CHAMA CHA
MAPINDUZI
MAFANIKIO YA
SERIKALI YA AWAMU YA TATU (1995-2005) NA UTEKELEZAJI WA ILANI YA UCHAGUZI YA
CCM YA MWAKA 2000
Kimetolewa
na Makao Makuu ya CCM
S.L.P.
50, DODOMA.
Aprili,
2005
UTANGULIZI
1. Serikali ya
Awamu ya Tatu ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ilitekeleza Ilani mbili za Uchaguzi za CCM; yaani Ilani ya 1995 na ile
ya 2000. Sura ya kwanza ya taarifa hii
inaelezea kwa ufupi mafanikio makubwa yaliyopatikana katika kipindi chote cha
miaka kumi cha 1995-2005 cha uongozi wa Awamu ya Tatu. Maelezo hayo yana umuhimu mkubwa wakati huu
tukijiandaa kwa Awamu ya Nne ya uongozi wa nchi yetu. Kutokana na ukubwa wa mafanikio hayo ambayo yameweka msingi wa
maendeleo ya haraka zaidi kwa nchi yetu,
Awamu ya Nne itawajibika kuyaendeleza.
2. Kwa kuwa
Serikali ya Awamu ya Tatu inamaliza muda wake wa kikatiba wa kuwa madarakani,
ni vyema kuchukua fursa hii ya kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya
CCM, pia kugusia japo kwa muhutasari mafanikio ya Awamu hiyo.
3. Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2000 ilikuwa ni programu ya utekelezaji wa kipindi cha
kwanza cha Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 Hadi 2010. Lakini pia ilisadifu kipindi cha pili cha
Awamu ya Tatu ya uongozi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini
ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa.
4. Sura zote
zilizobaki za taarifa hii zinaelezea kwa ufafanuzi utekelezaji wa Ilani ya
Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2000 yakiwa ni
sehemu ya maandalizi ya Ilani ya 2005 ambayo imechapishwa katika kijitabu
tofauti. Utekelezaji wa Ilani ya 2000
kwa upande wa Zanzibar unaelezewa katika Sura ya Sita.
SURA YA
KWANZA
MAFANIKIO YA SERIKALI YA
AWAMU YA TATU:1995-2005
5. Uchaguzi
Mkuu wa 2005 utafanyika katika mazingira ambapo Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania itaingia katika awamu mpya ya uongozi (Awamu ya Nne) baada ya Awamu
ya Tatu iliyoanza 1995 chini ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa kumaliza
muda wake kwa mafanikio makubwa. Katika
kipindi chake cha kwanza cha uongozi
cha 1995 – 2000, Awamu ya Tatu ilifanya
kazi nzuri ya kukamilisha kwa mafanikio makubwa utekelezaji wa sehemu ya pili
na ya mwisho ya Mwelekeo wa CCM Katika Miaka ya Tisini. Utekelezaji
huo ulifanyika kupitia Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 1995. Aidha katika kipindi chake cha pili na cha
mwisho cha 2000 - 2005, Awamu ya Tatu
imeweza kutekeleza kwa mafanikio makubwa
ya kujivunia, sehemu ya kwanza ya Mwelekeo wa Sera za CCM Katika
Miaka ya 2000 Hadi 2010 kupitia Ilani
ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2000.
6. Mafanikio
ya Awamu ya Tatu kutokana na utekelezaji wa dhati wa Sera na Ilani za CCM yanadhihirika katika mkakati wa
urekebishaji wa uchumi wa nchi kutoka uchumi
uliodumaa hadi kufikia uchumi
uliochangamka na unaokua. Mafanikio
hayo ya msingi yameweza kuzaa mafanikio
katika Sekta zote za Kiuchumi, Kijamii na Kisiasa na kuiweka Tanzania katika
njia ya uhakika ya maendeleo na kupambana na umaskini.
7. Kwa
jumla, katika kipindi cha miaka 10 iliyopita mafanikio makubwa yamepatikana yanayoendana
na matarajio ya Dira ya Taifa ya 2025 hasa katika nyanja kuu zifuatazo:-
(a)
Utulivu wa kisiasa.
