CHAMA CHA MAPINDUZI

 

 

 

 

 

 

TAMKO LA CHAMA KUHUSU

UCHAGUZI WA SERIKALI ZA MITAA TANZANIA BARA, NOVEMBA 2004

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

Imetolewa na:-

 

Makao Makuu ya CCM

DODOMA.

Agosti 2004

 

TAMKO LA CHAMA CHA MAPINDUZI

 

SURA YA KWANZA

 

         

UTANGULIZI

 

1.                 Uchaguzi uliopita wa Serikali za Mitaa ngazi ya Vitongoji, Vijiji na Mitaa ulifanyika Novemba, 1999.  Chama Cha Mapinduzi kilipata ushindi mkubwa sana.  Wananchi walionyesha imani yao wazi wazi kwa kuipa CCM ushindi wa asilimia tisini na tano (95%).  Viongozi wa Vitongoji, Vijiji na Mitaa waliochaguliwa mwaka 1999 wakiungwa mkono na Halmashauri zao na Serikali Kuu wameweza kuwashirikisha wananchi katika jitihada za kusukuma maendeleo ya kiuchumi na kijamii na kujenga mazingira muafaka ya utawala wa kidemokrasia.

 

2.                 Ushindi mkubwa wa CCM katika uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa mwaka 1999 uliweka jukwaa la kuandaa ushindi wa kishindo wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa Madiwani, Wabunge, Wawakilishi na wa Rais wa mwaka 2000.  Ndiyo maana, kwa mtazamo huo huo, CCM inayapa uzito na umuhimu mkubwa wa kipekee maandalizi ya sasa ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba, 2004.

 

3.                 Lengo na dhamira ya CCM ni kuona kwamba tunapata ushindi wa kupigiwa mfano katika mwezi Novemba mwaka huu wa 2004 ili utufagilie njia ya kupata ushindi wa kishindo kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2005.

 

4.                 Chama Cha Mapinduzi kinatoa Tamko ili kuwaomba wapiga kura katika Vitongoji, Vijiji na Mitaa kuwachagua wagombea wa CCM katika nafasi za uongozi katika uchaguzi ujao wa Serikali za Mitaa.

 

5.                 Chama Cha Mapinduzi kinaamini kwamba chenyewe ndicho Chama peke yake nchini ambacho kwa sasa kinastahili kuendelea kuaminiwa na wananchi kwa kupewa dhamana ya kuongoza Serikali za Mitaa za Vitongoji, Vijiji na Mitaa kwa hoja zifuatazo:-

 

(a)  Ndicho Chama pekee chenye mtandao na uhai kwenye Vitongoji, Vijiji na Mitaa na hivyo, kinayaelewa na kuyajua matatizo ya wananchi yalivyo huko.  Kutokana na ukweli huo, CCM ndicho Chama kinachostahili kupewa dhamana ya kuziongoza Serikali hizo za Mitaa.

 

(b) Ndicho Chama pekee chenye uzoefu wa kuongoza na kuendesha Serikali za Mitaa na uzoefu ambao umetoa matunda yanayoonekana.  Hakuna Chama kingine ambacho kina uzoefu kama  huo.

 

(c)  Ndicho Chama pekee chenye Sera sahihi juu ya Serikali za Mitaa.  Sera hii ni ya kupeleka madaraka kwa wananchi Vitongojini, Vijijini na kwenye Mitaa na kujenga utawala wa demokrasia shirikishi.

 

(d) Aidha, Sera ya CCM ya kujitegemea inaenda sambamba na Sera ya kupeleka madaraka na maamuzi kwa wananchi wenyewe pale walipo.  Hivyo, kuiweka CCM madarakani ni kuwa na uhakika kuwa wananchi wataendelea kuimarisha kujitawala wenyewe na kujitegemea.

 

6.     Nchi yetu bado iko nyuma na maskini.  Serikali ya Awamu ya Tatu imefanikiwa kuanzisha mchakato wa kuitoa nchi yetu pale tulipokuwa mwaka 1995 na kutuingiza katika mkondo wa maendeleo endelevu.  Ili tupige hatua zaidi tunahitaji kuendelea kuwa na Serikali Kuu imara na adilifu yenye uwezo wa kusukuma na kuchochea ukuaji wa uchumi, na hali kadhalika Serikali za Mitaa adilifu na zenye utawala wa kidemokrasia, zinazowaongoza wananchi wanaochapa kazi kwa bidii na maarifa kwa kujitegemea.  Haya yatapatikana wananchi wakiichagua tena CCM kuziongoza Serikali za Mitaa katika Vitongoji, Vijiji na Mitaa.

