokuwa ikisemwa sana katika jamii.
(d) Kuanzia mwaka 2003, wanafunzi wa mafunzo ya
ualimu tarajali wamekuwa wakiajiriwa moja kwa moja baada ya kuhitimu mafunzo
yao.
(e) Kati ya mwaka 2000 na 2004, vibali vya ajira
mbadala viliombwa na kutolewa ili kujaza mapengo ya jumla ya walimu 1,134
walioacha au kuachishwa kazi kutokana na sababu mbalimbali.
Elimu ya Juu
50. Ili Taifa liweze kuwa na maendeleo endelevu
na kuondokana na umaskini, elimu ya juu ni lazima ipewe kipaumbele. Katika kipindi cha 2000-2005, elimu ya juu
imepata mafanikio yafuatayo:-
(a)
Idadi ya Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki imeongezeka kutoka 14 mwaka
2000 hadi 20 mwaka 2004 ambalo ni
ongezeko la vyuo 6 sawa na asilimia 42.9.
(b)
Idadi ya Vyuo Vikuu na Vyuo Vikuu Vishiriki Binafsi vimeongezeka kutoka
9 mwaka 2000 hadi 13 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko la vyuo 4 sawa na asilimia
44.4.
(a)
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vya umma imeongezeka kutoka
wanafunzi 21,983 mwaka 2000 hadi wanafunzi 40,184 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko
la wanafunzi 18,201 sawa na asilimia 82.8.
(b)
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu binafsi imeongezeka kutoka 1,373
mwaka 2000 hadi 2,764 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko la wanafunzi 1,391 sawa na
asilimia 101.3.
(c)
Idadi ya wanafunzi wa kike katika vyuo vikuu imeongezeka kutoka 5,213
mwaka 2000 hadi 11,782 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 6,569 sawa na
asilimia 126.01.
(d)
Kwa lengo la kupanua uwezo wa kutoa huduma za afya, Serikali imetoa
udhamini kwa wanafunzi madaktari 256 wa mwaka wa kwanza (2004/2005) na 128 wa
mwaka wa pili wanaosoma kwenye vyuo vikuu binafsi, na vyuo vikuu vya umma wenye
udhamini binafsi.
(e)
Serikali imeanzisha Mamlaka ya Elimu Tanzania kwa lengo la kusimamia
Mfuko wa Elimu ili kuinua ubora wa elimu, kuongeza udahili wa wanafunzi na
upatikanaji wa elimu hiyo kwa usawa.
(f)
Mfuko wa Elimu ulioanzishwa mwaka 2001, hadi kufikia Desemba 2004
ulikuwa umetoa shilingi bilioni 16.1 kwa taasisi za umma na binafsi.
(g)
Hadi kufikia Desemba 2004, Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE)
lilikuwa limefanikiwa kuvipatia ithibati vyuo 22 na usajili vyuo 126 kwa lengo
la kutoa elimu ya ufundi.
(h)
Mwaka 2004, Serikali ya Jamhuri ya Muungano ilikikabidhi Chuo cha
TANESCO Morogoro kwa Taasisi ya Kiislamu (Islamic Foundation) kwa matumizi kama
Chuo Kikuu.
(i)
Hadi kufikia Desemba 2004, Baraza la Ithibati la Elimu ya Juu (HEAC)
lilikuwa limetoa ithibati kwa vyuo vikuu vya umma na binafsi 8, limesajili vyuo
vikuu 11 na limetoa barua ya kuviendesha vyuo vikuu 4.
(j)
Kutungwa kwa Sheria ya Bodi ya Mikopo kwa lengo la kutoa mikopo kwa
wanafunzi wa taasisi za elimu ya juu.
Elimu ya Ufundi
51. Elimu ya Ufundi ina nafasi ya msingi katika
kupanua maendeleo na matumizi ya sayansi na teknolojia ambayo ni muhimu katika
ujenzi wa uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea. Elimu ya Ufundi imepata mafanikio yafuatayo katika kipindi cha
2000 - 2005:-
(a)
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vya ufundi imeongezeka kutoka 2,049
mwaka 2000 hadi 2,103 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko la wanafunzi 54 sawa na
asilimia 2.6.
(b)
Idadi ya wanafunzi wa kike katika vyuo vya ufundi imeongezeka kutoka143
mwaka 2000 hadi 245 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 102 sawa na
asilimia 71.3.
(c)
Vyuo vya ufundi stadi vilivyosajiliwa na VETA vimeongezeka kutoka 574
mwaka 2000 hadi 794 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la vyuo 220 sawa na asilimia
38.
(d)
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vya ufundi stadi imeongezeka kutoka
4,525 mwaka 2000 hadi 15,554 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko la wanafunzi 11,029
sawa na asilimia 243.
(e)
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vilivyosajiliwa na VETA imeongezeka
kutoka 38,400 mwaka 2000 hadi 50,075 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi
11,675 sawa na asilimia 30.
(f)
Uwiano kati ya wasichana na wavulana katika vyuo vya ufundi stadi VETA
ulikuwa asilimia 21 mwaka 2000 na kuongezeka hadi asilimia 38 mwaka 2004.
(g)
Idadi ya stadi zinazofundishwa katika vyuo vya ufundi stadi
zimeongezeka kutoka 38 mwaka 2000 hadi 90mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la stadi
52 sawa na asilimia 137.
(h)
Idadi ya walimu wanafunzi wa ufundi stadi imeongezeka kutoka 28 mwaka
2000 hadi 114 mwaka 2004 ikiwa ni ongezeko la walimu wanafunzi 86 sawa na
asilimia 307.
Elimu ya Watu Wazima
52. Ili kuzipa msukumo jitihada za kuwawezesha wananchi kiuchumi na kujenga uchumi wa kisasa wa Taifa linalojitegemea, inabidi kutoa kipaumbele kwenye Elimu ya Watu Wazima, hususan elimu yenye manufaa ambayo inaendeleza maarifa ya kisasa yenye kuwasaidia wahusika kuongeza ufanisi na tija katika kazi zao wanazozifanya. Mafanikio yaliyopatikana katika elimu ya watu wazima katika kipindi cha 2000 - 2005 ni haya yafuatayo:-
(a)
Kupunguza ongezeko la watoto na vijana wasiojua kusoma, kuandika na
kuhesabu kwa kutumia utaratibu mpya wa elimu ya msingi bure na ya lazima.
(b)
Serikali imeanzisha Mpango wa Elimu ya Msingi kwa Walioikosa (MEMKWA).
(c)
Serikali imeboresha utoaji wa elimu ya watu wazima kwa kutumia mbinu
shirikishi ya reflekti ambapo walengwa wanajifunza kusoma, kuandika na kuhesabu
kwa namna inayowasaidia kujiongezea ujuzi katika shughuli zao za kiuchumi
katika maeneo yao.
53. Sekta ya Afya ambayo ina umuhimu mkubwa sana
katika kupambana na umaskini na kuleta ustawi wa jamii imeshuhudia maendeleo
makubwa katika miaka 10 ya uongozi wa Awamu ya Tatu. Katika mageuzi yaliyoanzia 1993, mabadiliko yasiyo kifani
yametokea katika Sekta ya Afya kufuatia kutekelezwa kwa shabaha ya kuinua
kiwango cha ubora wa huduma za afya zinazotolewa kwa wananchi, pamoja na
kuboreshwa kwa ufanisi wa menejimenti na utendaji wenyewe.
54. Katika kipindi cha 2000 hadi 2005, hatua
zilizochukuliwa na mafanikio yaliyopatikana ni kama ifuatavyo:-
(a)
Kuanzisha na kutekeleza sera ya uchangiaji huduma za afya iliyolenga
kuongeza uwezo wa Serikali kugharimia huduma za afya. Kero mbalimbali zimeondolewa au kupungua sana kufuatia
kutekelezwa kwa sera hiyo zikiwemo:-
(i) Upatikanaji wa dawa na vifaa vya tiba
katika hospitali umeongezeka.
(ii) Kufanyika kwa ukarabati wa majengo ya
kutolea huduma za afya palepale fedha zilipokusanywa kumeboresha huduma.
(iii) Msamaha wa kuchangia gharama za huduma za
afya kwa watoto, akina mama wajawazito, wasiojiweza pamoja na wagonjwa sugu
ulitolewa na unaendelea kuwafaidia wahusika.