(b)
Utawala bora.
(c)
Utulizaji wa misingi ya uchumi mkuu (stabilization of macro-economic
fundamentals)
(d)
Ukuaji mkubwa wa sekta ya Madini
8. Mafanikio
hayo ni kama yafuatavyo:-
(a) Mafanikio Katika Uchumi
(i) Pato la Taifa
limeongezeka kutoka Dola (za Kimarekani) 5.6 bilioni mwaka 1995 hadi Dola 9.8
bilioni mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 75.
(ii) Pato la kila
mtu limeongezeka kutoka Dola 160 mwaka 1995 hadi Dola 260 mwaka 2004 likiwa ni
ongezeko la asilimia 62.5.
(iii) Ukuaji wa Pato la Taifa
umeongezeka kutoka asilimia 3.6 mwaka 1995 hadi asilimia 6.7mwaka 2004.
(iv) Mfumuko wa bei umeshuka kutoka asilimia 27.1 mwaka 1995 hadi
asilimia 4.2 mwaka 2004.
(v) Asilimia ya
Watanzania wanaoishi kwa kipato cha chini ya Dola moja ilishuka kutoka 50 mwaka
1995 hadi 20 mwaka 2004.
(vi) Utekelezaji wa Sera ya Ubinafsishaji wa Mashirika ya Umma
umeweza kuiondolea Serikali mzigo mzito
wa kuendesha uchumi moja kwa moja.
Ubinafsishaji umeanza kujenga mazingira ya ongezeko la tija na
ufanisi katika uzalishaji wa bidhaa za
viwandani. Baada ya kubinafsishwa makampuni na mashirika hayo sasa yanaipatia Serikali mapato makubwa badala ya kuendeshwa kwa
ruzuku ya Serikali.
(vii) Mauzo ya nje ya bidhaa yameongezeka kutoka thamani ya Dola 682.9
milioni mwaka 1995 hadi Dola 1,165.9 milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la
asilimia 70.7
(viii) Akiba ya fedha za kigeni kwa ajili ya kuagizia bidhaa kutoka nje
imeongezeka kutoka uwezo wa kukidhi mahitaji ya mwezi 1.6 mwaka 1995 hadi mahitaji ya miezi 9 mwaka 2004.
(ix) Ruzuku ya Serikali Kuu kwa Serikali za Mitaa ambazo ni chombo
cha wananchi wenyewe cha kusimamia
maendeleo yao kule kule waliko, imeongezeka kutoka Shilingi 12.3 bilioni
mwaka 1995/96 hadi shilingi 392.2 bilioni mwaka 2004/05. Hili ni ongezeko la asilimia 3,088.6(yaani
zaidi ya mara 30).
(x) Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kuweka
mazingira mazuri ya kuvutia vitega uchumi na kupambana na
rushwa, hivi sasa Tanzania ni miongoni
mwa nchi zinazoongoza katika Afrika
katika kuvutia uwekezaji. Mwaka 2004 Tanzania ilipata tuzo ya kuwa nchi
ya kwanza Afrika kwa uwekaji wa mazingira mazuri ya uwekezaji. Uwekezaji wa
moja kwa moja wa mitaji kutoka nje umeongezeka kutoka Dola 50.2 milioni mwaka
1995 hadi Dola 247.8 milioni mwaka 2004 sawa na ongezeko la asilimia 394.
(xi) Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kupambana na
rushwa na kuziba mianya ya ukwepaji
wa kulipa kodi pamoja na zoezi
la ubinafsishaji wa mashirika ya umma, hatua ambayo imeboresha uzalishaji,
makusanyo ya mapato ya Serikali yameongezeka kutoka wastani wa shs. 25 bilioni
kwa mwezi, mwaka 1995 hadi wastani wa sh. 160 bilioni kwa mwezi, mwaka
2005. Hili ni ongezeko la asilimia 540.
(xii) Tanzania ilitimiza masharti ya Mpango wa Kuzifutia Madeni Nchi
Zenye Madeni Makubwa (HIPC) na
hivyo kuingizwa katika Mpango huo mwaka 1999.