 

 

 

 

 

 

 

             

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

SURA YA PILI

 

SERA YA MSINGI YA CCM KUHUSU SERIKALI ZA MITAA

 

7.          Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 hadi 2010 kwa kiasi kikubwa ulikuwa ni mwendelezo wa Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya Tisini.  Mwelekeo wa Miaka ya Tisini ulibainisha mtazamo wa jumla na dhamira za msingi za CCM kuhusiana na Serikali za Mitaa kama ifuatavyo:-

 

“… Serikali za Mitaa ni sehemu ya msingi ya madaraka ya umma kwa vile ni Taasisi zinazowezesha wananchi kujitawala wenyewe kidemokrasia … kwamba, Serikali za Mitaa ni chombo chao ambacho kinahitaji dhamira yao ya hali na mali, kwa hiyo wasingojee Serikali zao kuwaendeleza wao bali wazitumie Serikali hizo kujiendeleza wenyewe”.

 

8.       Kwa upande wake, Mwelekeo wa Sera za CCM katika Miaka ya 2000 – 2010   unakiri usahihi wa msimamo na dhamira hiyo ya CCM kutokana na uzoefu uliopatikana katika utekelezaji wa sera hiyo.  Baada ya kukiri hayo, Mwelekeo huo unasisitiza juu ya suala la Uwajibikaji wa Serikali za Mitaa kwa wananchi, na umuhimu wa Serikali Kuu kuziwezesha Serikali hizo kuwa kichocheo cha maendeleo na kupambana na umaskini.  Mwelekeo wa Sera za CCM Katika Miaka ya 2000 hadi 2010 unasema ifuatavyo katika ibara zake za 88 na 89:-

 

“Uzoefu umedhihirisha umuhimu wa Serikali za Mitaa kama chombo cha wananchi cha kuwashirikisha katika utawala wa umma…. Zimefanyika juhudi za makusudi … kuongeza uwajibikaji kwa wananchi.  CCM itahakikisha kuwa uwajibikaji huo kwa wananchi unaongezeka zaidi.” (Ibara ya 88); na

 

“CCM inaipongeza Serikali ya Awamu ya Tatu kwa kuanzisha Mpango wa uboreshaji wa Serikali za Mitaa.  Pamoja na kuziwezesha Serikali za Mitaa kutoa huduma za jamii, Mpango huo usisitize pia kuziwezesha Serikali za Mitaa kuwa kichocheo cha maendeleo ya wakazi wa maeneo yao na kufuta umaskini.  Lazima tujenge Serikali za Mitaa zinazowajibika”. (Ibara ya 89)

 

9.       Kwa hiyo, kwa ujumla wake, sera ya msingi ya CCM kuhusiana na Serikali za Mitaa inaweza kuelezewa katika matamko yafuatayo ya kisera:

 

(a)              CCM inazitambua Serikali za Mitaa kuwa chombo cha wananchi cha kuwashirikisha katika utawala wa umma;

 

(b)             CCM inazitambua Serikali za Mitaa kuwa chombo cha kuwahamasisha, kuwasaidia na kuwawezesha wananchi kujiletea maendeleo ya kiuchumi na kijamii katika maeneo yao;

 

(c)              CCM inazitambua Serikali za Mitaa kuwa ni kichocheo cha dhamira na jitihada za kupambana na  umaskini miongoni mwa wananchi;

 

(d)             CCM inawaongoza wananchi katika mtazamo wa kuzitumia Serikali za Mitaa kama nyenzo katika kujiletea wenyewe maendeleo na kupambana na umaskini badala ya kuzisubiri ziwaletee maendeleo na kuwaondolea umaskini;

 

(e)      CCM inazitambua changamoto zinazozikabili Serikali za Mitaa katika Karne ya 21 ambazo ni kupambana na umaskini, kuhakikisha matumizi endelevu ya rasilimali, kukuza uchumi na kuwajengea wananchi uwezo wa kutumia fursa zilizopo katika kujiendeleza wenyewe; na

 

(f)      CCM itaendelea kuhakikisha kuwa Serikali Kuu inaendelea kuziwezesha Serikali za Mitaa katika kupambana na changamoto zinazozikabili katika kutekeleza majukumu ya kuwatumikia wananchi kupitia Mpango wake wa Uboreshaji wa Serikali za Mitaa na mipango mingine.