(b) Kuanzishwa na kuendelea kuimarika kwa Mfuko
wa Taifa wa Bima ya Afya. Sera hiyo
imewawezesha watumishi wa sekta ya umma kukabiliana na gharama za tiba kwa
manufaa yao na wategemezi wao na imeendelea kupatikana kwa ubora stahiki. Hadi kufikia Aprili, 2004 idadi ya wanachama
imeongezeka kwa asilimia 44 kufikia 242,508, kulinganisha na 167,989 mwaka
2003.
(c) Kuendelea kutolewa kwa huduma za chanjo kwa
watoto kwa viwango vya kuridhisha na kufikia asilimia 90 kwa mwaka
2003/2004. Kiwango hicho ni zaidi ya
kile kinachokubalika kimataifa. Kuhusu
ugonjwa wa Polio, mafanikio makubwa yamepatikana ambapo Shirika la Afya Duniani
(WHO) limeiweka nchi yetu katika kundi la nchi zinazotazamiwa kutangazwa kuwa
hazina ugonjwa huo.
(d) Hospitali zimeongezeka kutoka 203 mwaka 2000
hadi 220 mwaka 2005. Vituo vya afya
vimeongezeka kutoka 367 mwaka 2000 hadi 395 mwaka 2005. Limekuwepo pia ongezeko kubwa katika ujenzi
wa zahanati kutoka 3,984 mwaka 2000 hadi 4408 mwaka 2005, likiwa ni ongezeko la
asilimia Zahanati 424 sawa na asilimia 10.6.
(e) Ukarabati mkubwa wa hospitali na majengo
mengine ya tiba kuanzia Hospitali ya Taifa Muhimbili mpaka hospitali za wilaya
umekamilika au uko katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Jumla ya majengo 475, vituo vya afya 60,
hospitali 84 na vyuo vya afya 43 yalifanyiwa ukarabati huo. Mashine za “X-ray” na “Ultrasound” na
jenereta zimefungwa katika hospitali za wilaya, mikoa na rufaa. Jumla ya Hospitali 98 za Serikali zikiwemo 70 za Wilaya, 20 za Mikoa, 4 maalum na 4 za rufaa zimehusika.
(f) Tanzania ipo mstari wa mbele duniani katika
vita dhidi ya malaria. Katika bajeti ya
2004/2005 Serikali ilifuta kodi kwenye vyandarua na bidhaa zinazosaidia vita
dhidi ya malaria pamoja na kuanzisha mpango wa hati punguzo. Hali hiyo imesaidia sana kupunguza
maambukizo ya malaria hasa kwa kina mama wajawazito na watoto wachanga. Uhamasishaji wa jamii kutumia vyandarua
vyenye viuatilifu umeendelea. Aidha,
utekelezaji wa majukumu ya kutoa mafunzo kwa wataalamu mbali mbali wa afya
katika kukabiliana na malaria; kutoa tiba sahihi na tiba ya tahadhari kwa
wajawazito, utafiti; udhibiti wa milipuko ya malaria katika maeneo husika na
katika ngazi ya jamii, vinaendelea kwa nguvu.
(g) Huduma za Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto
katika miaka mitano iliyopita ziliendelea kutolewa zikiwa na mwelekeo wa
kuongeza wingi na ubora wake. Miongoni
mwa mafanikio mbalimbali yaliyopatikana, ni kuendelea kutolewa bila malipo kwa
huduma kwa wanawake wakati wa ujauzito, kujifungua na baada ya kujifungua. Utaratibu huu umekuwa na mvuto mkubwa nchini kote.
55. Serikali kupitia Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI imeendelea kutoa kipaumbele katika maeneo mbalimbali husika ikiwa na lengo la kudhibiti maambukizi mapya ya UKIMWI na kutoa huduma kwa waathirika na kupata mafanikio ambayo baadhi yake ni yafuatayo:-
(a) Katika
kuhakikisha upatikanaji wa damu salama, Serikali ilinunua na kusambaza vipimo
vya damu dhidi ya maambukizo ya UKIMWI (HIV Test Kits) 1,100,000 katika
hospitali zitoazo damu kwa wagonjwa nchini.
Hatua hiyo ilinusuru watu zaidi ya 120,000 kupata damu yenye virusi na
kuambukizwa na UKIMWI.
(b) Vituo 400 kote nchini vinatoa huduma za Ushauri Nasaha vikiwemo na visivyo vya kiserikali.
(c) Dawa za kurefusha maisha kwa waathirika wa UKIMWI (ARV) zilinunuliwa kati ya mwezi Oktoba 2004 na mwaka 2005, na zilitolewa kwa waathirika 44,000.
Maji
56.
Hatua nyingi zilizochukuliwa katika kipindi cha 2000 – 2005 zililenga
katika utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Maji ya 2002 iliyotolewa baada ya
kuifanyia mapitio ile ya 1991. Sera
imeweka msisitizo katika ushirikishwaji wa wanachi katika kupanga, kujenga,
kuendesha na kumiliki miradi ya maji mijini na vijijini. Mafanikio yake yamedhihirika katika maeneo
yafuatayo:-
(a) Serikali imeweka na kuboresha mtandao wa kuchunguza na kukusanya takwimu za maji yaliyopo juu na chini ya ardhi katika kuhakikisha rasilmali maji inapatikana kwa ubora na wingi unaotakiwa kwa ajili ya matumizi ya kijamii na kiuchumi. Kati ya mwaka 2000 hadi 2004, Serikali iliendelea kuboresha mtandao huo kwa kuimarisha vituo 176 kwa ajili ya kukusanya takwimu kuhusu maji juu ya ardhi na vituo 3 kwa maji chini ya ardhi.
(b) Kati ya mwezi Novemba 2000 hadi Disemba 2004
Serikali ilifanya utafiti katika maeneo mbalimbali nchini ili kutambua maeneo
yanayofaa kuchimba visima vya maji kwa matumizi mbalimbali. Zoezi hilo limeongeza maeneo ya kuchimba
visima virefu na vifupi vya maji kutoka maeneo 497 mwaka 2000 hadi kufikia
maeneo 1033 mwaka 2004. Jumla ya maeneo
3082 yalipatikana kwa ajili ya kuchimba visima virefu na vifupi.
(c) Kwa kutambua kwamba asilimia 43.4 ya
rasilimali za maji katika nchi yetu zipo katika mabonde tunayoshirikiana na
nchi nyingine, Serikali kati ya mwaka 2000 hadi 2004 ilifanya majadiliano na
nchi husika ili kuweka utaratibu shirikishi na endelevu wa kusimamia matumizi
na kutunza rasilmali maji chini ya Vyombo na Taasisi mbali mbali kama
ifuatavyo:-
(i) Kamati za Usimamizi na Uongozi za Mto Songwe.
(ii) Kamati ya Majadiliano ya Bonde la Mto Nile (Nile
Basin Initiative).
(iii) Marekebisho ya Itifaki Juu ya Rasilimali za
Maji Shirikishi katika nchi za SADC.
(iv) Mkataba wa Makubaliano wa nchi za Tanzania,
Msumbiji na Malawi.
(v) Makubaliano ya Kuanzisha Kamisheni ya Bonde
la Mto Zambezi.
(vi) Itifaki ya
Maendeleo Endelevu ya Bonde la Ziwa Victoria.
(d) Katika kipindi cha mwaka 2000 hadi 2004
Serikali iliendelea kuimarisha mfumo wa kusimamia rasilimali ya maji katika
mabonde 9 (Mto Pangani, Mto Rufiji, Ziwa Victoria, Mto Wami/Ruvu, Ziwa Nyasa,
Ziwa Rukwa, Ziwa Tanganyika, Bonde la Kati la Ziwa Eyasi, Bububu na Manyara, na
Mto Ruvuma). Hadi kufikia Juni 2004,
zilikwishafunguliwa Ofisi za Maji na Bodi za Maji za Mabonde yote 9 tofauti na
awali zilipokuwa ofisi 2 tu.
(e) Kumekuwepo na utaratibu na ufuatiliaji wa
ubora na usafi wa maji ili kulinda afya za wananchi. Mwaka 2000 sampuli za maji 13344 zilipimwa na Maabara Kuu na
kuongezeka hadi kufikia sampuli 20707 mwaka 2004.