Kutokana na hali hiyo, kuanzia mwaka 2002/2003 hadi 2004/2005, Tanzania
ilitekeleza Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) ambapo fedha
ambazo zingetumika kulipia madeni ya nje yaliyofutwa, sasa zilielekezwa katika
sekta teule za huduma za jamii na kiuchumi na miundombinu zinazowagusa moja kwa moja wananchi wa kawaida
kwa manufaa ya pamoja. Sekta hizo ni
elimu, afya, maji, barabara za vijijini, kilimo na utawala bora, hususan
Mahakama.
(xiii) Kutokana na juhudi za makusudi za kuimarisha utalii kwa lengo la
kuchangia katika ukuaji wa uchumi na kuongeza ajira, idadi ya watalii
walioingia nchini imeongezeka kutoka watalii 295,000 mwaka 1995 hadi 582,000
mwaka 2004. Hili ni ongezeko la
asilimia 97.3 Aidha, mapato yatokanayo
na utalii nayo yameongezeka kutoka Dola 259 milioni mwaka 1995 hadi Dola 746
milioni mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 188.0. Nafasi za ajira kwenye Sekta ya Utalii
zimeongezeka kutoka 96,000 hadi 160,750 sawa na ongezeko la asilimia 67.4
(xiv) Kutokana na utekelezaji wa sera za makusudi za kuvutia
wawekezaji wakubwa na teknolojia ya
kisasa katika uchimbaji wa madini, hasa dhahabu, imefunguliwa migodi mikubwa
Nzega, Geita, Kahama, Mara n.k.
Kutokana na maendeleo hayo, uuzaji wa madini umeongezeka kwa kiasi
kikubwa kutoka thamani ya Sh. 452.0 milioni mwaka 1995 hadi Sh. 22,786.0 milioni
mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la asilimia 4,941.
(xv) Kutokana na
utulivu wa mazingira ya kisiasa na kiuchumi, biashara imechangamka nchini. Mchango wa Sekta ya Biashara kwa Pato la
Taifa umeongezeka kutoka asilimia 2.4 mwaka 1995 hadi asilimia 16.8 mwaka
2004. Mchango wa Sekta ya Fedha
umeongezeka kutoka asilimia 5.9 hadi asilimia 12.1 katika kipindi hicho. Mchango wa Sekta ya Viwanda nao uliongezeka
kutoka asilimia 4.5 hadi 8.7. Aidha,
mchango wa Sekta ya Madini kwa Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 0.1
mwaka 1995 hadi asilimia 3.0 mwaka 2004.
(b) Mafanikio
katika Huduma za Kiuchumi Na Miundombinu
(i) Toka mwaka 2001, Serikali imekuwa ikitenga Sh.1.8 bilioni kila mwezi kwa ajili ya ujenzi wa
barabara nchini. Fedha hizo kwa pamoja
na zile za Mfuko wa Barabara na za
wahisani zimewezesha uimarishaji na utanuzi wa kiasi kikubwa wa mtandao wa
barabara kuu na za vijijini nchi nzima.
Urefu wa barabara za lami nchini umefikia kilomita 4,837 mwaka
2004. Kwa upande wa barabara za
changarawe/udongo, urefu umefikia kilomita 80,063 mwaka 2004. Aidha, wakati ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami ukiwa unaendelea kwa
kasi, barabara za changarawe/udongo za Taifa, Mikoa, Wilaya na za Vijijini ziko katika hali nzuri ya
kupitika kuliko zilivyokuwa 1995 kutokana na kufanyiwa matengenezo ya mara kwa mara.
(ii) Ujenzi wa Daraja la Mto Rufiji linalojulikana sasa kama Daraja la
Mkapa ulikamilika mwaka 2004 na hivyo kuifungulia milango ya maendeleo ya kiuchumi Mikoa ya Kusini.
