CHAMA CHA MAPINDUZI

 

 

 

 

 

 

MAFANIKIO YA SERIKALI YA AWAMU YA TATU (1995-2005) NA UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI YA CCM YA MWAKA 2000

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Kimetolewa na Makao Makuu ya CCM

S.L.P. 50, DODOMA.

 

Aprili, 2005

 

 

 

UTANGULIZI

 

1.     Serikali ya Awamu ya Tatu  ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitekeleza Ilani mbili za Uchaguzi za CCM; yaani Ilani ya 1995 na ile ya 2000.  Sura ya kwanza ya taarifa hii inaelezea kwa ufupi mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi chote cha miaka kumi cha 1995-2005 cha uongozi wa Awamu ya Tatu.  Maelezo hayo yana umuhimu mkubwa wakati huu tukijiandaa kwa Awamu ya Nne ya uongozi wa nchi yetu.  Kutokana na ukubwa wa mafanikio hayo ambayo yameweka msingi wa maendeleo ya haraka zaidi kwa nchi yetu,  Awamu ya Nne itawajibika kuyaendeleza. 

 

2.     Kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tatu inamaliza muda wake wa kikatiba wa kuwa madarakani, ni vyema kuchukua fursa hii ya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, pia kugusia japo kwa muhutasari mafanikio ya Awamu hiyo.

 

3.     Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000 ilikuwa ni programu ya utekelezaji wa kipindi cha kwanza cha Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 Hadi 2010.  Lakini pia ilisadifu kipindi cha pili cha Awamu ya Tatu ya uongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa.

 

4.     Sura zote zilizobaki za taarifa hii zinaelezea kwa ufafanuzi utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2000 yakiwa ni  sehemu ya maandalizi ya Ilani ya 2005 ambayo imechapishwa katika kijitabu tofauti.  Utekelezaji wa Ilani ya 2000 kwa upande wa Zanzibar unaelezewa katika Sura ya Sita.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

SURA YA KWANZA

 

MAFANIKIO YA SERIKALI YA AWAMU YA TATU:1995-2005

 

 

5.     Uchaguzi Mkuu wa 2005 utafanyika katika mazingira ambapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itaingia katika awamu mpya ya uongozi (Awamu ya Nne) baada ya Awamu ya Tatu iliyoanza 1995 chini ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa kumaliza muda wake kwa mafanikio makubwa.  Katika kipindi chake cha kwanza  cha uongozi cha  1995 – 2000, Awamu ya Tatu ilifanya kazi nzuri ya kukamilisha kwa mafanikio makubwa utekelezaji wa sehemu ya pili na ya mwisho ya Mwelekeo wa CCM Katika Miaka ya Tisini.  Utekelezaji  huo ulifanyika kupitia Ilani ya CCM ya Uchaguzi  Mkuu wa Oktoba, 1995.  Aidha katika kipindi chake cha pili na cha mwisho  cha 2000 - 2005, Awamu ya Tatu imeweza kutekeleza kwa mafanikio makubwa   ya kujivunia, sehemu ya kwanza ya Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 Hadi 2010 kupitia   Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2000.

 

6.     Mafanikio ya Awamu ya Tatu kutokana na utekelezaji wa dhati wa Sera na Ilani  za CCM yanadhihirika katika mkakati wa urekebishaji wa uchumi wa nchi  kutoka  uchumi  uliodumaa  hadi kufikia uchumi uliochangamka na unaokua.  Mafanikio hayo ya msingi yameweza  kuzaa mafanikio katika Sekta zote za Kiuchumi, Kijamii na Kisiasa na kuiweka Tanzania katika njia ya uhakika ya maendeleo na kupambana na umaskini.

 

7.     Kwa jumla, katika kipindi cha miaka 10 iliyopita mafanikio makubwa yamepatikana yanayoendana na matarajio ya Dira ya Taifa ya 2025 hasa katika nyanja kuu zifuatazo:-

 

(a)            Utulivu wa kisiasa.

