MAPAMBANO DHIDI YA RUSHWA

 

 

Chama Cha Mapinduzi kimekwisha toa Toleo la 3 la Jarida la Mkereketwa ambalo linafuatana na jarida dogo la Mafanikio ya Sekta ya Elimu.  Majarida hayo hivi sasa yamo kusambazwa katika matawi na ofisi nyingine za CCM, taasisi mbali mbali na kwa walengwa wengine.

 

Miongoni mwa mambo yaliyomo katika toleo hili la Mkereketwa ni:-

Hata hivyo, mada kuu ya toleo hili ni Mapambano Dhidi ya Rushwa.  Mada hiyo imezungumziwa katika Tahariri na makala nyingine mbili.  Katika makala hizo, miongoni mwa mengine tumejenga hoja na kuonyesha yafuatayo miongoni mwa mengine.

 

(a)               Kuziba mianya ya rushwa (yaani kutumia falsafa ya kinga ni bora kuliko tiba)

(b)               Kuwachukulia hatua wanaothibitika kujihusisha na rushwa.

(a)               Kuundwa kwa TRA na marekebisho ya sheria za kodi kumewezesha kuzibwa kwa mianya mingi ya ukwepaji kodi inayoambatana na rushwa.  Matokeo yake ni kwamba makusanyo ya kodi na mapato mengine ya Serikali yameongezeka zaidi ya mara nne.

(b)               Marekebisho ya Sheria za Fedha na za Manunuzi Serikalini yamewezesha kuongezeka kwa udhibiti wa fedha na mali za Serikali.  Matokeo ni kwamba upotevu wa fedha na mali za Serikali umepungua kwa kiasi kikubwa.

(c)               Kufutwa kwa kodi ya maendeleo na kodi nyingine nyingi zilizokuwa kero na chanzo kikubwa cha rushwa, kumeziba mianya ya rushwa iliyokuwa ikiwasumbua sana wananchi.  Bila ya makelele na vishindo, rushwa zilizokuwa zimeambatana na kodi hizo zimeyeyuka na hivi sasa hakuna Mtanzania anayedaiwa rushwa za aina hiyo.

(d)               Kufutwa kwa ada ya shule za msingi na kuanzishwa kwa mpango wa MMEM, kuliziba mwanya mwingine mkubwa wa rushwa iliyokuwa ikiwasumbua wazazi.  Sasa hivi hakuna mzazi anayedaiwa rushwa kwa kumwandikisha mtoto shule 

Kwa bahati mbaya wakosoaji wengi wa Serikali kuhusu suala la rushwa, hasa wapinzani, sura hii ya vita dhidi ya rushwa hawaizungumzii; labda kwa sababu inaleta mafanikio makubwa.  Wao wamekazania ile sura ya pili tu ya kuwachukulia hatua wanaothibitika kujihusisha na rushwa.  Lakini hata katika hili, hawazungumzii cho chote kuhusu watu waliofungwa au watumishi waliofukuzwa kazi au kustaafishwa kwa manufaa ya umma baada ya kubainika kujihusisha na vitendo vya rushwa.  Badala yake wakosoaji hao wamejikita katika kuitaka Serikali iwahukumu watu kwa hisia tu, jambo ambalo ni kinyume kabisa na kanuni za msingi za utawala bora na utawala wa sheria.

 

Katika makala za Mkereketwa  kuhusu rushwa, tumetoa wito kwa wananchi washiriki kikamilifu katika vita dhidi ya rushwa, kwani pamoja na mafanikio yanayopatikana ambayo yanaashiria kupungua kwake, rushwa bado ipo nchini.  Tumetoa wito maalum wakati huu tukielekea Uchaguzi Mkuu wa 2005, kwamba wanachama wa vyama vya siasa wapambane na rushwa ndani ya  vyama vyao ili kuwazuwia wanasiasa watoa rushwa wasije wakapata nafasi za kugombea.  Aidha, tumewataka wapinzani wasidhani kwamba jukumu la kupambana na rushwa ni la CCM peke yake na wao kazi yao ni kulaumu tu.

 

Vita hivi ni vya wote, lakini vipiganwe ndani ya misingi ya Kanuni za utawala bora na utawlaa wa sheria.  Vita hivi visitumike vibaya kupakana matope na kuchafuliana majina kwa malengo ya kisiasa.  Tukifanya hivyo, rushwa hatutoiweza na badala yake tunaweza kujikuta katika vurugu.  Si sahihi kuishinikiza Serikali kuhukumu watu kwa hisia tu, kwani kama itafanya hivyo hao wanaoishinikiza watakuwa wa kwanza kuilaumu.  Ndiyo maana tunasisitiza umuhimu  wa kuwafichukua wala/watoa rushwa kwa ushahidi unaotosheleza.