Mawasiliano
(iii)
Tanzania katika kipindi hiki
imeshuhudia ongezeko kubwa la mtandao wa mawasiliano, hasa ya simu za
mkononi. Idadi ya watu wanaomiliki simu
(za aina zote) imefikia watu 2,115,591
mwaka 2004.
Uchukuzi na Usafirishaji
(iv) Reli ya Dodoma - Singida
ilifunguliwa katika kipindi
hiki. Aidha, kwa jumla, huduma za usafirishaji na uchukuzi wa
abiria na mizigo kwa njia za barabara, reli, maji na anga zimekuwa bora zaidi
kwa kiwango kikubwa mijini na mikoani
kuliko zilizvyokuwa mwaka 1995
Umeme
(v) Katika sekta ya umeme, Mradi wa Gesi ya Songosongo umekamilika na
kuunganishwa na mfumo wa uzalishaji wa umeme wa Gridi ya Taifa mwaka 2004. Aidha, mradi wa umeme wa Kihansi
ulikamilika. Miradi hiyo imeliongezea
Taifa uhakika wa upatikanaji wa umeme.
(vi) Hadi kufikia mwishoni mwa
mwaka 2004, Serikali ilikwishafikisha umeme katika miji iliyo Makao Makuu ya
Wilaya 8 kati ya 18 zilizoahidiwa na CCM katika Ilani yake ya
Uchaguzi ya 2000. Ufikishaji umeme katika miji mingine 6 ulikuwa umefikia
hatua kubwa kwa ajili ya ufunguzi mwaka 2005.
Miradi ya ufikishaji umeme katika miji 5 iliyobaki iko katika hatua za maandalizi ya awali.
Sekta
ya Fedha
(vii)
Sekta ya Fedha, hasa huduma za mabenki,
imeimarika kwa kiasi kikubwa kutokana na kufunguliwa mabenki kadha makubwa ya
biashara na ya rasilimali. Mabenki hayo
yameweka msingi wa kuwawezesha wawekezaji kwa kuwapatia mikopo na hivyo kuchangamsha harakati za kiuchumi
na kupambana na umaskini.
(c) Mafanikio Katika Huduma za Jamii
Kuongezeka
kwa ubora wa huduma mbalimbali za kiuchumi na kijamii ni miongoni mwa manufaa
ya kukua kwa uchumi wa taifa ambayo wananchi wa kawaida vijijini na mijini
wameanza kuyafaidi kwa pamoja.
(i) Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2000, uliandaliwa Mpango
wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) mwaka 2002 kama sehemu ya
utekelezaji wa Mkakati wa Kupunguza Umaskini (MKU) na ni matunda
ya Tanzania kuingia katika HIPC. Aidha,
Mpango wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) ulibuniwa kwa ajili ya kusaidia
nguvu za wananchi kwa kutumia mbinu shirikishi kama ilivyoelekezwa na Sera
za CCM na Ilani zake, katika juhudi zao za kujiondolea kero.
Kiasi cha asilimia 60 ya miradi ya TASAF katika Wilaya 40 za
kwanza za majaribio imekuwa katika sekta
ya Elimu. Chini ya mipango hiyo
miwili, yafutayo yamefanyika na yanaendelea:-
·
Kufutwa kwa ada ya shule za msingi za Serikali mwaka 2003.
·
Shule nyingi zimekarabatiwa nchi nzima.
·
Idadi ya vyumba vya madarasa ya elimu
ya msingi imeongezeka kutoka
vyumba 57,708 Mwaka 1995 hadi vyumba 96,215 Mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 66.7
·
Idadi ya shule za msingi za Serikali imeongezeka kutoka 10,891mwaka
1995 hadi 13,533 mwaka 2004, sawa na ongezeko la asilimia 24.3.