(f) Kufuatia jitihada za ukarabati wa mifumo ya
maji ya miji mikuu ya mikoa, upanuzi wa mifumo iliyopo, utafutaji wa vyanzo
vipya na uimarishaji wa uwezo wa uendeshaji wa Mamlaka husika, kiwango cha
upatikanaji wa maji kwa wakazi wa mijini kimeongezeka kutoka asilimia 63.1
mwaka 2000 hadi asilimia 74 mwaka 2004.
(g) Idadi ya wananchi vijijini wanaopata huduma
ya maji safi na salama karibu na makazi yao imeongezeka kutoka asilimia 50
mwaka 2000 hadi asilimia 53.5 mwaka
2004.
(h) Hadi kufikia Desemba 2004, Kamati za Maji
8725 zilianzishwa ikilinganishwa na 6,086 zilizokuwepo mwaka 2000, likiwa ni
ongezeko la asilimia 43.4.
(i) Mifuko ya maji vijijini iliongezeka kutoka 5,384 mwaka 2000 yenye thamani ya Sh. 765,700,890 hadi kufikia 7,254 yenye thamani ya Sh. 1,275,765,842/= mwaka 2004.
(j) Mamlaka nane za maji mijini katika miji ya
Arusha, Tanga, Moshi, Mwanza, Morogoro, Mbeya, Tabora na Dodoma hivi sasa
zinajitegemea katika gharama zote za uendeshaji zikiwemo za umeme, mishahara na
madawa ya kusafishia maji.
(k) Uwekezaji kwenye miradi ya maji mijini na vijijini umeongezeka. Hadi sasa imetekelezwa miradi yenye thamani
ya Sh. 20.4 bilioni katika mikoa ya Morogoro, Dodoma, Tabora, Arusha, Moshi na
Tanga. Vivyo hivyo, kwa upande wa
uondoaji majitaka, miradi ya thamani ya Sh. 11.4 bilioni katika mikoa ya
Morogoro, Tabora, Mwanza, Iringa, Arusha, Moshi na Mwanza imekamilika.
(l) Ujenzi wa mradi mkubwa wa maji kwa fedha za Serikali yetu kwa ajili ya wananchi wa miji ya Shinyanga na Kahama kupitia vijiji kadhaa umeanza mwezi Mei 2004. Awamu ya kwanza imepangwa kukamilika mwishoni mwa 2005.
(m) Ukodishaji wa huduma za maji safi na maji
taka jijini Dar es Salaam umekamilika.
Ukodishaji huu umewezesha kupata mkopo wa 164.6 bilioni zitakazotumika
kuboresha huduma za maji jijini pamoja na maeneo ya Kibaha na Bagamoyo. Kazi ya ukarabati wa miundombinu ya maji
imeanza. Kwa hatua hii matatizo ya maji
yatapungua kama sio kutoweka kabisa.
Kutokana na mapato yatakayoongezeka katika kuboresha huduma ya maji,
mradi hautategemea tena fedha kutoka Serikalini.
Ardhi na
Maendeleo ya Makazi
57. Makazi yaliyopangwa yanasaidia kuhakikisha
kwamba kunakuwa na matumizi bora na endelevu ya rasilimali za ardhi. Aidha, makazi yaliyopangwa na yenye
miundombinu na huduma muhimu yanachangia katika kuongeza tija na kuendeleza
uchumi wa watu wanaoishi katika maeneo hayo na hatimaye kupunguza umaskini.
58. Maendeleo ya makazi yamepata mafanikio yafuatayo katika
kipindi cha 2000 – 2005:-
(a) Kutokana na uhaba wa viwanja katika miji
nchini, mwaka 2002/2003 Serikali ilibuni na kutekeleza Mradi wa Kupima Viwanja
20,000 katika Jiji la Dar es Salaam.
(b) Upimaji wa mipaka ya vijiji 2,048 umefanyika
katika mikoa 8 kwa kutumia vifaa vya kisasa vya “Global Positioning System”. Mikoa hiyo ni Arusha, Kilimanjaro, Manyara,
Mbeya, Morogoro, Ruvuma, Shinyanga na Singida.
(c) Jumla ya vikundi 22 vya ujenzi na uzalishaji
wa vifaa vya ujenzi wa gharama nafuu vimeanzishwa katika mikoa ya Tanga,
Morogoro, Kilimanjaro, Pwani, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Kagera, Singida,
Manyara, Arusha na Mara. Vikundi hivyo
vinaendesha shughuli za ujenzi wa nyumba bora za gharama nafuu kwa kutumia
teknolojia rahisi na sahihi.
(d) Halmashauri 25 zimepatiwa mikopo ya jumla ya
shilingi 310,128,665 kwa
ajili ya kupima viwanja.
(e) Shirika la Nyumba la Taifa limezifanyia
matengenezo nyumba zake 15,875 nchini kote.
(f) Shirika la Nyumba la Taifa limejenga nyumba
za makazi na biashara 264 nchini kote zenye thamani ya shilingi bilioni 47.84.
Shirika la Nyumba la Taifa limeuza nyumba ndogo ndogo na za kati 4,268. Nyumba 660 zinaendelea kulipiwa na wateja
kwa awamu.
(g) Hadi Juni, 2004 watumishi 502 ambao ni sawa
na asilimia 30.6 ya waombaji wote wameidhinishiwa mikopo na Bodi ya Mfuko wa
Mikopo yenye jumla ya Shilingi 1.6 bilioni.
(h) Mpango wa kutambua ardhi katika maeneo ya
makazi yasiyopangwa Jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuwapatia wenye nyumba
leseni za makazi, uliendelea kutekelezwa.
Utangulizi:
59. Historia ya
uchaguzi kwa Zanzibar ndani ya mfumo wa vyama vingi vya siasa inatoa taswira
kwa vyama vya upinzani kutokubali matokeo yake pale vinaposhindwa, na hivyo
kuitia nchi katika vurugu, fujo na uvunjifu wa amani. Matokeo ya uchaguzi wa mwaka 1995 na yale ya mwaka 2000
yanadhihirisha kutokomaa kwa vyama vilivyoanzishwa baada ya kuanza kwa mfumo wa
vyama vingi kwani bado siasa za chuki, fujo na vurugu ndio mtaji wao wa kisiasa na kutafuta huruma ya jumuiya ya
Kimataifa.
60. Kama
ilivyotokea baada ya Uchaguzi Mkuu wa 1995 vyama vilivyoshindwa katika Uchaguzi
Mkuu wa 2000, viliyakataa tena matokeo na
kuendeleza tabia ya vurugu, fujo na kuifikisha nchi katika hali mbaya ya
kuitia doa kwa matukio ya tarehe 26 na 27 Januari, 2001. Hata hivyo, baada ya matukio hayo, CCM
kikiwa Chama tawala na kama ambavyo kilifanya baada ya vurugu na fujo zilizofuatia
matokeo ya Uchaguzi wa mwaka 1995, kiliwajibika kutoa uongozi kwa kuiondoa nchi
katika hali hiyo na kuirejesha katika amani na mshikamano. Wajibu huu wa CCM kujitokeza na kutoa
uongozi katika mazingira ya fadhaa kimsingi ni utekelezaji wa Mwelekeo wa Sera
za CCM katika miaka ya 2000 hadi 2010, kama ilivyoainishwa katika Ibara ya 114
(b)(kama ilivyo sasa).
61. Ni kutokana na mazingatio hayo, haja ya mazungumzo ilijitokeza na Mwenyekiti wa CCM Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Benjamin W. Mkapa, aliitisha mazungumzo hayo, ambayo hatimae yaliwawezesha Viongozi Wakuu wa CCM na CUF kutiliana saini makubaliano ya Muafaka hapo tarehe 10 Oktoba 2001, na kuwawezesha Wazanzibari kuendelea kuishi kwa umoja, amani na utulivu.
62. Aidha, kutokana na utekelezaji wa Sera sahihi za CCM, heshima ya Zanzibar na Tanzania kwa jumla ilirejea na kutoa nafasi nzuri zaidi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na CCM kwa pamoja kuendeleza harakati za kuimarisha uchumi wa Taifa kwa kutekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo na kupunguza kasi ya umaskini.