(b)            Utawala bora.

(c)             Utulizaji wa misingi ya uchumi mkuu (stabilization of macro-economic fundamentals)

(d)            Ukuaji mkubwa wa sekta ya Madini

 

8.     Mafanikio hayo ni kama yafuatavyo:-

 

 

 

(a)    Mafanikio Katika Uchumi

               

(i)     Pato la Taifa limeongezeka kutoka Dola (za Kimarekani) 5.6 bilioni mwaka 1995 hadi Dola 9.8 bilioni mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 75.

 

(ii)    Pato la kila mtu limeongezeka kutoka Dola 160 mwaka 1995 hadi Dola 260 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 62.5.

 

(iii)    Ukuaji wa Pato la Taifa  umeongezeka kutoka asilimia 3.6 mwaka 1995 hadi  asilimia 6.7mwaka 2004.

 

(iv)    Mfumuko wa bei umeshuka kutoka asilimia 27.1 mwaka 1995 hadi asilimia 4.2 mwaka 2004.

 

(v)    Asilimia ya Watanzania wanaoishi kwa kipato cha chini ya Dola moja ilishuka kutoka 50 mwaka 1995 hadi 20 mwaka 2004.

 

(vi)    Utekelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji  wa  Mashirika ya Umma umeweza  kuiondolea Serikali mzigo mzito wa kuendesha uchumi moja kwa moja.  Ubinafsishaji umeanza kujenga mazingira   ya ongezeko la tija  na ufanisi katika uzalishaji wa bidhaa   za viwandani.  Baada ya  kubinafsishwa  makampuni na mashirika hayo sasa yanaipatia Serikali  mapato makubwa badala ya kuendeshwa kwa ruzuku ya Serikali.

 

(vii)   Mauzo ya nje ya bidhaa yameongezeka kutoka thamani ya Dola 682.9 milioni mwaka 1995 hadi Dola 1,165.9 milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 70.7

 

(viii) Akiba ya fedha za kigeni kwa ajili ya kuagizia bidhaa kutoka nje imeongezeka kutoka uwezo wa kukidhi mahitaji ya mwezi 1.6 mwaka  1995 hadi mahitaji ya miezi 9 mwaka 2004.

 

 

 

(ix)    Ruzuku ya Serikali Kuu kwa Serikali za Mitaa ambazo ni chombo cha  wananchi wenyewe cha kusimamia maendeleo yao kule kule waliko, imeongezeka kutoka Shilingi 12.3  bilioni  mwaka 1995/96 hadi shilingi 392.2 bilioni mwaka 2004/05.  Hili ni ongezeko la asilimia 3,088.6(yaani zaidi ya mara 30).

 

(x)    Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kuweka mazingira mazuri  ya  kuvutia vitega uchumi na kupambana na rushwa, hivi  sasa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoongoza katika Afrika  katika kuvutia uwekezaji. Mwaka 2004 Tanzania ilipata tuzo ya kuwa nchi ya kwanza Afrika kwa uwekaji wa mazingira mazuri ya uwekezaji. Uwekezaji wa moja kwa moja wa mitaji kutoka nje umeongezeka kutoka Dola 50.2 milioni mwaka 1995 hadi Dola 247.8 milioni mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 394.

 

(xi)    Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kupambana na rushwa na kuziba mianya ya ukwepaji  wa  kulipa kodi pamoja na zoezi la ubinafsishaji wa mashirika ya umma, hatua ambayo imeboresha uzalishaji, makusanyo ya mapato ya Serikali yameongezeka kutoka wastani wa shs. 25 bilioni kwa mwezi, mwaka 1995 hadi wastani wa sh. 160 bilioni kwa mwezi, mwaka 2005.  Hili ni ongezeko la asilimia 540.