 

10. Sera hiyo ndiyo iliyokuwa mwongozo wakati wa kuandaa Ilani za Uchaguzi za 1995 na 2000 vilivyohusu Serikali za Mitaa.  Katika Ilani ya 1995, ibara ya 28 inaelezea dhamira na mikakati ya kuimarisha Serikali za Mitaa.  Zipo pia ibara nyingine za Ilani hiyo zilizogusia masuala ya Serikali za Mitaa.  Kwa mfano, ibara ya 24, hasa sehemu yake ndogo ya (vi) iliyozipa Serikali hizo jukumu la kuhakikisha zinakuwa na mikakati ya kupambana na umaskini.  Kwa upande wa Ilani ya 2000, ibara ya 90 ndiyo inayolenga zaidi Serikali za Mitaa hasa sehemu yake ndogo ya (vi) ambayo inazungumzia:

 

“kuziwezesha Serikali za Mitaa kupanga mipango itakayoongeza mapato yatakayosaidia kutoa huduma bora za jamii na kuwa kichocheo cha maendeleo ya wakazi wa maeneo yao na kufuta umaskini.”

 

11.       Sera na mikakati hiyo ya utekelezaji ndiyo itaendelea kuongoza 

Serikali za Mitaa zitakazochaguliwa na wananchi baada ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa wa Novemba 2004.

SURA YA TATU

 

MAFANIKIO YA KIUCHUMI, KIJAMII NA KISIASA KATIKA

KIPINDI CHA AWAMU YA TATU YA UONGOZI WA CCM

 

12.          Serikali ya awamu ya tatu ilipoingia madarakani Oktoba, 1995 iliyatambua matatizo yaliyokuwa yanaikabili nchi yetu ambayo ni pamoja na uwezo mdogo wa Serikali katika kutoa huduma.  Kwa hiyo kazi kubwa iliyoikabili Serikali katika kipindi hiki ni kubuni mikakati  mbalimbali ya kusukuma na kuchochea maendeleo ya kiuchumi, kijamii na kisiasa.  Mikakati hiyo imeleta mafanikio katika nyanja zifuatazo:

 

Mafanikio katika  Uchumi

 

(a)      Ukuaji wa Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 3.6 mwaka 1995, hadi kufikia kilele cha asilimia 6.2 mwaka 2002.  Kutokana na ukame ulioikumba nchi yetu, Pato la Taifa lilikua kwa asilimia 5.6 mwaka 2003.

 

(b)     Mfumuko wa bei umeshuka kutoka asilimia 27.1 mwaka 1995, hadi asilimia 4.4 mwaka 2003. 

 

(c)      Ujazi wa fedha umedhibitiwa na hivyo kuchangia katika kushuka kwa mfumuko wa bei na kuwafanya watu wajitume zaidi katika kutafuta pesa kwa njia halali.

 

(d)     Uzalishaji viwandani na katika mashirika sasa ni wa ufanisi mkubwa kufuatia mafanikio ya utekelezaji wa sera ya ubinafsishaji.  Baada ya kubinafsishwa, makampuni na mashirika hayo yanaipatia Serikali mapato makubwa badala ya kuendeshwa kwa ruzuku ya Serikali.

          Ubinafsishaji umeweza kuiondolea Serikali mzigo mzito wa kuendesha uchumi moja kwa moja.  Aidha umeanza kujenga mazingira ya ongezeko la tija katika uzalishaji wa bidhaa za viwandani. 

 

(e)      Mauzo ya nje ya bidhaa yameongezeka kutoka Dola 682.9 milioni mwaka 1995 hadi Dola 1,142.4 milioni mwaka 2003. 

 

(f)      Akiba ya fedha za kigeni kwa ajili ya kuagizia bidhaa kutoka nje imeongezeka kutoka uwezo wa kukidhi mahitaji ya mwezi 1.6 mwaka 1995 hadi mahitaji ya miezi 8.9 mwaka 2003.

 

(g)     Ruzuku ya Serikali Kuu kwa Serikali za Mitaa imeongezeka mara 24 kutoka Shilingi 12.3 bilioni mwaka 1995/96 hadi shilingi 292.0 bilioni mwaka wa 2003/04.