Utekelezaji
wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa 2000 - 2005
63. Mbali na misukosuko ya kisiasa iliyosababishwa na matukio ya tarehe 26 – 27 Januari 2001, hujuma za kigaidi za tarehe 11 Septemba 2001 nchini Marekani, vita vya Irak pamoja na magendo ya karafuu yaliyoendeshwa na wapinzani, utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2000, kwa upande wa Zanzibar, umefanikiwa sana. Mafanikio hayo yanajidhihirisha katika maeneo makuu yafuatayo:-
Kuimarisha
Uchumi:
64. Katika kuimarisha uchumi wa Zanzibar, mafanikio yafuatayo
yamepatikana:
Kuimarisha
utendaji na ukusanyaji wa Mapato ya Serikali
(a) Sheria za Kodi na Makampuni zimefanyiwa mapitio ya kina na kurekebishwa. Miongoni mwa Sheria hizo ni Sheria ya VAT, Hotel Levy, Stamp Duty, Mafuta, Ada ya Bandari na Ada ya Uwanja wa Ndege.
(b) Udhibiti wa mapato na matumizi ya fedha na mali za Serikali umeimarishwa. SMZ imefungua hesabu zake katika Benki Kuu ya Tanzania (BOT) na mfumo wa “Central Payroll System” na MTEF umeanzishwa na mafunzo kwa watendaji na elimu kwa walipa kodi imeendelea kutolewa.
(c) Mfumo wa utendaji wa serikali, madaraka ya watendaji na uwajibikaji umefanyiwa tathmini na programu za mageuzi ya fedha na uchumi, utawala bora na mageuzi ya kitaasisi na watendakazi zimeanza kutekelezwa.
Kuendeleza ujenzi wa Misingi Mipya ya Uchumi
(d) Sera mpya ya
Uwekezaji yenye vivutio vingi zaidi imeanzishwa na Sheria ya Kulinda na
Kuhifadhi Vitega Uchumi na kuundwa kwa Mamlaka moja ya Uwekezaji imepitishwa.
(e) Jumla ya miradi mipya 67 yenye mtaji wa thamani
wa (U$ 117,326,310) imeidhinishwa na miradi mingine minane yenye thamani ya (U$
69.42) milioni imewekezwa na kuanza kutoa huduma katika Mamlaka ya Maeneo huru
ya Kiuchumi.
(f) Katika Mamlaka
ya Bandari Huru, jumla ya miradi tisa imeanzishwa na kutoa fursa ya ajira kwa
wafanyakazi wazalendo 3210. Aidha, Serikali imeingia mkataba na Kampuni
binafsi wa kuliendeleza eneo huru la Fumba litakalojulikana kama “Zanzibar
World Zone”.
(g) Ili kuwavutia
wawekezaji, eneo lote la Micheweni limepimwa lna kuwekwa mipaka. Aidha, kazi ya ujenzi wa njia ya umeme hadi
Nyamanzi pamoja na ofisi mbili katika eneo la Fumba, imekamilishwa.
Uimarishaji
wa Taasisi na Mashirika ya Serikali.
(h) Sheria ya Mitaji ya Umma ya mwaka 2002,
imepitishwa ili kuyawezesha mashirika
ya Serikali kujiendesha kibiashara.
(i) Miradi ya ujenzi wa majengo ya vitega uchumi vya Mashirika yafuatayo, imekamilika na kuanza kutoa
huduma za kibiashara:-
(i) Jengo la Kitega – Uchumi la Shirika la
Biashara
la Taifa (ZSTC) Kinazini – Unguja.
(ii) Majengo
ya Afisi za Mfuko wa Hifadhi ya Jamii
(ZSSF) Kilimani – Unguja na Tibirinzi –
Pemba.
(iii) Jengo
la Bandari huru – Maruhubi.
(j) Shirika la Uvuvi
na Shamba la Mipira, yamefanyiwa tathmini na kukodishwa pia Kiwanda cha Maziwa
kimefanyiwa tathmini na kuuzwa kwa
mwekezaji wa ndani.
65. Kutokana na
mafanikio hayo ya utekelezaji wa sera za CCM na mageuzi ya kiuchumi, manufaa yafuatayo
yameweza kupatikana:-
(a) Kiwango cha
mapato ya Serikali kimeongezeka kutoka T.Shs. 46.7 bilioni mwaka 2000, hadi T.Shs. 51 bilioni mwaka
2004.
(b) Kiwango cha
ukuaji wa uchumi kimeongezeka kutoka asilimia 4.2 mwaka 2000 hadi asilimia 6.5
mwaka 2004.
(c) Kiwango cha mfumko wa bei kimeendelea kuwa
chini ya wastani wa asilimia 10.
66. Kwa upande wa sekta ya Uchumi, mafanikio
yafuatayo
yamepatikana:-
Kilimo
(a) Vituo vya
Utafiti wa Kilimo cha Kizimbani – Unguja na Matangatuani Pemba,
vimeimarishwa. Aidha, Sheria ya
uanzishaji wa Chuo cha Kilimo – Kizimbani, imepitishwa.
(b)
Wakulima wadogo wadogo 160 na vikundi 52 vya
wanawake, wamepatiwa mafunzo na mbinu za kilimo bora, matumizi ya mbolea za
kimaumbile na kilimo mchanganyiko.
(c)
Wafanyakazi 122 wamepatiwa mafunzo ya muda mrefu na
muda mfupi ndani na nje ya nchi. Tafiti
mbali mbali zimefanywa ili kuendeleza
uzalishaji wa mbegu bora za mazao ya
chakula na biashara. Wastani wa miche 300,000 ya mikarafuu imeoteshwa na kusambazwa
kwa wakulima kila mwaka.
(d)
Mpango Mkuu wa Kilimo cha Umwagiliaji maji (Zanzibar
Irrigation Master Plan), umeandaliwa na kukamilishwa. Jumla ya hekta 8,000
zimeonekana kufaa kwa kilimo hicho.
Mifugo
(e) Huduma za kinga na tiba kwa mifugo, zimeendelezwa. Jumla ya ng’ombe 23,520 walipatiwa chanjo
dhidi ya maradhi ya vibuma, mbavu, miguu na midomo na mbwa 2,655 walipatiwa
chanjo dhidi ya maradhi ya kichaa cha mbwa.
(f) Ili
kuwaendeleza wafugaji, Jumuiya ya Wafugaji wa Ng’ombe wa Maziwa na Jumuiya ya
Wafugaji wa Kuku zimeanzishwa. Wafugaji
wadogo wadogo 242, wamepatiwa mafunzo na taaluma za ufugaji bora na wananchi
310 wamepatiwa ng’ombe wa maziwa baada ya kupatiwa mafunzo ya utunzaji wa
ng’ombe hao chini ya mpango wa “kopa ng’ombe lipa ng’ombe”.
(g) Kiwanda cha
Maziwa cha Maruhubi baada ya kubinafsishwa, kimefufuliwa na kuanza kazi ya
usindikaji wa maziwa na mtindi. Hatua
hii imetoa fursa nzuri ya soko la maziwa kwa wafugaji.
Uvuvi
(h) Wavuvi wadogo
wadogo katika vijiji 19 Unguja na Pemba, wamepatiwa mafunzo na mikopo ya vifaa
na zana za uvuvi. Wananchi wa vijiji
viliyopo chini ya Mradi wa Menai wamepatiwa mafunzo na msaada wenye thamani ya T.Shs. 12.4 Milioni ili kuendeleza
miradi yao ya kijamii na kiuchumi.
(i) Utafiti wa zao
la mwani aina ya “Cottonii”, umefanyika na wakulima kupatiwa mafunzo na
mbinu bora za uzalishaji.
(j)
Ujenzi wa soko jipya la samaki la
Malindi, umekamilika.
Aidha,
kuimarika kwa Sekta ya Utalii, kumepanua sana soko la mazao ya baharini hasa samaki, pweza, kamba n.k.
Mazingira
(k) Wananchi
wamehamasishwa na kuelimishwa juu ya athari za uchafuzi wa mazingira. Jumuiya na vikundi 14 vya kijamii vimeanzishwa ili kusimamia hifadhi na
utunzaji wa mazingira katika maeneo
yao. Siku ya Mazingira Duniani (tarehe 1 – 5 Juni) imeadhimishwa kila mwaka.