·
Idadi ya watoto walioandikishwa Darasa la Kwanza kila mwaka imeongezeka
kutoka 712,593 mwaka 1995 hadi 1,368,315 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko la
asilimia 47.9
·
Idadi ya wanafunzi katika ngazi ya elimu ya msingi imeongezeka kutoka
wanafunzi 3,877,643 mwaka 1995 hadi wanafunzi 7,083,063 mwaka 2004 likiwa ni
ongezeko la asilimia 82.7.
·
Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi kwa kutumia kigezo cha GER
(wanafunzi wote kama asilimia ya idadi ya watoto wa rika husika la umri wa miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia
77.5 mwaka 1995 hadi asilimia 106.3 mwaka 2004.
·
Uandikishaji katika ngazi ya elimu ya msingi kwa kutumia kigezo cha NER (wanafunzi wa miaka 7 - 13 kama
asilimia ya watoto wote wa rika husika
la miaka 7 - 13) umeongezeka kutoka asilimia 55.3 mwaka 1995 hadi asilimia 90.5
mwaka 2004.
·
Kiwango cha kufaulu katika Mtihani wa Darasa la Saba kimefikia asilimia
48.6 mwaka 2004 kutoka asilimia 14.6 mwaka 1995.
·
Idadi ya watahiniwa wanaofaulu mitihadi ya ufundi stadi imeongezeka
kutoka asilimia 51 mwaka 1995 hadi asilimia 70 mwaka 2004.
·
Idadi ya watahiniwa wa Mitihani ya Ufundi Stadi imeongezeka kutoka
11,000 mwaka 1995 hadi 22,000 mwaka
2004 ambalo ni ongezeko la watahiniwa 11,000 sawa na asilimia 100.
·
Idadi ya wanafunzi katika shule za sekondari imeongezeka kwa asilimia
117.
·
Viwango vya kufaulu katika shule za sekondari vimeongezeka kutoka
asilimia 24.6 hadi asilimia 38.8 kwa sekondari za kawaida na asilimia 70.7 hadi
80.7 kwenye sekondari za juu.
·
Idadi ya wanafunzi katika vyuo vikuu vya umma imeongezeka kutoka 7,785
mwaka 1995 hadi 32,681 mwaka 2004/05 sawa na ongezeko la asilimia 319.8. Kwa upande wa wanafunzi wa kike,
waliongezeka kutoka 1,135 hadi 10,039 sawa na ongezeko la asilimia 784.5.
(ii) Baada ya mafanikio mazuri ya kusisimua ya MMEM, Serikali
imeanza kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES)
kuanzia mwaka 2004. Ada ya shule za
sekondari za kutwa za Serikali
imepunguzwa kwa asilimia 50 wakati hatua nyingine za kukarabati na kujenga
majengo ya sekondari nchi nzima zinaendelea.
Afya
(iii) Chanjo za watoto chini ya umri wa miaka mitano zimefikia asilimia
90 mwaka 2004. Kwa kiwango hicho, Tanzania imevuka kiwango cha kimataifa cha
asilimia 80.
(iv) Pamoja na janga la UKIMWI, Sensa ya Taifa ya 2002 imeonyesha
kwamba matarajio ya kuishi ya Mtanzania yameongezeka kutoka umri wa miaka 50
mwaka 1988 hadi miaka 51 mwaka 2002.
(v)
Mifuko ya Afya ya Jamii
imeanzishwa ili kuwawezesha wananchi wa kawaida vijijini na mijini kukabiliana na gharama za
tiba. Aidha, Bima ya Afya imeanzishwa kwa ajili ya wafanyakazi wa
Sekta ya Umma.
(vi) Ukarabati mkubwa wa hospitali kuanzia Hospitali ya Taifa ya
Muhimbili mpaka hospitali za Mikoa na
Wilaya ama umekamilika au uko katika hatua mbalimbali za utekelezaji. Mashine za “X-Ray” na “Ultra-sound”
na jenereta zimefungwa katika hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa.