 

(h)     Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kuweka mazingira mazuri ya kuvutia vitega uchumi na kupambana na rushwa, hivi sasa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoongoza katika Afrika kuhusu kuvutia uwekezaji.

 

(i)                Kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mikakati ya kupambana na rushwa na kuziba mianya ya ukwepaji wa kulipa kodi pamoja na zoezi la ubinafsishaji wa mashirika ya umma hatua ambayo imeboresha uzalishaji, makusanyo ya mapato ya Serikali yameongezeka kwa zaidi ya mara nne.  Makusanyo hayo yameongezeka kutoka wastani wa Shilingi 25 bilioni kwa mwezi mwaka 1995 hadi wastani wa Shilingi 120 bilioni kwa mwezi, mwaka 2004.

 

(j)      Tanzania ilitimiza masharti ya Mpango wa Kuzifutia Madeni Nchi zenye Madeni Makubwa na hivyo kuingizwa katika Mpango huo mwaka 2000.  Kutokana na hali hiyo kuanzia mwaka 2000 Tanzania imekuwa ikitekeleza Mkakati wa Kupunguza Umaskini kwa maana fedha ambazo zingetumika kulipia madeni ya nje (ambayo yamefutwa) sasa zinaelekezwa katika sekta teule za huduma za jamii na miundombinu ya kiuchumi zinazomgusa moja kwa moja mwananchi wa kawaida.  Sekta hizo ni elimu, afya, maji, barabara za vijijini, kilimo, na utawala bora.

 

(k)      Katika kipindi hiki Sekta ya Utalii imekua kwa kasi kubwa na kutoa mchango mkubwa katika kuliingizia Taifa letu fedha za kigeni.  Hii imetokana na juhudi za makusudi za Serikali za kuipa msukumo wa pekee sekta hii na hasa katika kuitangaza nje na ndani na kuboresha miundombinu inayosaidia ukuaji wake ikiwa ni pamoja na kuboresha barabara ziendazo kwenye hifadhi mbalimbali za kitaifa.  Kumekuwepo pia juhudi za kuibua maeneo mapya ya utalii kama vile Kilwa na Kitulo. Idadi ya watalii walioingia nchini imeongezeka kutoka watalii 295,000 mwaka 1995 hadi 576,000 mwaka 2003.  Aidha mapato yatokanayo na utalii nayo yameongezeka kutoka dola 259 milioni mwaka 1995 hadi dola 731 milioni mwaka 2003.

 

(l)      Uuzaji wa madini nje umeongezeka kutoka Dola 26.37 milioni mwaka 1998 hadi Dola 548.30 milioni mwaka 2003.  Dhahabu imechangia zaidi ya asilimia 90 ya thamani ya madini yote yaliyouzwa nje.  Aidha  upanuzi katika Sekta ya madini umeongeza ajira kwa wananchi katika maeneo mengi.  Katika maeneo mengi wenye migodi hiyo wamechangia katika kuboresha huduma za jamii na miundo mbinu.

 

Mafanikio katika Maendeleo ya Jamii

 

13.          Kuboreka kwa huduma mbali mbali za kijamii na kiuchumi ni miongoni mwa manufaa ya kukua kwa uchumi wa Taifa ambayo wananchi wa kawaida vijijini na mijini wameanza kuyafaidi kwa pamoja.  Kutokana na kuimarika kwa uchumi wa Taifa na kuongezeka kwa makusanyo ya mapato ya Serikali, imewezekana kwa Serikali kuongeza kwa kiwango kikubwa rasilimali ilizozielekeza katika huduma hizi ambazo ni zana za msingi katika kupambana na umaskini.

 

14.            Mpango wa TASAF kwa kushirikiana na wananchi umeleta mafanikio makubwa katika maeneo ya elimu, afya, barabara za vijijini, maji n.k.  Mpango huo ambao ulianza na wilaya 40 za majaribio, sasa utakuwa wa nchi nzima.