(l) Ukaguzi wa mara
kwa mara katika viwanda umefanywa na miongozo ya kufuatwa na wenye viwanda ili
kuhifadhi mazingira imetolewa.
(m) Utunzaji wa
misitu ya asili na maeneo maalum ya baharini umeimarishwa. Jumla ya miti 56,200 imepandwa katika maeneo
mbali mbali mijini na vijijini na Hifadhi ya Taifa ya Msitu wa Jozani
imeanzishwa.
Utalii
(n) Mpango Mkuu wa
Kuendeleza Shughuli za Utalii (Tourism Master Plan) umeandaliwa. Kikosi
cha Ulinzi wa Watalii (Tourism Patrol) kimeanzishwa. Chuo cha Hoteli cha
Maruhubi kimeimarishwa kwa kupatiwa vifaa vya kisasa na wataalamu.
(o) Hatua ya
kuitangaza Zanzibar katika maonyesho mbali mbali ya Kimataifa ili kupanua wigo
wa masoko mapya imetekelezwa.
(p) Ili kuwavutia
watalii wa daraja la kwanza, ujenzi wa hoteli kubwa za kisasa
umeendelezwa. Miradi ya ujenzi wa Renco
Hotel Ltd, Zamani International na Ocean Beach Resort, imeanzishwa huko Nungwi
na Kiwengwa.
Viwanda
(q) Rasimu ya
Sera na Mpango wa Viwanda Vidogo Vidogo na vya Kati, imekamilishwa. Viwanda vipya vitatu (Zanzibar Kool, Kiwanda
cha Kokoto na Kiwanda cha Chokaa) vimeanzishwa chini ya sekta binafsi na kutoa
fursa ya ajira kwa wananchi.
(r) Vikundi 45 vya
wanawake, vimepatiwa mafunzo na ujuzi wa kusindika vyakula vya matunda. Aidha, mfuko maalum wa kuwaendeleza
wazalishaji wadogo wadogo umeanzishwa na maeneo ya Saateni na Maruhubi
yametengwa kwa shughuli za uzalishaji na maonyesho ya kibiashara.
(s) Kiwanda cha
ushoni cha Vikosi vya SMZ kimeanzishwa.
Biashara
(t) Sera mpya ya
Biashara imeandaliwa na Jumuiya ya Wafanya biashara, Wenye Viwanda na Wakulima
imeundwa upya. Aidha, mazungumzo na
nchi mbali mbali duniani yameendelezwa ili kukuza ushirikiano na kupanua soko
la biashara.
(u) Sheria ya Mizani na Vipimo imefanyiwa
mapitio na
kurekebishwa. Vikwazo katika uendeshaji wa biashara
vimeondoshwa na wafanyabiashara wa ndani wamehamasishwa kuuza bidhaa zaidi nje
ya nchi. Bidhaa zisizo za asili zimezalishwa na kusafirishwa nje ya nchi.
Ardhi
(v) Ardhi
imeendelea kuwa ni mali ya Serikali.
Sheria ya umilikaji ardhi ambayo inaruhusu ardhi kutumika kama dhamana
na kuwawezesha wananchi kupata mikopo kutoka katika vyombo vya fedha,
imepitishwa.
(w) Jumla ya viwanja
4,234 vimepimwa na kugawiwa kwa wananchi kwa ajili ya makaazi, vitega uchumi,
kilimo na biashara. Mbinu za udhibiti
na ukusanyaji wa mapato na kodi za viwanja
zimeimarishwa.
Ushirika
(x) Kwa
kushirikiana na Shirika la ILO, programu maalum ya Uimarishaji wa Sekta ya
Ushirika imeanzishwa na Sheria ya Vyama vya Ushirika imefanyiwa mapitio na
kurekebishwa.
(y) Kazi ya ukaguzi
wa vyama vya ushirika na utoaji wa mafunzo, imeendelezwa. Jumla ya vyama vya
ushirika 43 vimeanzishwa na kusajiliwa rasmi.
67. Katika sekta ya Miundombinu ya Kiuchumi,
mafanikio yafuatayo yamepatikana:-
Barabara
(a) Jumla ya km 120.55 za barabara, zimejengwa kwa
kiwango cha lami na kukamilika, kama
ifuatavyo:-
·
Makunduchi
– Mtende km 5.5
(Barabara kuu)
·
Kitogani
– Paje km 11.2 (Barabara ya Vijijini)
·
Kaebona
– Kaepwani km 4.5
(Barabara ya Vijijini)
·
Bambi
– Njia nne km 6
(Barabara ya Vijijini)
·
Amani
– Welezo km 0.75
(Barabara ya Mjini)
·
Mazizizini –
Chukwani km 7
(Barabara ya Mjini)
·
Kidimni
_ Kitope/Kitundu, Ndagaa na
Machui
Ring roads
29.6 (Barabara ya
Vijijini)
Ø
Pemba
·
Chake
– Vitongoji km 7 (Barabara Kuu)
·
Chake
– Wesha km 7 (Barabara kuu)
·
Kilindini
– Micheweni km 6
(Barabara ya Kijijini)
·
Mkoani
– Chake km 36 (Barabara kuu)
(b) Jumla ya km 32.2
za barabara zimeanza kujengwa na kazi bado
inaendelea. Barabara hizo ni:-
Ø
Unguja
·
Jang’ombe
- Mpendae km 1.2
(Barabara ya Mjini)
·
Amani
– Mtoni km 4 (Barabara ya Mjini)
·
Mahonda
– Donge/Mkokotoni km 14
(Barabara ya Vijijini)
Ø Pemba
·
Mtuhaliwa
- Chokocho km 13
(Barabara ya Vijijini)
(c) Sheria ya
kusimamia matumizi ya barabara na vyombo vya moto, imerekebishwa. Huduma ya usafiri hasa Mjini na Ukaguzi wa
magari umeimarishwa.
Huduma
za Posta na Simu
(d) Shirika la Posta Tanzania,
limeendelea na juhudi zake za kuimarisha huduma za usafirishaji wa barua,
vifurushi, fedha na mawasiliano ya internet kati ya Zanzibar na nchi nyingine duniani.
(e)
Kampuni ya Simu Tanzania
(TCCL) kwa kushirikiana na makampuni mengine binafsi ya simu za mikononi
(ZANTEL, MOBITEL, VODACOM na CELTEL) imeendelea kuimarisha huduma za simu kwa
wananchi mjini na vijijini. Aidha,
idadi ya watumiaji wa simu imeongezeka kutoka asilimia 8 mwaka 2000 hadi
asilimia 15 mwaka 2004, na kufanya Zanzibar kufikia nafasi ya kwanza Barani
Afrika kwa watumiaji wa simu.
Bandari
(f) Kazi ya
upembuzi yakinifu na utayarishaji wa zabuni ya matengenezo ya bandari ya
Malindi, ujenzi wa chelezo cha
Malindi na ujenzi wa barabara itokayo
chelezoni hapo hadi bandarini zimekamilika.
(g) Gati ya Wete
imefanyiwa matengenezo na kuanza kutoa huduma kwa majahazi na meli za aina ya landing craft”. Minara yote ya kuongozea meli imefanyiwa
matengenezo na kuwekewa taa zenye kutumia nguvu za jua “solar – power”. Maboya
mapya 18, boti ya kuongozea meli na tishali vimenunuliwa.
Usafiri
wa Majini
(h) Shirika la
Meli limeweza kujiimarisha kwa kuzifanyia
matengenezo
makubwa meli zake zote (m.v Mapinduzi, m.v. Maendeleo na m.v. Ukombozi) na
hivyo kujiweka katika nafasi nzuri ya kuingia ubia na wawekezaji binafsi.
(i) Makampuni binafsi ya Azam Marine, Sea Star
Service, Afrika Shipping, Sea Express, Mkunazini Shipping Enterprise na Panda
II Enterprise yameendelea kuwekeza na kuongeza idadi ya boti za abiria na meli
za mizigo.
Usafiri
wa Anga
(j) Utayarishaji
wa Mpango Mkuu wa Uendelezaji wa kiwanja cha ndege cha Unguja, umekamilika. Aidha, kazi ya utanuzi wa njia ya kurukia
ndege imeanza kutekelezwa.