 

(xii)   Tanzania ilitimiza masharti ya Mpango wa Kuzifutia Madeni Nchi Zenye  Madeni Makubwa (HIPC) na hivyo kuingizwa katika Mpango huo mwaka 1999.  Kutokana na hali hiyo, kuanzia mwaka 2002/2003 hadi 2004/2005, Tanzania ilitekeleza Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) ambapo fedha ambazo zingetumika kulipia madeni ya nje yaliyofutwa, sasa zilielekezwa katika sekta teule za huduma za jamii na kiuchumi na miundombinu  zinazowagusa moja kwa moja wananchi wa kawaida kwa manufaa ya pamoja.  Sekta hizo ni elimu, afya, maji, barabara za vijijini, kilimo na utawala bora, hususan Mahakama.

 

(xiii) Kutokana na juhudi za makusudi za kuimarisha utalii kwa lengo la kuchangia katika ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira, idadi ya watalii walioingia nchini imeongezeka kutoka watalii 295,000 mwaka 1995 hadi 582,000 mwaka 2004.  Hili ni ongezeko la asilimia 97.3  Aidha, mapato yatokanayo na utalii nayo yameongezeka kutoka Dola 259 milioni mwaka 1995 hadi Dola 746 milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 188.0.  Nafasi za ajira kwenye Sekta ya Utalii zimeongezeka kutoka 96,000 hadi 160,750 sawa na ongezeko la asilimia 67.4

 

(xiv) Kutokana na utekelezaji wa sera za makusudi za kuvutia wawekezaji  wakubwa na teknolojia ya kisasa katika uchimbaji wa madini, hasa dhahabu, imefunguliwa migodi mikubwa Nzega, Geita, Kahama, Mara n.k.  Kutokana na maendeleo hayo, uuzaji wa madini umeongezeka kwa kiasi kikubwa kutoka thamani ya Sh. 452.0 milioni mwaka 1995 hadi Sh. 22,786.0 milioni mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 4,941.

               

(xv)   Kutokana na utulivu wa mazingira ya kisiasa na kiuchumi, biashara imechangamka nchini.  Mchango wa Sekta ya Biashara kwa Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.4 mwaka 1995 hadi asilimia 16.8 mwaka 2004.  Mchango wa Sekta ya Fedha umeongezeka kutoka asilimia 5.9 hadi asilimia 12.1 katika kipindi hicho.  Mchango wa Sekta ya Viwanda nao uliongezeka kutoka asilimia 4.5 hadi 8.7.  Aidha, mchango wa Sekta ya Madini kwa Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 0.1 mwaka 1995 hadi asilimia 3.0 mwaka 2004.

 

(b)    Mafanikio katika Huduma za Kiuchumi Na Miundombinu

               

Barabara na Madaraja

 

 

(i)     Toka mwaka 2001, Serikali imekuwa ikitenga Sh.1.8  bilioni kila mwezi kwa ajili ya ujenzi wa barabara nchini.  Fedha hizo kwa pamoja na zile za Mfuko  wa Barabara na za wahisani zimewezesha uimarishaji na utanuzi wa kiasi kikubwa wa mtandao wa barabara kuu na za vijijini nchi nzima.  Urefu wa barabara za lami nchini umefikia kilomita 4,837 mwaka 2004.  Kwa upande wa barabara  za  changarawe/udongo, urefu umefikia kilomita 80,063 mwaka 2004.  Aidha, wakati ujenzi wa barabara   kwa kiwango cha lami ukiwa unaendelea kwa kasi, barabara za changarawe/udongo za Taifa, Mikoa,  Wilaya  na  za Vijijini ziko katika hali nzuri ya kupitika kuliko zilivyokuwa 1995 kutokana na kufanyiwa matengenezo  ya mara kwa mara.

 


(ii)    Ujenzi wa Daraja la Mto Rufiji linalojulikana sasa kama Daraja la Mkapa ulikamilika mwaka 2004 na hivyo kuifungulia milango ya maendeleo  ya kiuchumi Mikoa ya Kusini.