 

Huduma za Jamii

 

Elimu

 

Sekta ya elimu ya msingi imepiga hatua kubwa kama ifuatavyo:-

 

(i)                Kufutwa kwa ada za shule za msingi mwaka 2002/2003   kumewezesha kuongezeka kwa idadi ya wanafunzi wa shule za msingi kutoka 3,877,643 mwaka 1995 hadi 7,083,063 mwaka 2004. Idadi ya watoto walioandikishwa darasa la kwanza kuanzia mwaka 2000 kwa kila mwaka  ni kama ifuatavyo:-

 

·        2000 -    897,569

·        2001 - 1,140,554

·        2002 - 1,632,141

·        2003 - 1,481,354

·        2004 - 1,368,315

 

Mwaka 2004 watoto 1,368,315 wameandikishwa darasa la kwanza sawa na asilimia 83.4 ya lengo la 1,640, 969. Kati ya walioandikishwa wavulana 697,594 na wasichana 670,721.  Kati yao shule za Serikali watoto 1,361,446  na  shule binafsi watoto 6,869.

 

(ii)              Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Msingi (MMEM) ulioanza kutekelezwa mwaka wa 2002 umekwishaleta mabadiliko makubwa ya sura za shule za msingi nchi nzima.  Majengo mengi ya shule yamekarabatiwa na mengine mengi mapya yamejengwa.

 

(iii)            Katika mwaka 2003, kulifanyika ujenzi wa madarasa 13,342; ofisi za walimu 226; nyumba za walimu 997; vyoo vya shimo 14,700; na kuajiri walimu wapya 15,921 ili kukabiliana na ongezeko la wanafunzi na kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia.  Serikali katika kuhakikisha kwamba mapengo ya walimu katika baadhi ya shule za msingi na sekondari yanazibwa imeajiri walimu 37,261 kati ya mwaka 2000 na 2004.  Miongoni mwao, walimu 15,000 ni wale waliokuwa wamekosa ajira baada ya kumaliza mafunzo ya ualimu miaka ya nyuma.  Kwa hiyo kero ya walimu 15,000 wenye vyeti bila kuwa na ajira imemalizika.

 

(iv)            Kutokana na mafanikio mazuri ya kusisimua ya Mpango wa MMEM Serikali imeanza kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari (MMES).  Tayari Serikali imepunguza ada  ya shule za sekondari za kutwa za Serikali kwa asilimia 50 wakati hatua nyingine za kukarabati na kujenga majengo ya Sekondari nchi nzima zinaendelea.

 

Afya

 

Sekta ya Afya nayo imekuwa na mafanikio makubwa kama ifuatavyo:-

 

(i)                Chanjo  za watoto chini ya umri wa miaka mitano zimefikia asilimia 90 na hivyo kuvuka kiwango cha kimataifa cha asilimia 80 katika mwaka wa 2003. Chanjo ya Kifua Kikuu ilifikia asilimia 88, polio asilimia 91, kifaduro, pepopunda na homa ya ini asilimia 89, na surua asilimia 89.

 

(ii)              Serikali imeanzisha sera ya bima ya afya ili kuwawezesha wafanyakazi wa sekta ya umma kukabiliana na gharama za tiba.  Kwa ajili ya wananchi wa kawaida Serikali imeanzisha Mifuko ya Afya ya Jamii.

 

(iii)            Ukarabati  mkubwa wa hospitali kuanzia Hospitali ya Taifa Muhimbili mpaka hospitali za Wilaya umekamilika au uko katika hatua mbalimbali za utekelezaji.  Mashine za “X-Ray” na “Ultrasound” na jenereta zimefungwa katika hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa.

 

(iv)            Katika harakati za kuboresha utoaji wa huduma za afya, kumekuwa na ongezeko kati ya mwaka 2000 hadi 2003  la mtandao mzuri wa vituo vya kutolea huduma nchi nzima kama ifuatavyo:-

 

·        Hospitali  kutoka 224  hadi 249

·        Vituo vya Afya kutoka 459 hadi 574

 

Nguvu za wananchi na halmashauri zimetumika katika kujenga:-

 

·        Zahanati 233 na

·        Vituo vya afya 16

 

(v)              Serikali imefuta kodi kwenye vyandarua na bidhaa zinazosaidia vita dhidi ya malaria.  Hali hiyo imesaidia sana kupunguza maambukizo ya malaria hasa kwa akina mama wajawazito na watoto wachanga.

 

(vi)            Programu kabambe ya kukabiliana na janga la ukimwi imeanzishwa na inatekelezwa.