(k) Wafanyakazi wa
viwanja vya ndege wamepatiwa mafunzo na vifaa vya kisasa vya ukaguzi wa abiria
na mizigo. Majengo ya abiria na kumbi za wageni mashuhuri (VIP) yamefanyiwa
matengenezo. Aidha, njia ya kurukia
ndege katika Uwanja wa Karume – Pemba, imejengwa upya.
Umeme
(l) Kazi ya
usambazaji umeme katika Vijiji (88) imekamilika, kati yake (57) vya Unguja na
(31) vya Pemba. Kituo cha usambazaji
umeme cha Mpendae – Unguja na vinu vyote (3) vya umeme Kisiwani – Pemba,
vimefanyiwa matengenezo makubwa. Hatua
hii imewezesha asilimia 80 ya vijiji vya Zanzibar, kuwa na huduma ya
umeme. Aidha, asilimia 53 ya makaazi
(House hold) na asilimia 55 ya wananchi wote wa vijijini kufikishiwa huduma ya
umeme.
(m) Jumla ya “transforma” 30 zilizokuwa na uwezo mdogo au
kuharibika, zimebadilishwa na njia mpya ya umeme mkubwa (HT) yenye urefu wa Km
10,452 na Km 7,133 za umeme mdogo (LV) zimejengwa Unguja na Pemba.
(n) Vituo vipya 39 vya kusambazia umeme vimejengwa
Unguja na Pemba na mita 13,500 za umeme wa TUKUZA zimesambazwa katika maeneo
mbali mbali ya Mji wa Zanzibar.
(o) Mbinu za
udhibiti na ukusanyaji wa mapato zimeimarishwa na mauzo ya umeme yameongezeka
kwa kiwango cha asilimia 80. Aidha,
utafiti wenye lengo la kufahamu bei muafaka ya kuuzia umeme ili kuwavutia
wawekezaji na kupunguza umaskini umefanywa.
Huduma za
Jamii
68. Katika sekta ya Huduma za Jamii, mafanikio
yafuatayo
yamepatikana:-
Elimu
(a) Kiwango cha
uandikishaji wa watoto waliofikia umri wa kuanza elimu ya msingi (darasa la
kwanza) kimeongezeka kutoka asilimia 94.6 mwaka 2000 hadi asilimia 100 mwaka
2004. Mafanikio haya yameiwezesha
Zanzibar, kuvuka kiwango cha malengo ya milenia ya kimataifa kabla ya mwaka
2015.
(b) Madarasa 133
yalifanyiwa matengenezo na mengine mapya 783 yamejengwa. Madawati 15,833 na meza 2,657 zimenunuliwa
na kusambazwa katika skuli mbali mbali.
(c) Idadi ya
skuli za Serikali na binafsi zimeongezeka kutoka 331 mwaka 2000 hadi 465 mwaka
2004. Jumla ya skuli 66 za maandalizi
zimefunguliwa, mbili za Serikali na 64 za binafsi. Skuli za msingi 28 zimefunguliwa, 21 za Serikali na 7 za binafsi. Aidha, Skuli 20 za msingi na kati
zimefunguliwa, 16 za Serikali na 4 za binafsi.
Kwa upande wa sekondari, skuli 23 zimefunguliwa, zikiwemo 20 za Serikali
na 3 za binafsi. Aidha, ujenzi wa
skuli ya Sekondari ya Mchepuo wa Biashara – Tomondo, umekamilika na kuanza
kutoa huduma.
(d) Idadi ya vijana waliofaulu kujiunga na Kidato
cha Tatu imeongezeka kutoka asilimia 31.6 mwaka 2000 hadi asilimia 43.1 mwaka 2004. Kidato cha nne asilimia 77.3 mwaka 2000 hadi asilimia 92.3 mwaka
2003. Kidato cha tano, kutoka wanafunzi 305 mwaka 2000 hadi 2,076
mwaka 2004.
(e) Kituo cha Taifa cha Walimu kimeanzishwa na
vituo tisa vya Kanda vimejengwa katika kila Wilaya. Chuo cha Ualimu cha Nkurumah kimefanyiwa matengenezo makubwa na
Chuo cha Ualimu Wete – Pemba, kimeanzishwa.
Idadi ya Vijana wanaojiunga na mafunzo ya ualimu, imeongezeka kutoka 962
mwaka 2000 hadi 2653 mwaka 2004. Aidha,
mafunzo ya Diploma ya Elimu ya Msingi yameanzishwa.
(f) Skuli za Ufundi za Mikunguni na Kengeja
zimeimarishwa na kupatiwa vifaa. Chuo
cha Ufundi cha Karume, kimepatiwa
maabara na vifaa vya kisasa na kuwa kituo cha Mafunzo kwa jamii na
mawasiliano ya moja kwa moja (Video
Conferencing).
(g) Chuo Kikuu cha
Taifa (SUZA) kimeanzishwa, na kufanya idadi ya vyuo vikuu vya Zanzibar kufikia
vitatu. Chuo kimeanza kufundisha masomo
ya Ualimu wa Sanaa, Lugha, na Sayansi ili
kuwaandaa walimu wa skuli za sekondari.
Elimu
ya Watu Wazima
(h) Kiwango cha idadi ya watu wanaojua kusoma,
kuandika na kuhesabu kimeongezeka kutoka asilimia 60 mwaka 2000 hadi asilimia
73.4 mwaka 2004. Idadi ya madarasa ya
kisomo cha elimu ya watu wazima imeongezeka kutoka 329 mwaka 2000 hadi 446 na
ile ya wanakisomo imeongezeka kutoka 5114 hadi 8,007 katika kipindi hicho.
(i) Idadi ya vituo vya elimu ya amali,
imeongezeka kutoka 39, mwaka 2000 hadi 72
mwaka 2004. Aidha, idadi ya
vituo vya kujiendeleza (Qualifying
test) vimeongezeka kutoka 21 na wanafunzi 2,298 mwaka 2000 hadi 42 na wanafunzi
4,938 mwaka 2004.
Utamaduni
na Michezo
(j) Rasimu za Sera za Utamaduni na Michezo
zimekamilika. Sheria za Uundaji wa
Baraza la Sanaa, Baraza la Kiswahili la Zanzibar na Mfuko wa Kutunza Kumbukumbu
za Historia ya Zanzibar, zimepitishwa. Aidha, Bodi ya Sensa ya Filamu na Sanaa za Maonyesho imeundwa upya na Umoja
wa Waandishi wa Vitabu na Washairi, umeanzishwa. Huduma za makumbusho
zimeimarishwa na Makumbusho Kuu ya kisasa imeanzishwa katika jengo la
Beit-el-Ajab.
(k) Michezo ya
aina mbali mbali imeimarishwa hususan mpira wa miguu ambapo timu ya vijana
walio na umri chini ya miaka 19 ilitwaa ubingwa wa Afrika Mashariki na
Kati mwaka 2003. Chama cha Mpira wa miguu (ZFA) kimefanikiwa
kupata uanachama kamili wa Shirikisho la Mchezo wa Mpira wa Miguu kwa Nchi za
Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) na Shirikisho la Afrika (CAF) na juhudi za
kuwa mwanachama kamili wa FIFA zinaendelea.
Afya
(l)
Elimu ya Afya imeendelea kutolewa na
Wananchi
wameelimishwa
jinsi ya kujikinga na aina mbali mbali ya maradhi ya kuambukiza. Kamati za malaria na maradhi ya kuambukiza
zimeanzishwa katika ngazi za Wilaya na Shehia. Idadi ya vyandarua 31,400 vyenye
dawa vimesambazwa kwa wananchi na matumizi ya vyandarua yameongezeka kutoka
asilimia 3 mwaka 2000 hadi asilimia 20 mwaka 2004.
(m) Huduma za
matibabu kwa wananchi zimeimarishwa na Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja, Hospitali
ya Wagonjwa wa Akili ya Kidongo Chekundu kwa Unguja na Hospitali za Mkoani,
Chake na Wete kwa Pemba zimefanyiwa matengenezo makubwa na kupatiwa vitendea
kazi, madawa na vifaa vya kisasa. Jumla
ya vituo vipya vya afya (12) vimejengwa, vinane kwa Unguja na vinne Pemba,
chini ya Mpango wa Kuwashirikisha Wananchi wenyewe katika maeneo yao.