 

Mawasiliano

 

                (iii)    Tanzania katika kipindi hiki imeshuhudia ongezeko kubwa la mtandao wa mawasiliano, hasa ya simu za mkononi.  Idadi ya watu wanaomiliki simu (za aina zote) imefikia  watu 2,115,591 mwaka 2004.

 

Uchukuzi na Usafirishaji

 

(iv)    Reli ya Dodoma - Singida  ilifunguliwa katika kipindi  hiki.  Aidha, kwa  jumla, huduma za usafirishaji na uchukuzi wa abiria na mizigo kwa njia za barabara, reli, maji na anga zimekuwa bora zaidi kwa kiwango  kikubwa mijini na mikoani kuliko zilizvyokuwa mwaka 1995

 

Umeme

 

(v)    Katika sekta ya umeme, Mradi wa Gesi ya Songosongo umekamilika na kuunganishwa na mfumo wa uzalishaji wa umeme wa Gridi ya Taifa  mwaka 2004. Aidha, mradi wa umeme wa Kihansi ulikamilika.  Miradi hiyo imeliongezea Taifa uhakika wa upatikanaji wa umeme.

 

(vi)    Hadi  kufikia mwishoni mwa mwaka 2004, Serikali ilikwishafikisha umeme katika miji iliyo Makao Makuu ya Wilaya  8 kati ya 18  zilizoahidiwa na CCM katika Ilani yake ya Uchaguzi ya 2000.  Ufikishaji  umeme katika miji mingine 6 ulikuwa umefikia hatua kubwa kwa ajili ya ufunguzi mwaka 2005.  Miradi ya ufikishaji umeme katika miji 5  iliyobaki iko katika hatua za maandalizi ya awali.

 

Sekta ya Fedha

 

                (vii)   Sekta ya Fedha, hasa huduma za mabenki, imeimarika kwa kiasi kikubwa kutokana na kufunguliwa mabenki kadha makubwa ya biashara na ya rasilimali.  Mabenki hayo yameweka msingi wa kuwawezesha wawekezaji kwa kuwapatia mikopo  na hivyo kuchangamsha harakati za kiuchumi na kupambana na umaskini.

 

(c)    Mafanikio Katika Huduma za Jamii

 

                Kuongezeka kwa ubora wa huduma mbalimbali za kiuchumi na kijamii ni miongoni mwa manufaa ya kukua kwa uchumi wa taifa ambayo wananchi wa kawaida vijijini na mijini wameanza kuyafaidi kwa pamoja. 

 

Elimu

 

(i)     Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2000, uliandaliwa Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) mwaka 2002 kama sehemu ya utekelezaji wa Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) na ni matunda ya Tanzania kuingia katika HIPC.  Aidha, Mpango wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ulibuniwa kwa ajili ya kusaidia nguvu za wananchi kwa kutumia mbinu shirikishi kama ilivyoelekezwa  na Sera  za CCM na Ilani zake, katika juhudi zao za kujiondolea  kero.  Kiasi cha asilimia 60 ya miradi ya TASAF katika Wilaya 40 za kwanza za majaribio imekuwa katika sekta  ya Elimu.  Chini ya mipango hiyo miwili, yafutayo yamefanyika na yanaendelea:-

 


·        Kufutwa kwa ada ya shule za msingi za Serikali mwaka 2003.

               

·        Shule nyingi zimekarabatiwa nchi nzima.

                            

 

 

·        Idadi ya vyumba vya madarasa ya elimu  ya  msingi imeongezeka kutoka vyumba 57,708  Mwaka 1995 hadi  vyumba 96,215  Mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 66.7

 

·        Idadi ya shule za msingi za Serikali imeongezeka kutoka 10,891mwaka 1995 hadi 13,533 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 24.3.

