Tamko la Chama Cha Mapinduzi kuhusu Kauli za Uchochezi za Mwenyekiti wa CUF

 

Katika gazeti la “Majira” la tarehe 27 Disemba, 2004, Chama Cha CUF kimeripotiwa kudai kupitia kwa Mwenyekiti wake, Ibrahim Lipumba, kwamba kikipokonywa ushindi katika Uchaguzi Mkuu ujao itamwagika damu.

 

Aidha, gazeti hilo limemnukuu Lipumba kwamba amesema maneno yafuatayo:-

 

Mwaka 1995 wananchi wa Zanzibar walichagua Serikali wanayoitaka wakanyang’anywa, tukakaa katika muafaka, mwaka 2000 wakachagua tena Serikali yao wakapokonywa tena, muafaka wa pili ukaja mwaka 2001, vipengele muhimu katika muafaka huo wa pili havijatekelezwa hadi sasa licha ya makubaliano ya kutekeleza muafaka huo hadi mwaka 2003.

 

Sasa iwapo hawatatekeleza na kuingia katika Uchaguzi Mkuu, na wananchi wakachagua tena Serikali yao wanayoitaka na kunyang’anywa, basi CCM ijue itaua watu wengi zaidi wasio na hatia kama ilivyotokea, kwani wananchi hawatakubali kupokonywa tena Serikali yao safari hii.”

 

·        Kwanza, kauli ya kumwaga damu ambayo ni maarufu kwa viongozi wa CUF ni mwendelezo wa kudhihirisha kiu ya damu ya Watanzania waliyo nayo viongozi hao.  La kusikitisha zaidi ni kwamba kauli hiyo inatoka mara tu baada ya Mheshimiwa Rais Benjamin William Mkapa kukemea kauli kama hizo na kuwaasa wanasiasa kuachana nazo wakati akitoa salamu zake za Krismasi kwa Watanzania.  Aidha, kauli hiyo ya Lipumba imetoka mara tu baada ya mahubiri yaliyotolewa makanisani nchi nzima yaliyokemea  kauli za shari za wanasiasa zinazochochea vurugu na uvunjifu wa  amani na kuwataka wanasiasa waachane nazo.  Mahubiri hayo yalitolewa karibu na Maaskofu, Makasisi na Wachungaji wote wakati wa ibada za Krismasi ambao walikuwa wakiiombea amani nchi yetu.  Kauli hiyo ya kumwaga damu kutoka mara tu baada ya mahubiri kama hayo ni kebehi na dharau kwa viongozi hao wa kidini wenye heshima kubwa katika jamii yetu.

 

·        Pili,  madai kwamba wananchi wa Zanzibar walipokonywa Serikali yao waliyoichagua ni uongo wa mchana tena usio na haya.  Serikali za Awamu ya 5 na 6 za CCM zilipata ridhaa ya wananchi wa Zanzibar na ndio waliozichagua na kuziweka madarakani kihalali kwa mujibu wa Sheria na Katiba.  Serikali hizo ziliingia madarakani baada ya kushinda uchaguzi na kuthibitishwa na Tume ya Uchaguzi. Hapakuwa na Serikali nyingine yo yote waliyochagua wananchi wa Zanzibar wakapokonywa.  Ni chama cha CUF tu ndicho kilichopingana na Katiba na Sheria kwa kukataa kushindwa.  Lakini chama cha CUF na wananchi wa Zanzibar ni vitu viwili tofauti.

 

·        Tatu,  madai kwamba vipengele muhimu vya muafaka havijatekelezwa ni upuuzi na upotoshaji mtupu.  Vipengele vyote muhimu vimetekelezwa.  Vipengele muhimu ni vile vilivyohitaji marekebisho ya Katiba na Sheria.  Hakuna asiyejua kwamba:-

 

(a)            Marekebisho ya 8 na 9 ya Katiba ya Zanzibar yamefanywa kutokana na matakwa ya Muafaka.

 

(b)            Imetungwa Sheria ya Tume ya Muafaka.

 

(c)             Sheria ya Uchaguzi ya Zanzibar imefanyiwa marekebisho katika kukidhi matakwa ya Muafaka.

 

(d)            Kutokana na marekebisho hayo ya Katiba na Sheria, hatua kubwa kubwa zifuatazo miongoni mwa nyingi nyinginezo za utekelezaji wa muafaka zimeweza kuchukuliwa:-

 

(i)                           Kuundwa upya kwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ambapo uteuzi wa wajumbe wake umeshirikisha wapinzani, hususan CUF;

 

(ii)                         Kuundwa kwa Tume ya Muafaka yenye wajumbe kutoka CCM na CUF;

 

(iii)                       Ofisi ya Mwendesha Mashitaka imeanzishwa Zanzibar;

 

(iv)                       Kufanyika kwa uchaguzi mdogo mwaka 2003;

 

(v)                         Kuanzishwa kwa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura.

 

Vipengele vichache vya muafaka vilivyobaki ni vya matokeo tu (consequential) na haviwezi kuwa na uzito wa umuhimu sawa na hivyo vya msingi vilivyogusiwa hapo juu.  Vipengele kama vya ulipaji wa fidia vinahitaji fedha ambazo hazipo.  Hata baadhi ya viongozi wenyewe wa CUF wamesaidia kuzifuatilia fedha hizo kwa wahisani waliokuwa wameahidi bila ya mafanikio.

 

·        Nne, madai ya Lipumba kwamba CCM iliwahi kuua watu wasiokuwa na hatia na kwamba eti itaua wengine zaidi, hizi ni tuhuma nzito ambazo lazima azithibitishe, vinginevyo CCM italazimika kuchukua hatua za kisheria dhidi yake.  Kwanza tunazikanusha vikali tuhuma hizo.  CCM ni chama ambacho hupitisha maamuzi yake kwenye vikao.  Wakati tunakanusha vikali tuhuma hizo, tunamtaka Lipumba ni lazima awaambie Watanzania ni vikao gani hivyo vya CCM vilivyopitisha maamuzi ya kuua watu na vilikaa lini na wapi?

 

Kauli hiyo ya Lipumba ni ya kukichafulia jina na kukivunjia heshima Chama Cha Mapinduzi ambacho kinaheshimika ndani na nje ya nchi yetu kama chama pekee nchini kinachohubiri sera za amani, utulivu, umoja na mshikamano wa kitaifa.  Kamwe hakiwezi kuachia heshima yake ivurugwe hivi hivi tu na wanasiasa muflis wa sera zenye matumaini kwa Watanzania kiasi cha kuishia kwenye sera za vitisho na kiu ya kumwaga damu.

 

Tunamtaka Lipumba aiombe radhi CCM kama kweli ametamka maneno aliyonukuliwa na Majira au akanushe kama hakuyatamka.  Vinginevyo, CCM italazimika kwenda kutafuta haki yake ya kusafishwa jina lake na heshima yake kwenye vyombo husika vya sheria.

 

 

 

 

 

Omar R. Mapuri (Mb.),

KATIBU WA NEC

ITIKADI NA UENEZI