(n) Huduma za Mama na Mtoto zimeendelezwa na
asilimia 90 ya watoto walio na umri chini ya miaka mitano wamepatiwa huduma za
chanjo. Aidha, watoto 139 wenye
matatizo ya moyo walipelekwa nje ya nchi kwa matibabu zaidi.
(o) Viwango vya
malipo na maslahi ya wafanyakazi wa Sekta ya Afya vimerekebishwa na mpango wa
mafunzo umeendelezwa. Jumla ya
wafanyakazi 92 wamepatiwa mafunzo katika Chuo cha Afya – Mbweni, 288
walipelekwa Tanzania Bara na 30
walipelekwa nje ya nchi.
Vita
dhidi ya Ukimwi
(p) Tume ya UKIMWI
Zanzibar imeanzishwa na rasimu ya Mpango wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na
Malaria imekamilika. Aidha, rasimu ya
Mpango wa Kuimarisha huduma za Maabara
kwa lengo la kupunguza maambukizo ya UKIMWI kutoka kwa Mama na Mtoto
imekamilika.
(q) Kitengo cha kudhibiti UKIMWI (ZACP), Kamisheni
ya UKIMWI (ZAC) pamoja na Asasi mbali mbali zisizokuwa za Serikali (AZISE) zimeendeleza juhudi ya kuelimisha wananchi
jinsi ya kujikinga na UKIMWI. Jumla ya
vituo 12 vya ushauri nasaha na huduma za upimaji wa VVU vimefunguliwa. Huduma za ufuatiliaji wa wagonjwa wa UKIMWI
na kuwapatia tiba zimeanzishwa.
Maji
(r) Hatua za kuwawezesha wananchi kupata huduma ya maji safi na salama mijini na vijijini, imeendelea kutekelezwa.
Jumla ya miradi (75) ya maji vikiwemo visima vipya 18 na matangi mapya 14 ya
kuhifadhia maji yenye ujazo tofauti yamejengwa, kati yake 6 kwa Unguja na 8 kwa
Pemba.
(s) Jumla ya vijiji 95 na wakaazi 495,508
wamepatiwa huduma ya maji safi na
salama, kati yake vijiji 28 na wakazi 124,407 wa Pemba na vijiji 67 yakiwemo
baadhi ya maeneo ya Mji wa Zanzibar na wakaazi 371,104 wa Unguja. Mafanikio haya yamewezesha asilimia 70 ya
wananchi wote wa Zanzibar mijini na vijijini kupatiwa huduma ya maji safi na
salama.
(t) Sera ya Maji ya Taifa, tayari
imekamilika. Aidha, kazi ya usanifu wa
mradi wa maji kwa Mji wa Zanzibar, chini ya msaada wa Japan, imekamilika.
Makaazi
(u) Kazi ya ujenzi wa nyumba bora za kisasa
imeendelezwa kwa kasi kubwa. Jumla ya nyumba
30 za mkopo nafuu katika eneo la Mombasa Unguja, fleti 24 katika nyumba za
maendeleo Michenzani tayari zimekamilika na ujenzi wa fleti 24 nyingine umo
katika hatua za mwisho. Aidha, ujenzi
wa nyumba Nam. 10 Michenzani, ambayo itakuwa na jumla ya fleti 142 pamoja na
maduka unaendelea.
(v) Jumla ya
nyumba 22 zilizomo katika eneo la Mamlaka ya Mji Mkongwe, zimefanyiwa
matengenezo makubwa na majengo mengine 827 yamefanyiwa matengenezo ya kawaida.
(w) Hifadhi ya Mji
Mkongwe wa Zanzibar imeendelezwa na kuingizwa katika orodha wa UNESCO wa urithi
wa Kimataifa. Mji wote wa Zanzibar sasa umekuwa mwanachama wa Jumuiya ya Miji
ya Urithi wa Kimataifa “Organisation of World Heritage Cities” (OWHC).
Vyombo
vya Habari
(x) Studio za TVZ
zimeimarishwa kwa kupatiwa vifaa vya kisasa na kituo cha Mkanjuni – Pemba,
kimepatiwa mtambo mpya wa kurushia
matangazo. Aidha, mpango wa kuunganisha
matangazo ya TVZ na BBC umeanzishwa.
(y) Sauti ya
Tanzania Zanzibar (STZ) imeimarishwa, Studio ya Pemba imepatiwa vifaa vya
kisasa na utaratibu wa kurusha matangazo yake ya moja kwa moja, umeanzishwa.
(z) Tume ya Utangazaji imeanzishwa. Radio “Spice FM” ya Sauti ya Tanzania
Zanzibar, Televisheni mbili za binafsi (Zanzibar Cable Television na Furaha
Cable Television) zimeanzishwa.
(aa) Chuo cha Waandishi wa Habari (chini ya Idara ya
Habari Maelezo) kimeimarishwa kwa
kupatiwa vifaa vya kisasa na Asasi nne zisizokuwa za Serikali za waandishi wa
habari (Zanzibar Press Club, Pemba Press Club, Zanzibar Media Women Forum na
Journalist Association of Zanzibar) zimeanzishwa.
(bb) Mafunzo kwa
wafanyakazi wa sekta ya habari yameendelea kutolewa na jumla ya wafanyakazi 84
wamepatiwa fursa za masomo.
69. Katika maeneo mengine muhimu, mafanikio yafuatayo
yamepatikana:-
Utawala
Bora
(a) Ili kuimarisha
utawala wa sheria, uwazi, uadilifu na uwajibikaji katika utendaji wa Serikali,
Wizara ya Nchi (AR) Katiba na Utawala Bora imeanzishwa na mabadidliko ya Nane
na Tisa ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 yamepitishwa. Aidha, bendera ya Zanzibar imeanzishwa.
(b) Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP)
imeanzishwa na Sheria ya Mwenendo wa Jinai imerekebishwa ili kutoa fursa kwa
waendesha mashtaka wa Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka kufanya usimamizi na uendeshaji wa kesi
mahakamani badala ya Polisi. Aidha
sheria mbali mbali zimeimarishwa na kurekebishwa.
Demokrasia
(c) Elimu ya
uraia imeendelea kutolewa na dhana ya haki za binadamu, demokrasia, utawala
bora na wajibu wa watumishi wa umma katika mfumo wa vyama vingi imepewa
msisitizo.
(d) Sheria ya
Uchaguzi ya Zanzibar imefanyiwa marekebisho. Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC)
imerekebishwa na Daftari la Kudumu la Wapiga kura limeanzishwa.
Madaraka
ya Wananchi
(e) Rasimu ya awali
ya Sera mpya ya Serikali za Mitaa,
imetayarishwa na kuwasilishwa kwa wadau mbali mbali.
(f) Kamati za
maendeleo za Mikoa na Wilaya zimeanzishwa. Katika ngazi ya Shehia kamati za
maendeleo zimeundwa na kuwashirikisha kikamilifu wananchi katika kupanga na
kusimamia utekelezaji wa miradi yao ya maendeleo. Jumla ya miradi 73 yenye thamani ya T.Shs. 2,246,761,187/=
imetekelezwa chini ya mpango wa TASAF, kati yake 33 ikiwa Pemba na 40 Unguja.
Wananchi wamechangia asilimia 20
ya gharama zote za miradi hiyo.
Vita
Dhidi ya Rushwa
(g) Ili kujenga
mazingira mazuri ya kuendeleza vita dhidi ya rushwa. uamuzi wa kuunganisha
masuala ya rushwa na maadili ya viongozi na kuunda taasisi moja ya kuzuia
rushwa na kusimamia maadili ya viongozi, umefikiwa. Rasimu ya awali ya Muswada wa Sheria ya Kuzuia Rushwa na
Kusimamia Maadili ya Viongozi, tayari imekamilika na Mpango wa Zanzibar wa
Kuimarisha Utawala Bora, umeandaliwa.
Ulinzi
na Usalama
(h) Vikosi vyote
vya SMZ vimeimarishwa kwa kupatiwa mafunzo, vifaa na vitendea kazi. Sheria ya
kuanzishwa kwa Kikosi cha Valantia imepitishwa ili kukipa nguvu za kisheria
katika utekelezaji wa kazi na majukumu
yake.