(vii) Katika harakati za kuongeza ubora wa utoaji wa huduma za afya,
kumekuwa na ongezeko la mtandao wa vituo vya kutolea huduma nchi nzima kama
ifuatavyo:-
·
Hospitali kutoka 194 mwaka 1995 hadi 221 mwaka 2004 likiwa ni ongezeko
la asilimia 14.
·
Vituo vya afya kutoka 343 mwaka 1995 hadi 433 mwaka 2004, likiwa ni
ongezeko la asilimia 26.2.
·
Zahanati kutoka 3,832 mwaka
1995 hadi 4,622 mwaka 2004, likiwa ni ongezeko la asilimia 20.6.
(viii)
Kufutwa kwa kodi kwenye vyandarua na bidhaa zinazosaidia vita dhidi ya
malaria.
(ix)
Programu kabambe ya kukabiliana na janga la UKIMWI imeanzishwa na
inatekelezwa.
(x)
Kwa jumla uhaba wa dawa uliokuwepo miaka ya tisini sasa haupo tena.
Maji
Mijini na Vijijini
(x) Idadi ya wakazi mijini wanaopata huduma ya maji safi na salama
imeongezeka kutoka asilimia 60 mwaka 1995 hadi asilimia 74.0 mwaka 2004.
(xi) Idadi ya wananchi vijijini wanaopata maji safi na salama
imeongezeka kutoka asilimia 42 mwaka 1995 hadi asilimia 53.5 mwaka 2003
(xii) Sambamba na miradi midogo midogo ya maji inayoendelea nchi nzima,
miradi mikubwa ya maji ya Dodoma na Chalinze imekamilika. Aidha, miradi kabambe ya Dar es Salaam na kuvuta maji toka Ziwa Victoria kwenda
Shinyanga Mjini na Kahama imeanza na inaendelea.
Ardhi
na Makazi
(xiii) Uwekezaji mkubwa wa sekta binafsi na wa wananchi mmoja mmoja
umeongezeka katika ujenzi wa majumba, na hivyo kubadili sura ya Jiji la Dar es
Salaam na miji mingine kwa kiasi kikubwa.
(xiv) Mwamko unaoongezeka wa kujenga nyumba nzuri miongoni mwa
wananchi vijijini unabadilisha kwa kasi
sura ya vijiji vingi nchi nzima.
(xv) Mradi wa kupima viwanja 20,000 katika jiji la Dar es Salaam
umepunguza bughudha katika kupata
viwanja na kuziba mwanya mkubwa wa rushwa iliyokuwa ikiwasumbua wananchi.
(d) Mafanikio Katika Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi
Uwezeshaji
wa Wananchi Kiuchumi ni sera iliyokusudiwa kuwajengea mazingira Watanzania
yanayowawezesha kufaidi mmoja mmoja manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa
katika kuongeza vipato vyao kutokana na juhudi zao za kupambana na umaskini. Katika kipindi hiki, Serikali ya CCM imeweza
kuchukua hatua kadha za kuyafikisha kwa wananchi mmoja mmoja manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa kama
ifuatavyo:-
(i) Kufuta kodi ya maendeleo mwaka 2004 na nyingi nyingine ambazo
zilikuwa kero kwa wananchi na ambazo
pia zilidumaza ari ya kupambana na umaskini.
Hatua hii imewakombolea wananchi kipato chao kilichokuwa kikiwatoka ambacho sasa wanakitumia wenyewe
katika harakati zao za kupambana na umaskini.
Pia imeziba mwanya wa rushwa uliokuwa ukiwasumbua sana wananchi, kupitia
kodi hii.
(ii) Serikali imeanza kutoa fidia kwa mbolea na baadhi ya dawa za
mifugo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji
wa Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi
Kiuchmi unaowasaidia kupambana na
umaskini kwa namna ambayo itawaongezea kipato.
(iii) Pamoja na kuongezeka na kushamiri kwa harakati za kujiajiri, ajira katika sekta rasmi pia zimeongezeka. Idadi ya waajiriwa katika sekta rasmi ya umma na isiyokuwa ya u