Pongezi za Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi kwa Mheshimiwa Getrude Ibengwe Mongella kwa Kuchaguliwa kwa Kura nyingi kuwa Rais wa Kwanza wa Bunge la Afrika
Katika kikao chake kinachoendelea,
Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama Cha Mapinduzi leo imetoa
pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Getrude Ibengwe Mongella kwa kuchaguliwa kwa kura
nyingi kuwa Rais wa Kwanza wa Bunge la Afrika hapo tarehe 18 Machi, 2004.
Ushindi wake huo mkubwa na wa
kishindo si wake peke yake bali pia ni wa Taifa zima na Watanzania wote. Kuchaguliwa huko kwa Mheshimiwa Mongella ni
kielelezo cha kutosha cha imani waliyonayo Wabunge wa Bunge la Afrika
kwake. Kwa vile Wabunge hao
wanawakilisha Waafrika, basi imani hiyo ni ya Waafrika wote.
Aidha, ushindi huo mkubwa alioupata
Mheshimiwa Mongella ni kielelezo kingine dhahiri cha heshima iliyonayo Tanzania
katika Bara la Afrika na Jumuiya ya Kimataifa kwa jumla.
Chama Cha Mapinduzi kinafahari kubwa
kwa imani hiyo iliyoonyeshwa na Bara la Afrika kwa mwanachama wake huyo mahiri
na mzoefu wa kisiasa na shughuli za Kimataifa.
Huu ni ushahidi wa jinsi CCM ilivyo
na hazina kubwa ya viongozi wenye busara na upeo unaoheshimika Kimataifa.
Kamati Kuu pia imewapongeza Ndugu
Emmanuel Nchimbi na Abioud Mugini Maregesi kwa kuchaguliwa kuwa Wenyeviti wa
Jumuiya za VIJANA na WAZAZI.
Ndugu Nchimbi alichaguliwa na
Mkutano Mkuu wa VIJANA uliofanyika Dodoma tarehe 28 Februari, 2004 na Ndugu
Maregesi alichaguliwa na Mkutano Mkuu wa WAZAZI uliofanyika pia Dodoma, tarehe
6 Machi, 2004.
Kamati Kuu imewapongeza pia waliochaguliwa
kuwa Makamu Wenyeviti wa Jumuiya hizo, Ndugu Amina Iddi Mabrouk (VIJANA) na
Ndugu Ramadhani Suleiman Nzori (WAZAZI).
Kamati Kuu imewatakia heri na fanaka
viongozi hao na wenzao wote waliochaguliwa katika nafasi mbali mbali za Jumuiya
hizo na kuwataka wote waelekeze nguvu zao katika kuhakikisha ushindi wa CCM
katika Uchaguzi Mkuu wa Dola mwaka 2005.
Omar R. Mapuri (Mb.),
KATIBU MWENEZI WA CCM TAIFA
19/03/2004