 

Maji Mijini na Vijijini

 

Ukosefu wa maji safi na salama ni kero ambayo inaendelea kushughulikiwa na Serikali kwa kushirikiana na wahisani, asasi zisizo za kiserikali na wananchi wenyewe.  Mafanikio ya Sera ya Taifa ya Maji yamejionyesha katika maeneo yafuatayo:-

 

(i)                Hadi kufikia Desemba 2003 kamati za Maji 8,368 zimeanzishwa na kati ya hizo 7,226 zilikuwa na mifuko ya maji yenye thamani ya Sh. 13 bilioni.

 

(ii)              Idadi ya wakazi mijini wanaopata huduma ya maji safi na salama imeongezeka kutoka asilimia 68 mwaka 1998 hadi asilimia 73 mwaka 2003.

 

(iii)            Idadi ya wananchi vijijini wanaopata maji safi na salama imeongezeka kutoka asilimia 48 mwaka 1995 hadi asilimia 53 mwaka 2003.

 

(iv)            Makusanyo ya mapato ya mamlaka za Maji Mijini yaliongezeka kutoka Sh. 400 milioni mwaka 1995 hadi Sh. 13.4 bilioni mwaka 2003. Ongezeko hili linatoa fursa kwa mamlaka hizi kuboresha huduma wanazotoa.

 

(v)              Pamoja na miradi midogo midogo inayoendelea, Serikali inashughulikia miradi mikubwa ambayo ni pamoja na mradi wa maji toka Ziwa Victoria kwenda Wilaya za  Shinyanga Mjini na Kahama, mradi wa maji wa Chalinze katika Mkoa wa Pwani, mradi kabambe wa Jiji la Dar es Salaam nakadhalika.

 

Huduma za Kiuchumi

 

Barabara

 

(i)                Toka mwaka 2001, Serikali imekuwa ikitenga Sh.1.8 bilioni kila mwezi kwa ajili ya ujenzi wa barabara nchini.  Fedha hizo kwa pamoja na zile za road toll na za wahisani, zimewezesha kuboresha kwa kiwango kikubwa mtandao wa barabara kuu na za vijijini nchi nzima.

 

Mawasiliano

(ii)              Tanzania katika kipindi hiki imeshuhudia ongezeko kubwa la mtandao wa mawasiliano, hasa simu za mikononi.

 

Umeme

(iii)            Katika Ilani ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 2000, Chama Cha Mapinduzi kilitoa ahadi ya kuendelea kushughulikia suala la usambazaji wa umeme katika miji mikuu ya Wilaya iliyobaki ambayo idadi yake ilikuwa 18.  Hadi Julai, 2004 miji mikuuu ya Wilaya 8 imepatiwa umeme.  Nayo ni: Geita, Igunga, Mbarali, Meatu, Mkuranga, Ruangwa, Tandahimba na Sikonge.  Hadi kufikia mwaka 2005 miji mikuu ya Wilaya za Biharamulo, Ngara, Rufiji, Serengeti, Ukerewe na Urambo itakuwa imepatiwa umeme.  Aidha hatua za awali zimeanza kuchukuliwa ili kuanza utekelezaji wa mradi wa kufikisha umeme katika miji iliyobaki ya Bukombe, Kilindi na Simanjiro.

 

16.          Serikali itaendelea kuweka mazingira bora, lakini tegemeo kuu la kukua kwa uchumi wetu ni pamoja na kuongezeka kwa kiwango cha uwekaji akiba, kuongeza kasi ya ongezeko la mitaji, kuongeza kasi ya mauzo nje, na wananchi wenyewe kufanya kazi kwa bidii, maarifa na ubunifu.

 

Mafanikio  ya Kisiasa

 

Utengamano wa Kisiasa

 

17.          Mazingira yaliyosababisha mafanikio haya makubwa ya kiuchumi na kijamii ni kuwepo kwa amani na utulivu wa kisiasa nchini. Serikali ya CCM ya Awamu ya Tatu imeweza kuendelea kujenga na kudumisha hali ya amani na utulivu kwa kipindi chote cha uongozi wake tangu ilipoingia madarakani mwaka 1995.

 

18.          Rushwa imendelea kupungua baada ya mianya mingi ya rushwa kuzibwa.  Katika tathmini za Kimataifa, Tanzania sasa imeondoshwa katika kundi la nchi zinazoongoza kwa rushwa duniani na Afrika. 