                       

·        Idadi ya watoto walioandikishwa Darasa la Kwanza kila mwaka imeongezeka kutoka 712,593 mwaka 1995 hadi 1,368,315 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 47.9

                       

·        Idadi ya wanafunzi katika ngazi ya elimu ya msingi imeongezeka kutoka wanafunzi 3,877,643 mwaka 1995 hadi wanafunzi 7,083,063 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 82.7.

                       

·        Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi kwa kutumia kigezo cha GER (wanafunzi wote kama  asilimia  ya idadi ya watoto  wa rika husika la umri wa miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia 77.5 mwaka 1995 hadi asilimia 106.3 mwaka 2004.

                       

·        Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi  kwa kutumia kigezo cha NER (wanafunzi wa miaka 7 - 13 kama asilimia  ya watoto wote wa rika husika la miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia 55.3 mwaka 1995 hadi asilimia 90.5 mwaka 2004.

                       

·        Kiwango cha kufaulu katika Mtihani wa Darasa la Saba kimefikia asilimia 48.6 mwaka 2004 kutoka asilimia 14.6 mwaka 1995.

 

·        Idadi ya watahiniwa wanaofaulu mitihadi ya ufundi stadi imeongezeka kutoka asilimia 51 mwaka 1995 hadi asilimia 70 mwaka 2004.

 

·        Idadi ya watahiniwa wa Mitihani ya Ufundi Stadi imeongezeka kutoka 11,000  mwaka 1995 hadi 22,000 mwaka 2004 ambalo ni ongezeko la watahiniwa 11,000 sawa na asilimia 100.

 

·        Idadi ya wanafunzi katika shule za sekondari imeongezeka kwa asilimia 117.

 

·        Viwango vya kufaulu katika shule za sekondari vimeongezeka kutoka asilimia 24.6 hadi asilimia 38.8 kwa sekondari za kawaida na asilimia 70.7 hadi 80.7 kwenye sekondari za juu.

 

·        Idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vya umma imeongezeka kutoka 7,785 mwaka 1995 hadi 32,681 mwaka 2004/05 sawa na ongezeko la asilimia 319.8.  Kwa upande wa wanafunzi wa kike, waliongezeka kutoka 1,135 hadi 10,039 sawa na ongezeko la asilimia 784.5.

 

        (ii)    Baada ya mafanikio mazuri ya kusisimua ya MMEM, Serikali imeanza kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES) kuanzia mwaka 2004.  Ada ya shule za sekondari  za kutwa za Serikali imepunguzwa kwa asilimia 50 wakati hatua nyingine za kukarabati na kujenga majengo ya sekondari nchi nzima zinaendelea.

 

Afya

               

(iii)    Chanjo za watoto chini ya umri wa miaka mitano zimefikia asilimia 90 mwaka 2004. Kwa kiwango hicho, Tanzania imevuka kiwango cha kimataifa cha asilimia 80.

 

(iv)    Pamoja na janga la UKIMWI, Sensa ya Taifa ya 2002 imeonyesha kwamba matarajio ya kuishi ya Mtanzania yameongezeka kutoka umri wa miaka 50 mwaka 1988 hadi miaka 51 mwaka 2002.

               

(v)             Mifuko  ya Afya ya Jamii imeanzishwa ili  kuwawezesha              wananchi wa kawaida  vijijini na mijini kukabiliana na gharama za tiba.  Aidha, Bima ya Afya  imeanzishwa kwa ajili ya wafanyakazi wa Sekta ya Umma.

 

(vi)    Ukarabati mkubwa wa hospitali kuanzia Hospitali ya Taifa ya Muhimbili mpaka  hospitali za Mikoa na Wilaya ama umekamilika au uko katika hatua mbalimbali za utekelezaji.  Mashine za “X-Ray” na “Ultra-sound” na jenereta zimefungwa katika hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa.

 

(vii)   Katika harakati za kuongeza ubora wa utoaji wa huduma za afya, kumekuwa na ongezeko la mtandao wa vituo vya kutolea huduma nchi nzima kama ifuatavyo:-

 

·        Hospitali kutoka 194 mwaka 1995 hadi 221 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 14.