(i) Vikosi vya SMZ
kwa kushirikiana na vyombo vyengine vya ulinzi na usalama hususan Jeshi la
Polisi, vimeshiriki kikamilifu katika kuimarisha ulinzi wa raia na mali zao na
kushiriki katika shughuli mbali mbali
za maendeleo ukiwemo ujenzi wa nyumba za
Michenzani.
(j) Vikosi vya SMZ,
hususan KMKM vimeshiriki katika mapambano dhidi ya magendo ya karafuu na
hujuma nyingine za uchumi na kujenga
mahusiano mema na wananchi wanaoishi karibu na maeneo yao. Chuo cha Ufundi cha JKU kinatoa mchango
mkubwa katika kuwapatia vijana elimu ya amali na stadi mbali mbali za ufundi.
70. Katika kuyaendeleza
makundi mbali mbali ya kijamii, mafanikio yafuatayo yamepatikana:-
Watoto
(a) Sera ya Uhai,
Hifadhi na Maendeleo ya watoto, imetayarishwa na utafiti wenye lengo la
kufahamu ukubwa wa tatizo la ajira kwa watoto “rapid assessment” umefanywa.
Mafunzo yametolewa kwa wadau
mbali mbali juu ya Mkataba Nam. 182 na 138 wa ILO kuhusiana na suala la ajira
kwa watoto.
Wanawake
(b) Hatua ya
kurekebisha sheria zinazowabagua na
kuwadhalilisha
wanawake katika usawa na maslahi yao imetekelezwa. Sheria ya makosa ya
kujamiiana na sheria ya kuwalinda wari, wajane na vizuka, zimerekebishwa na
Sera ya Hifadhi na Maendeleo ya Wanawake, imetayarishwa.
(c) Mradi maalum wa
kuinua kipato cha wanawake ili kupunguza ajira mbaya kwa watoto umeanzishwa.
Jumla ya vijana wanawake 3,434 wameunganishwa na mashirika yanayotoa mikopo
likiwemo PRIDE, WEDTF na CHANGAMOTO na kupatiwa mikopo yenye thamani ya T.shs.
405 milioni.
(d) Hatua ya kuwashirikisha wanawake katika ngazi mbali mbali za maamuzi
ya kisiasa, utawala, uongozi na menejimenti, imeendelea kutekelezwa. Marekebisho ya Nane ya Katiba ya Zanzibar ya
mwaka 1984, yameongeza idadi ya viti
vya wanawake katika BLW (viti maalum) kutoka asilimia 15 hadi 30. Aidha, wanawake wamepatiwa nafasi za elimu
na kuwa na mazingira mazuri ya kupata elimu kuanzia skuli za msingi hadi vyuo
vikuu.
Vijana
(e) Sera ya
Maendeleo ya Vijana imetayarishwa na rasimu ya awali ya Sera ya Elimu ya Amali na Mafunzo, imekamilika. Mradi wa Elimu Mbadala na Mafunzo ya Elimu
ya Amali umeanzishwa na Kituo cha Elimu
ya Amali cha Mwanakwerekwe kimefanyiwa matengenezo na kuimarishwa.
(f) Jumla ya vijana
1,534 wamepatiwa ajira kupitia sekta binafsi na wengine 360 wamepatiwa mafunzo
na ujuzi katika fani mbali mbali za ufundi.
Mahkama ya kazi imeanzishwa.
Walemavu
(g) Ili kulinda na
kusimamia haki, usawa na maendeleo ya watu wenye ulemavu, Baraza la Taifa la
Maendeleo ya Watu wenye Ulemavu, limeanzishwa chini ya uongozi wa Afisi ya
Waziri Kiongozi. Aidha, Sera ya
Walemavu imepitishwa na rasimu ya awali ya Sheria ya Walemavu imekamilika.
(h) Hatua za kuelimisha jamii juu ya masuala mbali
mbali ya kuwaendeleza watu wenye ulemavu, zimetekelezwa. Jumla ya watu 219 wenye ulemavu wamepatiwa
mafunzo ya uendeshaji wa biashara ndogo ndogo Unguja na Pemba pamoja na
kupatiwa mkopo wa kujiendeleza. Watu
193 wenye ulemavu wa kutosikia (viziwi) wamepatiwa mafunzo ya lugha ya
ishara. Aidha, kazi ya utengenezaji wa
visaidizi vya walemavu hasa viatu na fimbo
katika Hospitali ya Mnazi Mmoja inaendelezwa.
71. Ili kuendeleza
na kuimarisha shughuli za wananchi za kujitegemea, hatua ya kuutambua na kuupatia usajili rasmi Umoja wa
Wafanyabiashara ndogo ndogo (Jua Kali), Umoja wa Wenye Magari ya daladala na
Umoja wa Watembezaji Watalii imetekelezwa.
Eneo maalum la Saateni, limetengwa kwa wafanyabiashara wadogo wadogo na
kazi ya kulijenga na kulitengeneza
inaendelea vizuri. Mfuko maalum wa kuwaendeleza wazalishaji wadogo
wadogo, umeanzishwa.
SURA YA SABA
Utawala Bora na Haki za Binadamu
72. Umuhimu wa kipekee umekuwa ukitolewa na Chama
Cha Mapinduzi kuhusu suala la ujenzi na uimarishaji wa utawala bora na
demokrasia katika nchi. Kwa takriban miaka 13 sasa (1993 - 2005)
Serikali, chini ya uongozi na usimamizi thabiti wa CCM imeendelea kufanya
mageuzi makubwa katika utumishi wa umma
ngazi za Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.
73. Kwa kupitia Programu ya Kuboresha Utumishi
Serikalini (1993-1999); Programu ya Kuboresha Utendaji Kazi na Utoaji Huduma
Bora (2000-2011) katika utumishi wa Umma na Programu ya Maboresho ya Serikali
za Mitaa (1998-2008) lengo kuu limeendelea kuufanya utumishi wa umma nchini
kuwa chombo chenye kutukuka; chenye kuiwezesha Tanzania kuwa na uchumi
endelevu; wenye kuleta matumaini; na unaoweza kutokomeza umaskini katika karne
hii. Mabadiliko makubwa pia yamefanyika
katika mfumo, muundo na menejimenti ya Serikali za Mitaa kwa makusudi ya
kuimarisha madaraka ya wananchi.
Matokeo yake ni kujenga misingi ya utawala bora na demokrasia, na
kudhoofisha kabisa hulka za "Miungu-watu" katika ngazi za Kata,
Vijiji, Vitongoji na Mitaa. Utashi huu
wa kisiasa umeweza kuwa na matokeo
katika uimarishaji wa Serikali za Mitaa kwa kuzipa madaraka zaidi ya uamuzi (Political
decentralisation); na kuzipa mamlaka zaidi ya uamuzi juu ya matumizi ya
fedha (finacial decentralisation); kuzipa mamlaka zaidi
juu ya masuala ya uendeshaji (administrative decentralisation). Hali hii imepelekea kwenye kujenga misingi
ya uwajibikaji, yenye kuzingatia demokrasia, uwazi, mipango shirikishi, sheria,
kanuni, na taratibu ndani na nje ya vikao.
74. Kwa upande wa haki za binadamu, Tume ya Haki
za Binadamu na Utawala Bora iliundwa mwaka 2001 na inafanya kazi zake kwa uhuru
na uwazi. Kuundwa kwa Tume hiyo
kumeiwezesha Tanzania kuwa na mfumo mzuri na wa uhakika wa kufuatilia masuala
ya haki za binadamu.
Sheria
75. Sheria ni
huduma muhimu ya kiuchumi kwani ni mwezeshaji wa msingi katika kujenga
mazingira mazuri ya kuvutia vitega uchumi na kukuza biashara. Mfano wa sheria unapotetereka kiasi cha
kuonekana kuwa haki haitendeki kwa wakati au haitendeki kabisa, wawekezaji
hawavutiki kuleta mitaji yao.
76. Katika kipindi
cha 2000-2005, Sekta ya Sheria ilipewa uzito mkubwa kuliko ilivyokuwa miaka
mingi iliyopita. Yafuatayo ni miongoni
mwa mambo makubwa yaliyoweza kufanyika katika kipindi hicho:-
(a)
Kuanzishwa kwa Mahakama ya Biashara.
(b)
Kufunguliwa Ofisi mbili za Kanda za Mahakama Kuu,
Dar es Salaam na Bukoba.