 

Aidha, napenda kuongeza kwamba vita dhidi ya rushwa visitumike kudumaza ujasiriamali.  Watanzania tusiendeleze makosa tuliyoyafanya mwanzoni katika safari yetu ndefu ya kujenga ujamaa.  Itakumbukwa kwamba katika  miaka ya sitini, sabini na themanini, chuki dhidi ya ubepari iliendelezwa hadi kuchukia utajiri ambapo wajamaa wakaanza kujinasibu kwa umaskini, na ujamaa ukapewa maana ya umaskini.  Matokeo yake yakawa ni kudumaa kwa ujasiriamali.

 

Hivi sasa, katika mazingira mapya ya ujenzi wa ujamaa, tumo katika jitihada za kufufua ujasiriamali.  Na kwa lengo hilo, CCM kupitia Serikali yake imetunga Sera ya Uwezeshaji wa Wananchi, na Sheria imo kutungwa, itayaowawezesha Watanzania kujenga ujasiriamali ili waweze kuupiga vita umaskini kwa ufanisi.

 

Lakini ghafla umejitokeza mtindo wa kuwaandama viongozi wanaojitokeza kuonyesha njia na mfano katika ujasiriamali.  Kwa kutumia kisingizio cha vita dhidi ya rushwa, wanapakwa matope na kuchafuliwa majina kwa kuhusishwa na rushwa bila ya ushahidi wowote.

 

Halafu shutuma hizo zinaambatana na unafiki.  Viongozi waliopata nafasi za uongozi wakiwa matajiri wao hawaguswi. Lakini wale waliopata uongozi wakiwa maskini, wakianza juhudi za kuondokana na umaskini kwa njia halali, wanaandamwa na kukatishwa tamaa.  Hivyo katika Tanzania wenye haki ya utajiri ni matajiri tu?  Maskini akipata uongozi wajibu wake ni kuendeleza umaskini?  Na ikiwa hivyo atatoa mfano gani kwa watu anaowahubiria sera za kupiga vita umaskini?  Jambo la kuchunga wakati wote ni kuhakikisha kuwa viongozi hawajilimbikizii mali kwa kutumia nyadhifa zao.  Lakini  wasikatishwe tamaa wanapotumia kipato chao halali kujiendeleza kimaisha na kuhudumia familia zao.

 

Natoa wito kwa Watanzania waubaini na kupuuza unafiki wa baadhi ya wanasiasa.  Tusikubali kuelekezwa kwenye kuamini kuwa ujasiriamali ni ula rushwa kama tulivyofikishwa huko nyuma kuamini kuwa ujamaa ni umaskini.  Fikra kama hizo zitazidi tu kutuzamisha katika dimbwi la umaskini.

 

Tuhuma Potofu Dhidi ya Waziri Mkuu

 

Namalizia kwa kutumia fursa hii kukanusha uzushi uliochapishwa katika gazeti la Mtanzania la jana tarehe 9/8/2004 lililojaribu kutoa picha kana kwamba shamba la Kibaigwa la Mheshimiwa Waziri Mkuu Frederick Sumaye lilikuwa la Magereza.  Shamba hilo liko umbali wa zaidi ya kilomita 6 toka eneo lililokuwa likitumiwa na Magereza huko nyuma kama Kambi ya Kilimo ya Manyata chini ya Gereza la Kongwa.

 

Magereza walilitumia eneo hilo la ekari 70 kwa kuazimwa na kijiji cha Manyata toka 1980 hadi 2001 walipoifunga kambi hiyo.  Walipofunga kambi, Magereza walilirejesha eneo hilo kwa uongozi wa kijiji cha Manyata ambao nao uliwagawia wananchi ambao ndio wanaolitumia hivi sasa kujitafutia riziki zao.  Magereza hawakuwahi kulimiliki eneo hilo.

 

Ni kitendo cha kuishiwa hoja kwa Mheshimiwa Slaa, kupitia gazeti la Mtanzania, kujaribu kupotosha ukweli na kutaka Watanzania waamini kwamba shamba la Mheshimiwa Waziri Mkuu linatokana na eneo lililokuwa likitumiwa na Magereza.  Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mhe. Andrew Chenge alikwishaelezea kwa urefu Bungeni namna Mheshimiwa Frederick Sumaye na familia yake walivyolipata eneo hilo wanalolitumia kwa kukodishwa na kijiji kama inavyofanyika kwa wengi wengine wanaolima maeneo hayo.  Mwanasiasa anapoishiwa hoja ni bora akanyamaza kuliko kujaribu kujenga chuki binafsi na kupaka watu matope.

 

 

 

 

Omar R. Mapuri (Mb),

KATIBU WA NEC

ITIKADI NA UENEZI