 

Kupanuka na kuimarika kwa Demokrasia na Utawala Bora

         

19.     Katika kipindi hiki demokrasia imepanuka na kuimarika katika nyanja za uhuru wa kuabudu, kutoa maoni, kuanzisha asasi zisizo za kiserikai na uhuru katika nyanja mbalimbali zinazowagusa wananchi vikiwemo vyombo vya habari, vyama vya siasa na kuanzishwa kwa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora nakadhalika.  Kupanuka na kuimarika huku kwa demokrasia kumechangia kwa kiwango kikubwa kuimarisha amani na utulivu.

 

20.     Kwa ujumla manufaa ya ukuaji wa uchumi, pamoja na ukuaji wa huduma za jamii ni mafanikio dhahiri katika kukua kwa amani na utulivu na kupanuka kwa demokrasia, na utawala bora. Hayo yote yameweza kuwafikia wananchi kwa njia mbalimbali ambazo zinazidi kuongezeka na mpya kubuniwa.   Kwa kiasi kikubwa mafanikio hayo yamewezekana kupitia Sera ya CCM ya Ushirikishaji wa Wananchi Katika Maendeleo yao.

 

21.     Katika utekelezaji wa sera hiyo ya ushirikishaji wa wananchi, hasa katika eneo la kupambana na umaskini, Serikali Kuu inaitambua nafasi ya Serikali za Mitaa katika kusimamia  na kuratibu utekelezaji huo.  Ndiyo maana Serikali Kuu imechukua hatua za  makusudi kuziwezesha Serikali hizo kutekeleza kwa ufanisi jukumu hilo kwa manufaa ya wananchi. 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

SURA YA NNE

 

KUPAMBANA NA UMASKINI NA

UWEZESHAJI WA WANANCHI

 

Kupambana na Umaskini

 

22.     Katika Mwelekeo wa Sera za CCM za Miaka ya Tisini Ibara ya 31 umefanyika uchambuzi wa kina kuhusu Sekta ya Wananchi Wazalishaji Mali na Wafanyabiashara Wadogo.  Uchambuzi huu ambao bado ni sahihi kwa Chama Cha Mapinduzi, umebainisha hali halisi inayoikabili sekta hii, kwamba wananchi wetu walio wengi wanaendelea kupata riziki zao wakiwa wazalishaji na wafanyabiashara wadogo wadogo katika kilimo, uvuvi na ufugaji, viwanda vidogo  biashara na huduma mbali mbali.  Zaidi ya hayo,  CCM  ilitambua kwamba sekta hii ilikuwa inakabiliwa na vikwazo vingi ikiwa ni pamoja na urasimu wa kupata mikopo,  leseni, mahali pa kufanyia kazi, ukosefu wa mafunzo ya kuongeza ujuzi wa shughuli zao, na ukosefu wa masoko ya bidhaa zao.

 

23.     Sera za Chama Cha Mapinduzi za kupambana na umaskini zimeweka bayana mikakati inayoelekeza nini kifanyike katika kufanikisha mapinduzi katika kilimo, ufugaji na uvuvi.  Licha ya juhudi zilizofanyika hadi sasa, kilimo, ufugaji na uvuvi wetu bado havijawa vya kisasa kwa sababu havitumii sayansi na teknolojia. Hivyo mikakati ifuatayo itatekelezwa katika kuleta mabadiliko hayo:-

 

Kilimo

 

24.     Ili kuondokana na hali hiyo, msisitizo mkubwa utaendelea kuwa wa           kumwezesha mkulima kutoka katika kilimo cha jadi na kuingia katika kilimo cha kisasa kinachozingatia:-

 

(i)                Kanuni za kilimo bora.

 

(ii)              Matumizi ya samadi, mboji na mbolea ya viwandani.

 

(iii)            Kueneza matumizi ya majembe ya kukokotwa na ng’ombe na punda nchini kote, pamoja na kutumia matrekta.

 

(iv)            Kueneza matumizi ya mikokoteni inayovutwa na wanyamakazi badala ya mizigo kuendelea kubebwa na binadamu hususani wanawake.

 

(v)              Kuendelea kutumia mashine na teknolojia mbalimbali za kilimo na  kuhakikisha kuwa mashine zinatumika zaidi katika  kuchakata mazao ili kuyaandaa kwa ajili ya soko la ndani na nje ikiwa ni mkakati wa kuyaongezea thamani.