 

·        Vituo vya afya kutoka 343 mwaka 1995 hadi 433 mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 26.2. 

 

·        Zahanati kutoka 3,832  mwaka 1995 hadi 4,622 mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 20.6.

 


        (viii) Kufutwa kwa kodi kwenye vyandarua  na bidhaa zinazosaidia vita dhidi ya malaria.

 

(ix)           Programu kabambe ya kukabiliana na janga la UKIMWI imeanzishwa na inatekelezwa.

 

(x)             Kwa jumla uhaba wa dawa uliokuwepo miaka ya tisini sasa haupo tena.

 

 

 

 

 

 

Maji Mijini na Vijijini

 

(x)    Idadi ya wakazi mijini wanaopata huduma ya maji safi na salama imeongezeka kutoka asilimia 60 mwaka 1995 hadi asilimia 74.0 mwaka 2004.

 

(xi)    Idadi  ya wananchi  vijijini wanaopata maji safi na salama imeongezeka kutoka asilimia 42 mwaka 1995 hadi asilimia 53.5 mwaka 2003

 

(xii)   Sambamba na miradi midogo midogo ya maji inayoendelea nchi nzima, miradi mikubwa ya maji ya Dodoma na Chalinze imekamilika.  Aidha, miradi  kabambe ya Dar es Salaam na kuvuta maji toka Ziwa Victoria kwenda Shinyanga Mjini na Kahama imeanza na inaendelea.

 

Ardhi na Makazi

 

(xiii) Uwekezaji mkubwa wa sekta binafsi na wa wananchi mmoja mmoja umeongezeka katika ujenzi wa majumba, na hivyo kubadili sura ya Jiji la Dar es Salaam na miji mingine kwa kiasi kikubwa.

 

(xiv) Mwamko unaoongezeka wa kujenga nyumba nzuri miongoni mwa wananchi  vijijini unabadilisha kwa kasi sura ya vijiji vingi  nchi nzima.

 

(xv)   Mradi wa kupima viwanja 20,000 katika jiji la Dar es Salaam umepunguza  bughudha katika kupata viwanja na kuziba mwanya mkubwa wa rushwa iliyokuwa ikiwasumbua wananchi.

 

(d)    Mafanikio Katika Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi

               

Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi ni sera iliyokusudiwa kuwajengea mazingira Watanzania yanayowawezesha kufaidi  mmoja  mmoja manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa katika kuongeza vipato vyao kutokana na juhudi zao za kupambana na umaskini.  Katika kipindi hiki, Serikali ya CCM imeweza kuchukua hatua kadha za kuyafikisha kwa wananchi mmoja mmoja manufaa  ya kukua kwa uchumi wa Taifa kama ifuatavyo:-

 

(i)     Kufuta kodi ya maendeleo mwaka 2004 na nyingi nyingine ambazo zilikuwa kero  kwa wananchi na ambazo pia zilidumaza ari ya kupambana na umaskini.  Hatua hii imewakombolea wananchi kipato chao kilichokuwa  kikiwatoka ambacho sasa wanakitumia wenyewe katika harakati zao za kupambana na umaskini.  Pia imeziba mwanya wa rushwa uliokuwa ukiwasumbua sana wananchi, kupitia kodi hii.

 

(ii)    Serikali imeanza kutoa fidia kwa mbolea na baadhi ya dawa za mifugo  ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Uwezeshaji wa  Wananchi Kiuchmi unaowasaidia kupambana na  umaskini kwa namna ambayo itawaongezea kipato.

 

(iii)    Pamoja na kuongezeka na kushamiri kwa harakati za kujiajiri, ajira katika sekta rasmi pia zimeongezeka.  Idadi ya waajiriwa katika sekta  rasmi ya umma na isiyokuwa ya u